UTAFITI WA MBEGU UNAVYOLETA TIJA KWA WAKULIMA.

 


📌NA DOTTO KWILASA.

WAKATI  nasoma shule ya msingi,moja ya mambo niliyofundishwa ni kuhusu mazao yanayopatikana Tanzania na asili ya mazao hayo kwa kila mkoa.

Namkumbuka sana mwalimu wangu wa somo la Jiografia alinifundisha kuwa nchini hapa kilimo cha Mpunga kinalimwa zaidi  Kyela,Mahindi-Iringa,Karanga-Kongwa,Miwa-Kirombero ,Ndizi -Bukoba wakati Korosho ikilimwa zaidi Mtwara.

Na huu ndiyo ulikuwa mfumo wa kilimo kabla kuanza  mapinduzi ya ukuaji wa sekta ya kilimo cha kisasa sambamba na matumizi ya teknolojia bora zikiwemo mbegu bora za kilimo.

Mazoea haya yalidumaza sana suala la kilimo kwani iliwabidi wakulima kulima mazao yaliyozoeleka katika eneo husika huku sababu ya kufanya hivyo ikitajwa kuwa ni kila mmea hustawi   kulingana na hali ya hewa ya eneo husika.

Hali hiyo inabadilika sasa,kadri siku zinavyokwenda mambo yanabadilika ,unaweza kusema kuwa watu wanaenda na wakati .

Namaanisha kuwa kulima kwa mazoea kumepitwa na wakati unaweza ukawa Shinyanga na ukakuta wakulima wa huko wanalima mazao yaliyozoeleka kulimwa Dodoma hali inayopunguza uhaba wa chakula kwa kiasi kikubwa.

Hatua hii imetokana na faida ya uwepo wa Wataalam wa utafiti wa mbegu bora za kilimo ambao hutumia muda mwingi kubuni mbinu za kuzalisha mbegu za kisasa ili kumrahisishia mkulima kulima kwa faida na kuondoa umaskini .

Hii imejidhihirisha mkoani Dodoma ambako kwa kiasi kikubwa sasa         wakulima wanaanza kuhamasika na kilimo cha mazao ya kimkakati Kama vile Ndizi ,korosho na Mpunga kwa maeneo ya Wilaya Bahi na kitongoji Cha Swaswa  nje kidogo ya jiji la Dodoma  jambo ambalo mwanzo halikuwepo.

kiuhalisia hali ya hewa katika mkoa huu ni savana kavu ambayo huwa na kipindi kirefu cha ukame kuanzia mwezi Aprili hadi mwezi Desemba, na kipindi kifupi cha mvua katika miezi inayosalia.

Aidha wastani wa mvua katika mkoa huu  ni milimita 570 na asilimia 85 ya wastani huu hunyesha kwa miezi minne yaani kati ya mwezi Desemba na mwezi Machi kila mwaka.

Licha ya kuwa imezoeleka maskioni mwa wengi kuwa Dodoma ni kame,kauli hii hupingwa na wanamazingira wengi huku wakisistiza kuwa mkoa huu una asili ya maji mengi kuweza kusapoti kilimo cha umwagiliaji ikiwa jamii itakubali kubadili mtizamo huo.

Kutokana na hayo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hasan katika uzinduzi wa kampeni yake ya kujanikisha Dodoma iliyofanyika Desemba 21 mwaka 2017  katika eneo la Mzakwe Kata ya Makutupora Manispaa ya Dodoma alizitaka Halmashauri za Mkoa wa Dodoma kutunga Sheria Ndogo zitakazomtaka kila Mkazi wa eneo katika Mkoa huo kupanda miti ili kupambana na mabadiliko ya hali tabia Nchi. 

Alisema upandaji miti si kwa ajili ya kuhifadhi mazingira tu bali ni fursa ya kilimo, kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ambapo alitolea mfano mti mmoja uliokomaa unaweza kunyonya kiasi cha kilogramu 150 za gesi ya hewa ya ukaa kwa mwaka na hivyo kusaidia kupunguza joto kwenye uso wa dunia, na pia kusaidia kuboresha afya ya mwili na akili.

Hali hiyo  imesaidia  kwa kiasi kikubwa ambapo sasa utafiti wa mbegu bora za mtama,zabibu,migomba,alizeti,mihogo na uwele zinaendelea kuwanufaisha wakulima katika mkoa huu na kupata mazao mengi yenye ubora wa viwango vya kisayansi.

Ili kutoa nafasi kwa wakulima wengi zaidi kujifunza kuhusu uzalishaji wa ndizi ,Mtafiti wa Idara ya Udongo kituo cha utafiti TARI-Makutupora   Ashura Ally anasema,Kawaida migomba inaweza kupandwa kwa utaratibu

wa nafasi ya umbali wa mita 2.75 kwa 2.75, kigezo hiki mara nyingi kinakuwa kwa migomba mifupi  na umbali wa mita 3 kwa 3, kwa migomba ya urefu wa kati huku umbali wa mita 3.6 kwa 3.6, kwa migomba mirefu zaidi

 Anazidi kueleza kuwa uchimbaji mashimo inafaa ufanywe mapema kabla ya muda wa kupanda Shimo lichimbwe kwa kutenganisha udongo wa juu na wa chini.

