DKT FAUSTINE NDUGULILE : KUNA MPANGO WA KUANZISHA MFUMO WA UNUNUZI WA VOCHA KAMA ILIVYO KWENYE LUKU.

 

📌FAUSTINE GIMU.

Waziri  wa  Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dkt.Faustine Ndugulile amesema kuwa serikali ipo katika Mchakato wa kuweka sera ya kuhakikisha makampuni ya simu  yanakuwa na mfumo wa uuzaji wa  vocha kama ilivyo kwenye mfumo wa uuzaji wa LUKU kwenye Umeme  ili kuondoa malalamiko ya wananchi kuibiwa vifurushi vyao na makampuni hayo

Dkt.Ndugulile amebainisha hayo  jijini Dodoma  wakati akifanya mahojiano maalum na  mtandao huu   kufuatia wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini kutoa malalamiko kwa kampuni za simu juu ya vifurushi ama bando walizojiunga  kuisha mapema ikilinganishwa na kiasi cha fedha walizotumia kujiunga.

“Malalamiko  yamekuwa mengi sana kwa wananchi kutokana na vifurushi kuisha kabla ya wakati  ikilinganishwa na fedha walizotumia kujiunga hivyo sisi kama serikali tumeamua kuchukua hatua ili wananchi wanufaike na mawasiliano ya  simu ambapo kuna haja sasa kuwa na mfumo wa vifurushi  kama ilivyo kwenye LUKU za Umeme “alisema.

 Aidha,Dkt.Ndugulile amesema tayari ameshatoa maagizo kwa mamlaka ya Mawasiliano Tanzania [TCRA]kulifanyia Uchunguzi kwa Muda wa miezi mitatu pamoja na kuwa na mpango wa kupeleka malalamiko Wizarani kila mwezi.

“Tumeagiza TCRA kwenda kulifanyia uchunguzi  suala hili kubainisha nini changamoto lakini pili waje na mapendekezo kwa serikali na tuone namna ya kuyafanyia uchunguzi na maagizo hayo tumetoa ndani ya miezi mitatu”alisema.

 Hata hivyo,Dkt.Ndugulile amebainisha kuwa hadi sasa zaidi ya simu kadi milioni 50 zimesajiliwa ,huku watanzania milioni 27 wanatumia internet na Watanzania milioni 29 wakitumia miamala ya fedha kwa njia ya Simu. 

“Mhe.Rais alivyoanzisha hii wizara mpya alikuwa na makusudi yake ,moja ni kuongeza wigo wa Matumizi ya TEHAMA kwa manufaa ya Watanzania,hivi tunavyoongea  hadi sasa zaidi ya simu kadi milioni 50 zimesajiliwa ,huku watanzania milioni 27 wanatumia internet na Watanzania milioni 29 wakitumia miamala ya fedha kwa njia ya Simu”amesema.

 

 

Wakizungumza na mtandao huu   jijini Dodoma baadhi ya wananchi  jijini Dodoma wamesema kuishiwa virufurushi kabla ya matumizi  limekuwa changamoto kubwa katika maisha yao  huku wakiipongeza serikali  kupitia Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari  kwa kuanza kufuatilia malalamiko hayo ya muda Mrefu.

 Danson Mwaluko ni miongoni mwa Wananchi waliopata fursa ya kuzungumza na Gazeti hili ambapo alisema jambo hilo limekuwa ni kero kubwa kwani hurudisha nyuma uchumi.

"Kwa kweli siku hizi changamoto mno ukijiunga bando la Tsh.1000 ndani ya Dk 15 au 7 linakata tunashindwa tufanyaje"alisema Danson.

 

Tatizo la Wananchi kulalamika vifurushi kukata mapema katika simu zao limekuwa la nchi nzima ambapo serikali ya awamu ya tano imejipanga kutatua malalamiko hayo.

MWISHO.

 

Post a Comment

0 Comments