TBA WATAKIWA KUJITATHIMINI UPYA KUHUSU MATUMIZI YA FEDHA KATIKA MIRADI


Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi) Arch. Elius Mwakalinga, akifafanua jambo mara baada ya kikao kazi chake na Mameneja wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), mkoani Dodoma.

************************************

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi) Arch. Elius Mwakalinga, amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kufanya uchunguzi kuhusiana na utekelezaji wa miradi ya ujenzi inayosimamiwa na wakala huo katika mikoa mitano ili kujiridhisha na matumizi ya fedha katika miradi hiyo.

Ameitaja mikoa hiyo  kuwa ni Kigoma, Kagera, Njombe, Ruvuma na Dar es Salam ambayo imekuwa ikilalamikiwa mara kwa mara kuwa miradi yake haikamiliki kwa wakati na gharama zake kuongezeka hivyo kusababisha kuenda kinyume na kasi inayotarajiwa na Serikali.

Hakikisheni katika kipindi cha mwezi mmoja ninapata taarifa ya utekelezaji wa miradi katika mikoa hiyo mitano na mikoa mingine na hatua za kuchukua kwa wale wote watakaokuwa wamehusika na changamoto za ucheleweshaji wa miradi husika
 Arch. Mwakalinga.

Aidha, Katibu Mkuu huyo amewataka Mameneja wote wa TBA kufanya kazi zao kwa uadilifu na umahiri ili kuiwezesha Taasisi hiyo ya Serikali kutimiza malengo ya kuanzishwa kwake kwa kuhakikisha nyumba zinazojengwa na kumilikiwa zinakuwa katika viwango bora vya matumizi wakati wote.



"Tunao wataalamu wengi TBA hivyo meneja atakayeonekana kushindwa kumudu majukumu yake tutambadilisha mara moja ili tuweze kufikia malengo yanayotarajiwa na Serikali", amesisitiza Katibu Mkuu huyo.

Baadhi ya wafanyakazi na viongozi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), wakimsikiliza Katibu  Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi) Arch. Elius Mwakalinga (hayupo pichani), katika kikao kazi kilichofanyika mkoani Dodoma.

Naye, Mtendaji Mkuu wa TBA, Arch. Daud Kondoro, amemuhakikishia Katibu Mkuu huyo kuwa atahakikisha anatekeleza maelekezo hayo kwa wakati ili kuhakikisha uwiano wa miradi na fedha zinazotumika tba zinatumika kwa maslahi ya umma na taifa kwa ujumla.


Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Post a Comment

0 Comments