WENYE SIKOSELI WAIOMBA SERIKALI KUONGEZA WATAALAMU WENYE UJUZI

 


📌NA DOTTO KWILASA 

WAZAZI wenye watoto wanaoishi  na ugonjwa wa Sikoseli wameiomba Serikali kuona haja ya kuongeza madaktari maalumu wenye ujuzi wa ugonjwa huo ili kupunguza madhara kwa wagonjwa. 

Hayo yameelezwa jana jijini Dodoma  wakati wa kufunga mwezi wa uhamasishaji jamii kuhusu ugonjwa wa sikoseli.  

Mmoja wa mama hao Zuhura Makuka amesema vituo vingi vya kutolea huduma za afya nchini hazina wataalamu wa kutosha wa ugonjwa sikoseli  na hivyokusababisha wagonjwa wengi kukosa huduma kwa wakati.

Hospitali nyingi hazina kliniki maalumu za kutolea huduma za sikoseli hivyo ukienda unakutana na wahudumu wa afya ambao hawana uelewa,hali hii inatuvunja moyo

Zuhura Makuka

Licha ya hayo ameeleza kuwa  baadhi ya watoa huduma za afya nchini wakiwemo madaktari hawana uelewa wa kutosha kuhusu ugonjwa wa sikoseli hali inayosababisha unyanyapa kuendelea kuwepo katika jamii .

Amefafanua kuwa wao kama wazazi wenye Watoto wa ugonjwa huo wamekuwa na wakati mgumu wanapokutana na vikwazo hivyo ambapo hufika wakati wanakata tamaa ya kuendelea  kuwahudumia Watoto wao.

Kutokana na hayo ,Wizara ya afya ,Mkurugenzi Msaidizi wa Magonjwa yasiyoambukiza,kutoka Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia Wazee na Watoto,Dk.James Kiologwe alisema ,Serikali kupitia wizara hiyo tayari imeafanya mkakati wa kutatua kero zote zinazohusu ugonjwa huo.

Tayari tumechukua hatua kadhaa kukabiliana na ugonjwa huo ikiwemo kuunda kikosi kazi cha wataalamu wa kukabiliana na ugonjwa huo,tunaamini Htua hii itasaidia kwa kiasi kikubwa kuondoa uhaba wa wataalamu wa sikoseli.

Dk.James Kiologwe

Hata hivyo amesema pia mpango wa Serikali ni kuhakikisha kila Hospitali ya Mkoa inakuwa na Kliniki kwa ajili ya kupima ugonjwa wa Sikoseli.

Hata hivyo ameiasa jamii kuzingatia uchunguzi wa afya kabla ya kuingia kwenye mahusiano ili kuepuka kupata watoto wenye ugonjwa wa sikoseli.

Akizungumza kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Serikali,Profesa Abeid Makubi ,Dk.Kiologwe amesema,utafiti  unaonesha  kwamba kila watoto 100 waliopimwa ugonjwa wa Sikoseli 15 ama 20 wamekutwa na vinasaba vya ugonjwa huo huku Kanda ya Ziwa ikitajwa kuwa na wagonjwa wengi.

Aidha amesema katika utafiti uliofanywa na Shirika la Afya Duniani (WHO) mwaka 2015 unaonesha kwamba  kati ya watoto 100 waliopimwa ugonjwa wa Sikoseli watoto kati  15 mpaka  20  wamekutwa na vinasaba vya ugonjwa wa Sikoseli.

Dk.Kiologwe pia alisema jumla  ya watu 1000 huzaliwa na ugonjwa wa Sikoseli kila siku duniani.

Mkurugenzi huyo alieleza kuwa Tanzania ni nchi ya tano duniani kuwa na idadi ya wagonjwa wengi wa Sikoseli huku ikishika nafasi ya nne barani Afrika.

Nchi zenye wangonjwa wengi duniani ni Nigeria,India,Kongo,Angola na Tanzania,ambapo kwa Afrika Tanzania inashika nafasi ya nne hali inayopaswa kutiliwa mkazo zaidi kuhakikisha ugonjwa huu unazuiwa

Dk.James Kiologwe

Amesema ,Tanzania ,kila watoto 100 wanaozaliwa nchini ,8 Kati yao wana ugonjwa wa Sikoseli.

Pamoja na hayo ameongeza kuwa,Licha ya juhudi nyingi zinazofanywa na wizara ya Afya Katika kuelekeza nguvu za uelimishaji jamii juu ya ugonjwa huo ,jamii bado haina uelewa wa kutosha hali inayosababisha unyanyapaa kwa waathirika wa ugonjwa huo.

Kwa upande wake,Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT)  ambaye pia ni Daktari bingwa wa Magonjwa ya ndani kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili,Dk.Elisha Osati  amesema walitumia mwezi mmoja kutoa elimu kwa jamii katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa ambapo kati ya watoto  1,800 waliowapima 360 wamewakuta na vinasaba vya ugonjwa huo.

Tumejitahidi kufanya mambo mengi kwanza kutoa elimu, tumepita katika shule 15 zilizopo Kanda ya Ziwa,tumewafikia  wanafunzi  10,000 tumewapa elimu.

Dk.Elisha Osati 

Hata hivyo amesema katika Hospitali 6 walizozitembelea Kanda ya Ziwa  ni mbili pekee ndizo zenye Kiliniki ya kupima ugonjwa wa Sikoseli huku akikiri wagonjwa wengi kuwa katika Mkoa wa Mara.

Kwa upande wake,Daktari bingwa wa Magonjwa ya Watoto,kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma,Dk.Halima Kassim amesema wameanzisha Kiliniki wa ugonjwa huo mkoani Dodoma baada ya kugundua kuna watoto wengi wenye ugonjwa huo.

 

Post a Comment

0 Comments