Katibu Mkuu wa Wizara ya
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi) Arch. Elius Mwakalinga,
akifafanua jambo mara baada ya kikao kazi chake na Mameneja wa Wakala wa
Majengo Tanzania (TBA), mkoani Dodoma.
************************************
Katibu Mkuu wa Wizara ya
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi) Arch. Elius Mwakalinga,
amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kufanya uchunguzi
kuhusiana na utekelezaji wa miradi ya ujenzi inayosimamiwa na wakala huo katika
mikoa mitano ili kujiridhisha na matumizi ya fedha katika miradi hiyo.
Ameitaja mikoa hiyo kuwa ni Kigoma, Kagera, Njombe, Ruvuma na Dar
es Salam ambayo imekuwa ikilalamikiwa mara kwa mara kuwa miradi yake haikamiliki
kwa wakati na gharama zake kuongezeka hivyo kusababisha kuenda kinyume na kasi
inayotarajiwa na Serikali.
Hakikisheni katika kipindi cha mwezi mmoja ninapata taarifa ya utekelezaji wa miradi katika mikoa hiyo mitano na mikoa mingine na hatua za kuchukua kwa wale wote watakaokuwa wamehusika na changamoto za ucheleweshaji wa miradi husika
Arch.
Mwakalinga.
Aidha, Katibu Mkuu huyo
amewataka Mameneja wote wa TBA kufanya kazi zao kwa uadilifu na umahiri ili
kuiwezesha Taasisi hiyo ya Serikali kutimiza malengo ya kuanzishwa kwake kwa
kuhakikisha nyumba zinazojengwa na kumilikiwa zinakuwa katika viwango bora vya
matumizi wakati wote.
"Tunao wataalamu wengi TBA hivyo meneja atakayeonekana kushindwa kumudu majukumu yake tutambadilisha mara moja ili tuweze kufikia malengo yanayotarajiwa na Serikali", amesisitiza Katibu Mkuu huyo.
Naye, Mtendaji Mkuu wa TBA, Arch.
Daud Kondoro, amemuhakikishia Katibu Mkuu huyo kuwa atahakikisha anatekeleza
maelekezo hayo kwa wakati ili kuhakikisha uwiano wa miradi na fedha
zinazotumika tba zinatumika kwa maslahi ya umma na taifa kwa ujumla.
Imetolewa
na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano
0 Comments