WALIMU WATAKIWA KUBAINISHA AINA ZA ULEMAVU WA WANAFUNZI ILI KUIRAHISISHIA SERIKALI KUTOA MSAADA.

 



📌DOTTO KWILASA.

WALIMU wakuu wa shule za msingi nchini wametakiwa kubainisha aina za ulemavu wa wanafunzi ili kuirahisishia Serikali kuwasaidia watoto hao kulingana na aina ya ulemavu walionao.

 Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa elimu Maalum kutoka Wizara ya Elimu ,Sayansi na Teknolojia Dk.Magret Matonya wakati wa kufunga Mkutano wa Pili wa walimu wakuu wa shule za msingi Tanzania Bara (TAPSHA).

 Aidha mkutano huo wa siku mbili  uliowakutanisha walimu 314 ulikua na lengo la kuwaunganisha walimu na kubadilishana uzoefu ikiwa ni pamoja na kujadili changamoto mbalimbali za kielimu ili kuendelea kuinua kiwango Cha elimu Tanzania.

 Akieleza zaidi Dk.Matonya amesema,watoto wengi wenye mahitaji ya elimu Maalum hawapatiwi huduma zao za msingi Kutokana na taarifa zao kutowekwa wazi kutokana na sababu mbalimbali huku baadhi ya walimu wakuu wa shule za msingi wakiwa chanzo kikuu.

 "Serikali yetu haina ubaguzi,inahitaji kuwahudumia watoto wote lakini kwa bahati mbaya ninyi walimu mnashindwa kuwasilisha taarifa zao,kuna wanafunzi wengine wana ulemavu zaidi ya aina moja ya ulemavu hivyo taarifa zao pia zinapaswa kuzingatiwa,"anasema.

 Mkurugenzi huyo wa elimu Maalum ameeleza kuwa ,jamii ya watanzania imezungukwa na watoto Wenye aina nyingi za ulemavu ambazo Wakati mwingine sio rahisi kuzibaini hivyo kuwataka walimu wakuu nchini kuwa makini wakati wa usajili.

 "Tafadhali niwaombe muwapokee watoto wote kisha  wapelekwe kwenye hospitali za Halmashauri ili kubainisha aina za ulemavu wa watoto na kuwapangia shule husika kwa kuzingatia aina ya mtu na ulemavu alionao,"anasisitiza.

 Mbali na hayo ,Dk.Matonya amebainisha Kuwa licha ya Serikali kuwapa kipaumbele watoto Wenye mahitaji Maalum bado kuna walimu wakuuu wanakataa kuwasajili .

 "Hatutamvumilia mwalimu yeyote ambaye atakataa kumsajili mtoto mwenye ulemavu,nawakumbusha kuwa kila mtoto anahitaji elimu bila kubaguliwa kwani sisi tunaamini watoto wte ni sawa,”anasema na kuongeza;

 “Kila mtoto anahitaji mwalimu ambaye anaendeleza kwa vitendo ujumuishi katika elimu na ndio maana Serikali inapanua uelewa wa Walimu kuhusu Ujumuishi ili kuwasaidia kikamilifu wanafunzi waliotengwa kama vile walemavu wa kutosikia au wenye vilema vingine,”alisema.

 Kutokana na hayo,Naibu waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia Omary Kipanga amesema kuwa Serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania itaendelea kusimamia maboresho ya upatikanaji wa elimu ya msingi kwa kuzingatia maadili ya haki za binadamu bila ubaguzi ikiwa ni pamoja na kuweka miundombinu rafiki ya kufundishia.

 Katika kufanikisha hilo ,alieleza kuwa imefanya maboresho kwa shule za msingi kwa kusambaza vitabu vya kiada na ziada kwa nchi nzima kwa kuzingatia uwiano wa kitabu kimoja kwa wanafunzi wawili huku lengo likiwa ni kitabu kimoja kwa kila mwanafunzi.

 Mbali na hilo, Serikali katika kuhakikisha elimu inakua bora zaidi kwa kuzingatia usawa kwa watoto wote ,imeongeza uchapaji na usambazaji wa  vitabu kwa wanafunzi wenye mahitaji ya elimu maalum kwa uwiano wa moja kwa moja nchi nzima.

Aidha ameeleza kuwa  ili kurahisisha upatikanaji na kupunguza gharama za uchapaji wa vitabu vya kiada , zida na machapisho ya kielimu, tayari Wizara imepokea mashine ya kubwa ya kisasa  yenye thamani ya shilingi bilioni 6.9.

 Hatua hiyo itaimarisha upatikanaji wa vitabu kupitia huduma ya maktaba mtandao ambapo wanafunzi wanapata vitabu hivyo moja kwa moja kwa njia ya mtandao lengo ni kumwezesha mwanafunzi kujisomea na kuimarisha utamaduni wa kujisomea bila kusukumwa.

 “Pamoja na jitihada zote hizi ifahamike kuwa mafanikio katika elimu yanategemea sana mwalimu kwani ana mchango mkubwa wa kuchangia katika ufaulu au kufeli kwa mwananfunzi,”anasema

 Kwa upande wake Mkurugenzi wa Elimu,Sekondari kutoka OR-TAMISEMI ambao ndio waandaaji na wasimamizi wakuu wa Mkutano huo wa TAPSHA Benjamini Oganga alieleza umuhimu wa walimu kwa shule za msingi kuwa ndio nguzo ya mafanikio ya wanafunzi wa Sekondari.

 “Kila mwaka kwa miaka mitano mfululizo darasa la saba wamekuwa na takwimu nzuri za ufaulu wa mitihani yao ya mwisho ambapo kwa mwaka huu wanafunzi laki nane wanaingia kidato cha kwanza kwa nchi nzima,”anasema.

 Naye Mwenyekiti wa TAPSHA Mwl.Rehema Ramole ameishukuru serikali kwa kuwajali walimu kwa kuwapatia stahiki zao na kusema kuwa wana deni kubwa la kuhakikisha wanatekeleza misingi ya elimu kwa watoto  .

 “Tukitoka hapa kazi yetu ni moja kuwafikishia wenzetu tuliyojifunza kuleta mabadiliko chanya kwenye elimu ya msingi,”anasema.

Post a Comment

0 Comments