SERIKALI HAINA MPANGO WA KUPOKEA CHANJO ZA COVID 19:

 


📌HAMIDA RAMADHANI.

SERIKALI imesema kuwa kwa sasa haina mpango wa kupokea chanjo ya ugonjwa wa Corona (COVID 19) inayoripotiwa kuwepo na kutumika katika mataifa mengine.

Hayo yamebainishwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk. Doroth Gwajima, wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma.

Dk, Gwajima amesema kuwa, kutokana na mlipuko wa pili wa ugonjwa wa corona katika mataifa jirani, amekuwa akipokea maswali mengi kutoka vyombo vya habari kuhusu matumizi ya chanjo hiyo, pamoja na njia za kujikinga.

“Naomba ifahamike kuwa serikali kupitia wizara ya Afya inazo taratibu zake za kufuata pale inapotaka kupokea bidhaa yoyote ya afya na hufanyika baada ya serikali kijiridhisha hivyo sasa ni hadi tujiridhishe na siyo vinginevyo”ameeleza Dk, Gwajima

Amesema, kuhusu mbinu za kujikinga na ugonjwa huo Wizara inaendelea kuwakumbusha wananchi kujielekeza kwenye elimu ambayo imekuwa ikitolewa na wataalamu wa afya.

“Hii ni pamoja na kuimarisha usafi, kujifukiza, kufanya mazoezi, kula lishe bora, kunywa maji mengi bila kusahau matumizi ya tiba asili ambazo taifa hili limejaliwa”amesema Dk. Gwajima

Amesema Wizara kwa kushirikina na Mkemia Mkuu wa Serikali na Baraza la tiba asili na wananchi watengenezaji wa tiba ya asili tayari wameshafanya usajili wa bidhaa za tiba asili.

Dk, Gwajima alisema kuwa upo ushahidi wa kutosha kuhusu watu wengi ambao wamepata nafuu na kupona magonjwa mbalimbali ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza mara baada ya kutumia dawa za tiba ya asili hataka kama walikuwa kwenye matibabu ya hospitali

“Naomba wataalamu wote na wajuzi wa tiba asili wasisite kujitokeza kufuata taratibu za kuwasilisha dawa na bidhaa zao kwa mamlaka ya maabara ya Mkemia Mkuu wa serikali ili zifanyiwe uchunguzi “amesisitiza Waziri huyo wa Afya.

Amesema Wizara hiyo, itawapa ushirikiano mkubwa wote watakajitokeza na kujiandikisha kupitia madawati ya tiba asili yaliyoko katika halmashauri na mikoa.

“Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto imedhamiria kuinua huduma za tiba ya asili”amebainisha

Kadhalika, amesema kuwa analielekeza Baraza la tiba asili kutoa orodha ya dawa zote ambazo zimepita kwenye utaratibu wa kufanya uchunguzi wa kimaabara na maabara ya Mkemia Mkuu wa serikali na kuonekana kuwa ni salama.

“Ifahamike kuwa dawa nyingi zinazotumika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya zinatokana na miti au mimea kwa mfano dawa ya kwinini inatengenezwa kutokana na  mti wa mkwinini ambao hapa Tanzania unastawi maeneo ya Lushoto, Korogwe na Mufindi”amefafanua Dk, Gwajima

Pia, amesema kuwa serikali itaendelea kuchukua tahadhari zote za ufuatiliaji wa mwenendo wa magonjwa yote kama ambavyo imekuwa ikifanya siku zote na kuelimisha wananchi juu ya hatua za kuchukua.

“Nawaelekeza Waganga wakuu wa Mikoa, Wilaya na Waganga wafawidhi na Maafisa afya mazingira nchini kote, kuendelea kuimarisha mifumo yote ya udhibiti na kinga ya magonjwa kwa kushirikiana na wananchi ili kudhibiti magonjwa yote ya kuambukiza na yasiyo ambukiza”alisema Dk. Gwajima

Hata hivyo, amezikumbusha Taasisi zote za Umma, Binafsi, Kidini, Kijamii na Vyombo vya habari kuepuka kutoa taarifa za afya ambazo hazifuati miongozo ya wizara zinazoleta taharuki kwa wananchi.

“Ieleweke kuwa taasisi zetu zote kama shule, vyuo, taasisi za kijamii na kidini zinawajibika kwa Wizara zao husika katika kutoa taarifa zozote au kuchukua maamuzi yanayoweza kugusa maisha ya wananchi wengine”ameeleza

Mwisho

 

 

 

 

Post a Comment

0 Comments