MKANDARASI APEWA HADI DISEMBA KUKAMILISHA KITEGA UCHUMI DODOMA

 


📌NA DOTTO KWILASA

 

MENEJIMENTI ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma imemuagiza Mkandarasi kampuni ya Mohammedi Builders anayejenga mradi wa jengo la kitegauchumi ‘Government City Complex’ kukamilisha na kukabidhi mradi huo ifikapo  30 Disemba, 2020.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Joseph Mafuru alipoongoza timu yake ya menejimenti kutembelea na kukagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa kitegauchumi wa jiji ‘Government City Complex’ katika mji wa Serikali eneo la Mtumba jijini hapa.

Mafuru amesema “nimekuja na timu ya Menejimenti ninayoiongoza hapa kumsimamia na kumkumbusha mkandarasi anayejenga mradi huu kuwa kwa mujibu wa mkataba wetu, mradi huu unatakiwa kuisha tarehe 30 Disemba, 2020 na bahati nzuri yeye anasema hana tatizo na kukamilisha mradi huu tarehe hiyo”.

Mkurugenzi Mafuru amesema kuwa mradi huo umejengwa katika mji wa Serikali yalipo makao makuu ya Serikali eneo la Mtumba ili kuwezesha kutoa huduma katika eneo hilo la Mtumba. “Lengo la mradi huu ni kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wakati yeye anapambana kujenga ofisi za Serikali hapa Mtumba, sisi kama Jiji tunapambana kuhakikisha huduma ambazo zitakosekana kwenye maeneo mengine zinapatikana katika jengo hili. Jengo hili lina awamu nne.

Hii ni awamu ya kwanza ambayo tumekuja kuishuhudia ikiwa inaelekea ukingoni, nimetaarifiwa kuwa awamu hii ujenzi wake umefikia asilimia 60

Joseph Mafuru.

Licha ya hayo Mkurugenzi huyo anawaalika wafanyabiashara na wawekezaji kujitokeza kutembelea mradi huo na kuweka miradi ya kupanga katika jengo hilo.

“Mradi huu utakuwa na maeneo ya biashara, ‘apartments’, maduka makubwa ya biashara, sehemu za taasisi za kifedha. Lakini pembeni tunajenga ukumbi mkubwa wa mikutano wenye uwezo wa kuchukua watu 500 ili kurahisisha shughuli zote za Serikali kufanyika katika eneo hili.

 Eneo hili la mji wa Serikali litakuwa na wageni wengi ambao watakaokuwa wakihitaji huduma za Serikali, mabalozi, wawekezaji na watumishi mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi” anasema Mafuru.

Mradi wa ujenzi wa jengo la kitega uchumi la Jiji la Dodoma ulibuniwa na timu ya menejimenti na kupitishwa katika vikao vyake vya kisheria ili utekelezwe na kuiwezesha Halmashauri kuongeza wigo wa mapato ya ndani. Mradi huo, awamu ya kwanza itagharimu shilingi bilioni 18.

Kwa upande wake, Mhandisi Merinyo amemuhakikishia Mkurugenzi wa Jiji kuwa mradi huo utakabidhiwa ifikapo tarehe 30 Disemba, 2020.

Amesema kuwa katika kufanikisha kukamilika kwa mradi huo, ujenzi utafanyika usiku na mchana ili kuharakisha mradi huo.

Post a Comment

0 Comments