NEC YAMTUNUKU CHETI CHA USHINDI MAGUFULI

 


📌 DOTTO KWILASA

 

TUME ya Taifa ya uchaguzi (NEC)imemkabidhi cheti Cha ushindi wa kiti Cha Rais Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 Rais mteule wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dk.John Magufuli Pamoja na mgombea mwenza mama Samia Suluhu Hassan huku akisema kuwa ana deni kubwa katika kuwatumikia  wananchi.

Akiongea Katika hafla hiyo Mkurugenzi mkuu wa tume hiyo Wilson Mahera amesema tume hiyo imetangaza Rais Magufuli kuwa mshindi Kutokana nankupata idadi ya kura nyingi ikilinganishwa na Wagombea wote.

Akizungumza  mara baada ya kukabidhiwa cheti hicho alisema kuwa uchaguzi wa mwaka huu umefanyika vizuri na kwa kiwango cha juu huku ukijali utu na haki za binadamu.

Mbali na hayo Dk.Magufuli ametumia nafasi hiyo kuwashukuru watanzania kwa kumuamini na kumpa nafasi ya  kumchagua tena kwa ajili ya kuwatumikia katika kipindi kingine Cha  miaka 5.

"Mmetupa ushindi ambao umetuachia deni kubwa sana maana kupata asilimia 84.4 ni imani kubwa sana na imani yao nitaitimiza kwa kufanya kazi sana"amesema.

Dk.Magufuli amesema kuwa ushindi huo sio wake bali ni wawananchi wenyewe hivyo atawatumikia wananchi wote bila kujali mahali wanapotoka.

Katika hatua nyingine Rais Magufuli ameipongeza Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) nakusema kuwa kwa mara ya kwanza kulikuwepo na karatasi maalu kwa watu wasioona.

"Pamoja na hayo lakini pia kulikuwa na vitendea kazi vingi na vyakutosha ndio maana kulikuwa na vituo vingi vya kupigia kura ili kuepusha msongamano"amesema.

ATOA SHUKRANI KWA WAGOMBEA WENGINE.

Dk.Magufuli amewashukuru wagombea wengine waloshiriki katika kinyanganyiro cha kugombea urais huku akiahidi kushirikiana nao katika kuleta maendeleo ya nchi.

Siasa siyo vita wala siyo vita na katika hilo na katika hilo napenda kuwaahidi kuwa nitashirikiana nanyi kwani maendeleo hayana chama

Pamoja na hayo Rais Magufuli amewashukuru viongozi wa dini kwa kuendelea kuombea uchaguzi na kuilinda amani.

"Lakini pia navishukuru vyombo vya ulinzi na usalama kwa kuhakikisha amani inakuwepo tangu kipindi cha mchakato wa uchaguzi mpaka sasa"

 


PONGEZI KWA CCM.

Pamoja na mambo mengine ,Magufuli amekishukuru chama cha mapinduzi kwa kuweza kumteua tena kuwa mgombea wa urais lakini pia kuwa pamoja naye katika kampeni.

Ilani ya uchaguzi tuliyokuwa tukiinadi nitahakikisha tunayatimiza yale yote yaliyomo ili kuweza kuleta maendelo katika nchi yetu 

Hata hivyo Rais Magufuli amewataka wale wote waliochaguliwa katika ngazi mbalimbali ikiwemo ubunge na udiwani kuwajibika kwa wananchi katika yale waliyoyaahidi.

"Twende tukashikamane kwa pamoja kwa maslahi ya taifa letu kwani maendeleo hayana chama"amesema.

RAIS MSTAAFU WA BURUNDI.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Rais mstaafu wa Burundi Silvester Ntibantunganya ambaye amewakilisha waangalizi wa uchaguzi mkuu kutoka nchi za Afrika mashariki ambapo alisema uchaguzi ulikuwa huru na demokrasia.

Licha hayo Ntibantunganya amesema mchakato wa uchaguzi nchini hapa unatazamwa na mataifa mengine Kama funzo na kuepusha mtafaruko katika nchi nyingi za kiafrika.

"Dunia imeshuhudia uchaguzi Wenye demokrasia ya hali ya juu na ni matumaini yangu kuwa wengi tumejifunza na kujionea neema iliyopo ya amani na utulivu,"alisema.

WAWAKILISHI WA VYAMA VINGINE VYA SIASA.

Katika hafla hiyo ya utoaji wa cheti kwa mshindi wa kiti Cha Rais ambaye  ametokana na Chama Cha mapinduzi (CCM),baadhi ya Wagombea wa kiti hicho ambao kura zao hazikitosha ,Walipata nafasi ya kuzungumza kwa niaba ya wengine huku wakisisitiza kuendelea kishirikiana na serikali bega kwa bega Katika Maendeleo.

Queen Sendiga ambaye alikuwa mgombea wa kiti cha urais kupitia Chama cha ADC mbali na  kumpongeza Dk.Magufuli kwa kupata  ushindi wa kishindo alimshukuru kwa kuendesha uchaguzi mkuu kwa njia ya  demokrasia na amani.

Sendiga alisema,mbali na kwamba  kura zake hazikutosha hiyo sio sababu ya yeye kushindwa kishirikiana na Serikali katika kuijenga Tanzania na kuahidi kuendelea kusimama bega kwa bega na Serikali iliyopo madarakani kuwatumikia watanzania.

"Utofauti wa vyama si uadui,nakubaliana kuanza upya kushirikiana kwa vitendo na Viongozi waliopo madarakani Katika kuanza kwa matumaini mapya ya miaka mingine mitano ijayo,"amesema.

Licha ya hayo amemuomba Rais Magufuli kuendelea kuenzi matakwa ya wananchi Katika kuleta maendelo na maisha mazuri hali itakayosaidia zaidi kulinda na kuuheshimu Muungano na amani.

Mbali na hayo Mgombea huyo wa ADC ametumia nafasi hiyo kumuomba Rais Magufuli kutoa ruzuku ya fedha kwa vyama vyote vya siasa nchini ili kuweza kujiendesha.

Kwa upande wa Mgombea wa NRA Leopord Mahona amesema ushindi wa Magufuli ni ishara ya mafanikio ya maendeleo zaidi kwa miaka mingine ijayo.

"Kutokana na ushindi huu tunatarajia mazuri mengi zaidi ,na sisi kama wafuasi wa vyama vingine vya siasa tunaahidi kushirikiana na Serikali ijayo kwa Maendeleo ya watanzania,"anasisitiza .

 

Mwisho.

 

 

 

 

 

 

 

 

Post a Comment

0 Comments