“Iwapo utachimba shimo la mviringo litafaa liwe na kipenyo cha sentimeta 60 hadi 90 na kina cha sentimeta 60 hadi 90,iwapo utachimba shimo la mstatili au mraba litakuwa na urefu, upana na kina cha sentimeta 60 hadi 90, kutegemea kiasi cha mbolea kilichopo na kiasi cha kvua kinachonyesha sehemu hiyo,”anasema.

 Pamoja na mambo mengine anaeleza uwekaji wa mbolea hufuata mara baada ya mashimo kuwa tayari Mbolea ya samadi iliyooza vizuri au mboji iwekwe kwenye lundo la udongo wa juu kando ya kila shimo na tayari kusubiri kuja kurudishiwa kwenyeshimo baada ya mche/machipukizi kuwekwa kwenye shimo.

 “Zao la ndizi huweza kuanza kuvunwa katika kipindi cha miezi 9 hadi miezi 15 tangu kupandwa ,Muda wa kuvunwa hutegemea hali ya hewa ambapo sehemu za joto ndizi huvunwa mapema zaidi kuliko sehemu za baridi,Pia migomba iliyopandwa kwa kutumia machipukizi huzaa mapema kuliko iliyopandwa miche iliyozalishwa kwa chupa (tissue culture),”anafafanua.

Dosca David ni mmoja wa wakulima mkoani hapa ambaye ametumia fursa ya uwepo wa vituo vya utafiti wa mazao na kuanza kulima zao la ndizi  jambo linalowashangaza wengi.

 "Wengi walinishangaa ,hawajazoea kuona mashamba ya Migomba Dodoma,wengi walinibeza lakini kwa kuwa nilijiamini na kuamini elimu niliyopewa na Watafiti sikuwa na shaka,"alisema kwa kujiamini.

 Anasema pamoja na kuwa ni zao la kibiashara kwa soko la ndani bado njia bora zikitumika katika kuzalisha migomba inayotoa ndizi zinazokidhi vigezo vya uhitaji wa soko la nje itasaidia zaidi kukuza vipato vya wakulima mkoani Dodoma.

“Niliamua kutafuta eneo linalofaa kwa kilimo katika Kijiji cha Mtumba(mji wa Serikali) eneo ambalo lipo kimkakati zaidi hasa Kutokana na Ofisi nyingi za Serikali kuwepo mahali hapo,

 Jambo hili limewavutia wenyeji wengi wa Kijiji hiki na kuanza kuiga,naweza kusema nimekua mfano wa kuigwa ,ukifika Mtumba karibu kila nyumba  ina Migomba japo si mingi lakini inatia moyo kwamba utaalamu wa utafiti wa mazao unafanya kazi,"anaeleza.

 Hata hivyo anasema kabla ya kuanza kilimo hicho alitafuta ushauri wa kitaalam katika kituo cha utafiti TARI-Makutupora ambapo alishauriwa kuwa zao hilo linafaa kulimwa kutokana na hali ya hewa  Kiasi cha chini cha mvua kifaacho ni 100mm kwa mwezi au 1200mm kwa mwaka,

 “Mtafiti wa Idara ya Udongo kituo cha utafiti TARI-Makutupora   alinipa maelekezo  ya  kuanzia uandaaji wa mashamba hadi kufikia uvunaji wa zao hilo jambo linalotia moyo zaidi ni kuwa wakati wowote mimi na wakulima wenzangu tunapohitaji ushauri tunapewa elimu bure,”anafafanua.

“Alinieleza Mgomba hustawi zaidi kwenye Udongo wenye rutuba ya kutosha,Usiotuamisha maji na usio na chumvi,Chachu ya udongo inafaa iwe kati ya pH 5 mpaka pH 8 ndicho nilichofanya,”anafafanua.

 David anaeleza kuwa Migomba huhitaji maji mengi hivyo kutokana na hali ya hewa ya mkoa huo humlazimu Wakati wa kiangazi kutumia zaidi kilimo cha umwagiliaji kuepuka kudhoofisha mimea yake.

"Baada ya kujifunza vizuri kuhusu zao hilo nilichukua jukumu la kuandaa sehemu husika ambapo kwa kuanza alianza kilimo cha majaribio katika eneo lenye ekari Moja wazo ambalo limezaa matunda ,"anasema

Hata hivyo anatumia nafasi hii kuwatoa hofu wakulima wanao ogopa kulima mazao mengine na kusema kuwa wanapaswa kutumia fursa ya Dodoma kuwa makao makuu na kuanza kuwatumia wataalamu wa utafiti wa mazao kuwasaidia mbegu bora  na kujikita zaidi katika kilimo cha umwagiliaji kuondokana na uhaba wa chakula.

 Mbali na hayo ameiomba Serikali kupitia Tume  ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kuendelea kusambaza matokeo ya Utafiti wa mbegu kwa wakulima ili kuongeza tija.

        Mwishooo.

 

 

Post a Comment

0 Comments