UHUSIANO WA MAKAZI HOLELA NA MAGONJWA YA MLIPUKO




 ðŸ“ŒRONALD SONYO

KWA mujibu wa takwimu za Umoja wa Mataifa (UN) inakadiriwa kuwa zaidi ya watu bilioni moja wanaishi kwenye makazi holela huku ikitarajiwa idadi hiyo kuongezeka mara mbili zaidi ifikapo mwaka 2030.

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia makazi (UN-HABITAT) limefafanua kuwa makazi duni au holela ni eneo la miji lenye ukosefu wa huduma za msingi (usafi wa mazingira, maji ya kunywa, umeme) na lenye msongamano wa nyumba na watu.

Tafiti mbalimbali zinaonesha hali hiyo inasababishwa na ongezeko la watu mijini, kupanuka kwa mipaka ya miji, kukosekana kwa ardhi huru iliyopangwa, uwezo mdogo kiuchumi wa mamlaka za upangaji na kukosekana kwa nyumba zenye gharama nafuu.

Takwimu zinaonesha kwamba, Kusini mwa Jangwa la Sahara, asilimia 71.8 ya wakazi wa mijini kuishi katika makazi yasiyo rasmi.

Kwa upande wa Tanzania, kwa mujibu wa Ripoti ya Miji Tanzania iliyoandaliwa na Mtandao wa Miji Nchini ya mwaka 2014, wastani wa kiwango cha ujenzi holela kwenye miji hiyo ni asilimia 67.

Aidha, wananchi wengi kutozingatia Sheria ya Mipangomiji, upungufu wa rasilimali watu na fedha pamoja na kukosekana kwa utashi wa kisiasa katika kusimamia Sheria za Mipangomiji ni miongoni mwa sababu za ongezeko hilo.

MAKAZI HOLELA NA MAGONJWA YA MILIPUKO

Makazi yaliyojengwa kiholela yamekuwa katika hatari zaidi ya kushambuliwa na magonjwa ya milipuko kutokana na sababu mbalimbali.

Moja ya sifa ya makazi holela ni hali ya kutopatikana kwa huduma za kijamii kama vile maji hali ambayo inasababisha kwa kiasi kikubwa mlipuko wa magonjwa.

 “Mengi ya maeneo hayo hayana miundombinu na huduma za msingi kama vile maji safi na salama, barabara na mifereji ya maji ya mvua na udhibiti wa majitaka na taka ngumu,” alikaririwa Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angelina Mabula, katika Bunge la 11 alipokuwa akijibu swali la aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalumu, Upendo Peneza (Chadema).


Dk. Mabula amesema hali hiyo husababisha mafuriko, milipuko ya magonjwa, mazalia ya mbu, nzi na mandhari mbaya ya kuishi inayosababisha afya duni na kupunguza nguvukazi.

Pia mengi ya maeneo hayo hayana miundombinu na huduma za msingi kama maji safi na salama, barabara, mifereji ya maji ya mvua na udhibiti wa majitaka na taka ngumu.

Zote hizi ni athari mbaya kwa kuwa mafuriko yamekuwa yakitokea katika makazi mengi ya mijini kutokana na ujenzi holela, mazalia ya mbu na inzi nayo ni chimbuko la malaria na magonjwa ya milipuko.

MSONGAMANO

Maeneo haya yanabainishwa kuwa hatari zaidi katika usambaaji na uambukizwaji wa magonjwa ya mlipuko ikiwemo COVID-19.

Msongomano wa watu katika makazi holela inawafanya wakazi wa maeneo haya kutoweza kuzingatia ushauri wa wataalamu wa afya unaotaka watu kukaa umbali wa mita kadhaa ili kupunguza maambukizi.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) jamii zinazoishi kwenye hali msongamano zipo kwenye hatari zaidi ya kukumbwa na magonjwa ya mlipuko ikiwemo kipindupindu.

Katika makazi yenye msongamano wa watu ni hatari zaidi katika maambukizi ya magonjwa yenye uwezo wa kuambukizana kama vile maambukizo ya vikoozi, TB na magonjwa mengine ya upumiaji, kipindupindu na magonjwa ya ngozi ikiwemo upele.

Hali ya hatari pia ipo katika miundombinu mingine ya umma kama vile vituo vya afya ambako mara nyingi vimeonekana kuwa na uwezo mdogo kuliko idadi ya watu inayojitokeza kufuata huduma katika vituo hivyo.

Msongamano wa watu hurahisha usafirishaji wa viini (germs) kutoka kwa mtu mmoja kwenda mwingine.

Katika maeneo ya masoko na vituo vya mabasi nako kuna hatari zaidi ya kusambaa kwa magonjwa ya mlipuko.

“Ni kweli kama hakuna mipangilio mzuri wa miji magonjwa ya milipuko lazima yajitokeze mara kwa mara lakini kama miji imepangika vizuri hatari inakuwa haipo kwa vile hata mitaro ya maji taka itaeleweka, barabara zitakuwepo na hata vyoo vikijaa inakuwa rahisi kuvi-empty (kunyonya kinyesi),” anaeleza, Fransic Bukulu, Ofisa Afya na Usafi wa Mazingira Mkoa wa Dodoma.

NINI KIFANYIKE?

Kwa kuona umuhimu wa kupambana na janga la makazi holela serikali ilianzisha Programu ya kitaifa ya kupanga, kupima na kumilikisha kila kipande cha ardhi nchini ya mwaka 2015-2025 inayolenga pamoja na mambo mengine kuzuia na kudhibiti ujenzi holela ambao husababisha kuwepo kwa makazi duni, hivyo utekelezaji wa mpango huo uwe endelevu ili kutokomeza makazi holela nchini.

Pia mamlaka husika (zikiwemo Mamlaka za Maji Safi na Taka na usafi wa Mazingira) zijitahidi kupeleka huduma kijamii ili kupunguza madhara yatokanyo na ukosefu au upungufu wa huduma hizo.

Wananchi wapewe elimu ya madhara ya kuishi kwenye makazi holela na elimu ya usafi wa mazingira katika maeneo hayo ili kujilinda na magonjwa.



Post a Comment

0 Comments