VIONGOZI WA DINI WATOA NENO KUELEKEA MWAKA MPYA

 


📌DEVOTHA SONGORWA.

KUELEKEA siku kuu ya mwaka mpya viongozi wa umma na watanzania wametakiwa kujitathimni kuhusu utendaji wao kwa mwaka mzima na kwa namna gani wanajipanga kutekeleza majukumu kwa uadilifu kwa maslahi ya Taifa.

Akizungumza jana na gazeti hili Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mustafa Rajabu Shaban alisema kufanya tathimini huwezesha kutambua ikiwa malengo yaliyokusudiwa yalifikiwa na kufanyia kazi changamoto zilizojitokeza.

“Kwanza tumshukuru Mungu kwa kutujalia uzima mwisho mwaka  huu ni wa kujitathimini kuanzia Kaya, Wilaya, Mkoa hadi Taifa kwamba je, katika mwaka uliopita wamefanya nini,yapi hayajatekelezwa  wajue ni kwanini na wanajipanga vipi mwaka ujao wa 2021”,alisema Sheikh Shaban.

Akizungumzia suala la kulinda amani alihimiza watanzania kuheshimu,kulinda amani na utulivu katika nchi badala ya kutumika kuharibu  tunu hiyo muhimu akisistiza kusameheana  kutokana na mapungufu ya kibinadamu na kuanza mwaka upya kwa upendo na mshikamano.

“Sisi hatuna cha kumlipa Mungu zaidi ya kufanya toba,majuto na kujiongeza zaidi kumjua Mungu na uwe mwaka wa kudumisha amani  siyo kupanga kuvuruga kama tumeishi vyema mwaka uliopita tujiulize tulitumia vigezo gani kuwa salama hadi sasa?”,alieleza Sheikh huyo.

Naye Mchungaji wa Kanisa la International Evengelism Church,Askofu Sylvester Thadey alisema ipo sababu ya kila mmoja kumshukuru Mungu kwa kulipigania Taifa   mwaka 2020 dhidi ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu unaosababishwa na Virusi vya Corona(COVID-19) na kusheherekea kwa amani mwaka mpya.

“Nitoe salamu za kheri ya mwaka mpya na tunapoanza mwaka mpya waumini wa imani zote tufanye kazi kwa bidii kuunga juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano kuinua uchumi wetu,wazazi na walezi nao niwasihi kuwalea watoto wao katika maadili mema kwani ndiyo nguvu kazi ya Taifa kwa siku zijazo”,alifafanua Askofu Thadey.

Kwa upande wake Kamanda wa Jeshi la Polisi MKoa wa Dodoma,Gilles Muroto alitoa onyo kwa baadhi ya watu watakaofanya fujo au vitendo vya uhalifu wakati wote hasa kipindi cha siku kuu akisema jeshi halitomfumbia macho mtu huyo.

“Sisi Jeshi tuko imara kuhakikisha watu wanasherehekea salama na tumeshirikisha wenye nyumba za wageni, vikundi vya ulinzi shirikishi kutoa taarifa za watu ambao  wanawatilia shaka, tuna doria za magari,miguu na tuwatake wazazi kuwa makini na watoto wao”,alisisitiza Kamanda Muroto.

Akitoa salamu za mwaka mpya Neema Chitete mkazi wa Chamwino aliishauri jamii kupendana na kushirikiana katika shughuli za uzalishaji kwa kupeana fursa za kiuchumi kujiletea maendeleo kwa mwaka ujao.

Aidha Rehema Suleiman Idd alieleza mwaka huu umekuwa wenye historia kubwa kwa nchi kutokana na ugonjwa wa COVID-19 ulioyakumba mataifa mengi Duniani akiwaomba watanzania kumtegemea Mungu katika maisha yao na kuishi kwa malengo.

 

 

Post a Comment

0 Comments