TASISI ZA UMMA ZATAKIWA KUWA NA BARAZA LA WAFANYAKAZI LA KUISHAURI SERIKALI

 


📌HAMIDA RAMADHANI

NAIBU waziri wa Maji Maryprisca Mahundi amesema kuwa ni muhimu kwa taasisi za umma kuwa na Baraza la wafanyakazi kwani mabaraza haya yameanzishwa kisheria kwa dhumuni la kuishauri Serikali.

Uundwaji wa baraza la wafanyakazi ni Agizo la Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania la mwaka 1970, na ni utekelezaji wa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya mwaka 2004 Kifungu 73(1-3) kinachoelekeza juu ya kutekeleza Sera ya kuwashirikisha Wafanyakazi katika uongozi wa pamoja.

Naibu waziri huyo Maryprisca  ameyasema hayo leo jijini hapa alipokuwa akifungua baraza la kwanza la wafanyakazi EWURA katika ofisi zoa zilizopo Dodoma . 

Amesema  Baraza la Wafanyakazi ndilo jukwaa la kisheria la majadiliano ya pamoja, kati ya viongozi na watumishi katika utumishi wa umma, kuhusu wajibu na maslahi ya watumishi.

Amesema madhumuni ya kuanzishwa kwa baraza hilo la wafanyakazi nipamoja na kushauri serikali katika ngazi za idara, taasisi na Wizara kuhusu usimamizi wa kazi na rasilimali watu, utekelezaji wa majukumu,kulinda haki na wajibu wa waajiri na wafanyakazi, kutoa ushauri kuhusu kujenga hali bora za kazi, maslahi ya Wafanyakazi na kusimamia haki na ustawi katika sehemu za kazi. 

Vile vile amesema  Baraza lina wajibu wa kutoa ushauri, kusimamia na kuhakikisha kuwa waajiri na watumishi wanatambua wajibu na haki zao, pia wanazingatia maadili ya utumishi wao ili kuleta matokeo ya utendaji wa kazi yenye tija, staha na upendo.

“Napenda kuwakumbusha kwamba Serikali ya awamu ya tano imedhamiria kwa dhati, kuondoa uzembe, rushwa na vitendo vyote visivyofaa mahala pa kazi ikienda sambamba na kubana matumizi yasiyo ya lazima ili kuongeza tija. Hivyo, ni wajibu wa kila mfanyakazi wa EWURA kuhakikisha anafahamu wajibu wake mahali pa kazi,”amesema Naibu waziri huyo.

Pia kutekeleza malengo aliyopangiwa katika muda uliopangwa, vile vile kutunza mali na vifaa alivyokabidhiwa kufanyia kazi, pamoja na kufika kazini na kuondoka kwa muda uliopangwa 

Aidha amesitiza mambo machache ambayo ni muhimu, ambapo jambo la kwanza amewataka watumishi hao kuzingatia  Uwajibikaji, suala ambalo  ni nguzo kuu ya Mafanikio katika sehemu yoyote ya kazi.

 


Pia amewaomba kutoa ushirikiano kwa watumishi ilikuondoa malalamiko na kuhakikisha wanashughulikia masuala ya maendeleo kwa wakati kwa Wajumbe mnaowakilisha Wafanyakazi wote wa EWURA. 

“Hamna budi kuwa mfano katika jambo hili la uwajibikaji na kuleta ufanisi lakini pia Katika mkutano huu, nimeambiwa kutakuwa na mada zitakazowasilishwa kuhusu mabaraza ya wafanyakazi na, vyama vya wafanyakazi hususani TUGHE. na Sheria ya Utumishi wa Umma na Masuala ya nidhamu Ni imani yangu kuwa mtasikiliza na kushiriki majadiliano ili mwisho wa siku tupate kuelewa kile kilichokusudiwa,”amesema .

Na kuongeza kusema “Ni Matarajio yangu kwamba, kila Mjumbe wa baraza aliyeko hapa atatimiza wajibu wake, Naamini sote tukifanya kazi zetu kwa umakini tutaweza kutoa mchango wetu kikamilifu katika kufikia malengo ya Serikali ya awamu ya tano ya Ujenzi wa Uchumi wa Viwanda na Katika kukamilisha azma hiyo, Watumishi wa EWURA wanaowajibu mkubwa wa kuongeza kujituma na kuwa waadilifu,”amesema.

kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi, Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Muhandisi Godfrey Chibulunje,amesema baraza hilo ni lakwanza tangia kuanzishwa kwa Ewura.

Amesema kuanzishwa kwa baraza hilo ni kulenga kuongeza ufanisi na tija kwa wafanyakazi bila kusahau utendaji kazi wao wa kila siku na majukumu ya EWURA.

 

Post a Comment

0 Comments