UJENZI WA VYOO USIOZINGATIA UTAALAMU CHANZO KUENEA MAGONJWA YA MILIPUKO

 


📌BEN BAGO/MTANDAO

 UKOSEFU wa vyoo bora katika jamii nyingi duniani umebainishwa kama mojawapo wa sababu inayochangia kwa kiasi kikubwa kuibuka kwa magonjwa ya mlipuko.

Hivyo basi serikali nyingi duniani hususani nchi za dunia ya tatu ambako tatizo linaonekana kuwa kubwa zaidi, zinapambana kuondokana na tatizo.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) zaidi ya watu bilioni 20 duniani inasemekana hawana vyoo. Kati yao watu milioni 673 wanajisaidia kwenye maeneo ya wazi ikiwemo vichakana, vichochoroni na hata kwenye vyanzo vya maji hali inayosababisha asilimia 10 ya watu dunia kutumia mboga mboga zilizomwagiliwa na maji machafu.

Kwa upande wa Tanzania, Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu  Hassan, amesema kuwa takwimu zinaonyesha watu wapatao 30,000 huugua magonjwa ya kuhara kila mwaka na baadhi yao hupoteza maisha, hivyo jamii inatakiwa kuzingatia usafi wa mazingira  ili kuepuka vifo hivyo ambavyo inakadiriwa ni sawa na idadi ya wastani wa watu 83 kwa siku.

“Kama Taifa hatuna budi kuwekeza nguvu na rasilimali zetu katika suala la usafi wa mazingira ikiwemo matumizi ya maji safi na vyoo bora ili kufikia malengo yetu ya kitaifa pamoja na yale ya kidunia,” amekaririwa Mhe. Samia Suluhu, wakati wa uzinduzi wa kampeni ya nyumba ni choo, Disemba 8 jijini Dodoma.



Uhamasishaji wa ujenzi na matumizi ya vyoo bora ili kuzuia magonjwa ya mlipuko ulianza  rasmi mwaka 1973 hadi mwaka 1978 ambapo serikali ilianzia kampeni iliyojulikana kama  “Mtu ni Afya.”

Kampei hii ililenga kuhamasisha wananchi kujenga aina yeyote ile ya choo ili kuepuka mlipuko wa magonjwa kama vile kipindupindu.

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Magufuli ameonyesha kusikitishwa kwake kutokana na uwepo wa kipindupindu nchini, hivyo Watanzania hatuna budi kuwa wasafi wa mazingira ili kuepuka mlipuko wa ugonjwa huo,” alikaririwa aliyekuwa Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu wakati wa uzinduzi wa kampeni ya nyumba ni choo.

Wakati  hali yauboreshaji, ujenzi na matumizi ya vyoo ukiendelea kuwa katika viwango vya juu, hali ya magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu na kuhara yanapungua kwa kasi.

Takwimu za kitaifa zinaonyesha wazi kwamba uboreshaji wa usafi wa mazingira ukiwemo vyoo bora na matumizi sahihi, upunguza kwa kiasi kikubwa magonjwa ya mlipuko.

Mkoa wa Dodoma unaweza kuwa kielelezo katika eneo hili ambapo umiliki wa vyoo upo kwa asilimia 65.9 hali inayofanya mkoa huu kutopata kesi ya kipindupindu kwa takribana miaka minne.

Katika kampeni ya nyumba ni choo iliyokuwa inaratibiwa na Wizara ya afya, Mkoa wa Dodoma imeshika nafasi ya tatu, hivyo tunajitahidi kuhamasisha matumizi bora ili tuendelee kuepuka magonjwa ya milipuko

Fransis Bukulu, Kaimu Ofisa Afya na Usafi wa Mazingira Mkoa wa Dodoma.

SABABU ZINAZOWAFANYA WATU KUTOJENGA NA KUTUMIA VYOO

Zipo sababu kadhaa zinazoanishwa na watafiti kama ndio chanzo cha baadhi ya watu kutoona umuhimu wa kujenga na kutumia choo. Miongoni mwa sababu hizo ni ukosefu wa elimu ya afya ya mazingira pamoja na tabia ya mazoea.

Yapo mazoea kwa baadhi ya jamii kutojenga na kutumia vyoo kutokana na mazoea waliyoyakuta katika jamii zao.

Mfano baadhi ya jamii zilizopo kandokando ya vyanzo vya maji kama vile maziwa, mito na hata bahari, kujisaidia haja zote kwenye vyanzo husika, hivyo vizazi vyao pia vinaendela na utamaduni huo ambao huchochea magonjwa ya mlipuko.

Kwa mantiki hiyo, elimu na uhamasishaji wa ujenzi na matumizo bora ya vyoo inahitajika katika maeneo hayo ikiwemo Mkoa wa Mara ambao katika ripoti ya kampeni ya uhamasishaji wa ujenzi na matumizi ya vyoo “Nyumba ni Choo” inaonesha mkoa huo unashika mkia.

TAHADHARI KATIKA MATUMIZI YA VYOO

Suala la ujenzi ni jambo la kuzingatiwa ambapo wataalamu wa afya wanasema ujenzi usiozingatia mipango miji, unaweza kuwa chanzo cha magonjwa ya milipuko katika makazi ya watu.

Mara kadhaa hususani maeneo ya mjini kumekuwa na malalamiko ya matumizi yanayokwenda kinyume na kanuni za afya kutokana na utunzaji mbaya wa vyoo.

Mfano katika matumizi ya vyoo vya maji, vyoo vinavyotumia maji kuna utaratibu zake ambao mhusika lazima azifuate ili kulinda afya yake na majirani wanaomzunguka.

Vyoo vinavyotumia maji husafirisha majitaka yenye kinyesi kupitia mifumo maalum ya bomba ambayo hutengenezwa kwa ajili ya kazi hiyo. Husaidia kuboresha afya hasa katika maeneo yenye msongamano wa makazi mijini na mara nyingi ndio aina ya vyoo ambavyo watu wengi hupendelea.

Hata hivyo, gharama ya kunyonya vyoo vinapo jaa huwa ni kubwa, hivyo mara nyingi huwalazimisha wenye nyumba kuelekezea majitaka yenye kinyesi kwenye mito, maziwa au bahari.

Kuna watu wanakwepa gharama kunyonya maji yale kwa kutumia magari maalumu, kipindi cha mvua wanakitumia kutitirisha maji taka hayo kwenye mifereji ya maji ya mvua kitu ambacho ni hatari zaidi katika uthibiti wa magonjwa ya milipuko anabainisha

Abdalla Mahia, Afisa Afya Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Afisa hiyo ameongeza kuwa hali hiyo hueneza vijidudu vya maradhi kutoka kwenye majitaka hadi kwenye njia  za maji za kawaida au za majirani.

Hivyo basi, ujenzi wa vyoo usiozingatia utaalamu wa mipango miji unaweza kuwa chanzo cha kueneza kwa magonjwa ya milipuko

Post a Comment

0 Comments