SERIKALI YALEGEZA MASHARTI MIKOPO ASILIMIA 10



📌ATLEY KUNI-TAMISEMI

SERIKALI imelegeza masharti ya kukopa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa halmashauri kwa vikundi vya wanawake, vijana na walemavu ili kuviwezesha vikundi vingi zaidi kukopa.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Selemani Jafo wakati akifunga mkutano mkuu wa nne wa maafisa maendeleo jamii.

Waziri Jafo amesema kuanzia leo tarehe 26 Februari, 2021, Serikali imerekebisha na kutoa kanuni mpya ambazo zimechapishwa kwenye gazeti la Serikali ili zianze kutumika na kuwa moja ya kigezo kilicholegezwa ni kupungua kwa idadi ya wanavikundi.

“Kigezo cha kuwa na idadi ya watu kumi kwa vijana na wanawake na watu watano kwa walemavu, kwa muda mrefu kimechangia kwa baadhi ya watu waliokubaliana na malengo yanayofanana kushindwa kuungana.”

“Kanuni mpya zinasema kwa vikundi ya vijana na kina mama wakipatikana watano kikundi hicho kinaweza kukopesheka, lakini tumeenda mbali zaidi kubadilisha kanuni kumwezesha hata mtu mmoja mwenye ulemavu aweza kupewa mkopo, haya ni mapinduzi makubwa,” amesema Waziri Jafo

Amesema kuanza kutumika kwa kanuni hizo mpya kutatoa fursa kwa vikundi vingi kuwa na sifa ya kupata mikopo hiyo.

Waziri Jafo katika eneo lingine ambalo limeimarishwa ni suala la urahisishwaji wa ufuatiliaji wa mikopo kwa Serikali kwa kutenga fungu kulingana na ukopeshaji wa kila mamlaka.

Kuanzia sasa kanuni mpya zinaelekeza kwa kila halmashauri kutenga kiasi cha fedha ili kuwawezesha maafisa maendeleo jamii kufanya tathmini na ufuatiliaji wa mikopo iliyotolewa

Akifafanua zaidi, Waziri Jafo amesema kwa halmashauri ambazo mapato yake ya ndani hayazidi shilingi bilioni moja katika kila marejesho idara ya Maendeleo ya Jamii itatengewa shilingi laki tano wakati halmashauri ambazo mapato yake ni zaidi shilingi bilioni moja zimeelekezwa kutenga kati ya Sh milioni moja na shilingi milioni moja na nusu kwa mwezi kwa ajili ya ufuatiliaji.

Aidha kwa halmashauri ambazo mapato yake yapo kati shilingi bilioni tano, na kuendelea amesema idara ya maendeleo ya jamii ipatiwe shilingi milioni tano kwa ajili ya tathmini na ufuatiliaji.

Sambamba na maboresho hayo, waziri Jafo amewataka, wataalamu wa kada hiyo, kwenda kusimamia ipasavyo marejesho ya mikopo na atakayeshindwa kufanya hivyo, basi atakuwa ameshindwa kazi.

Katika hatua nyingine Waziri Jafo, ameziagiza Mamalaka za Serikali za Mitaa, kuhakikisha wanawahusisha wataalamu wa Maendeleo ya Jamii, kwenye Miradi yote inayotekelezwa katika eneo husika kuanzia hatua za awali.

Amesema kutokana na umuhimu wa Maafisa Maendeleo Jamii kama wahamasishaji wa Jamii kwenye shughuli za Maendeleo, ameziagiza Mamlaka za Serikali za Mitaa, kuwashikisha wataalam wa kada hii katika miradi yote inayotekelezwa.

Kufuatia kauli hiyo ya Waziri Jafo, akizungumza kwa niaba ya Maafisa Maendeleo Jamii wenzake, rais mpya wa chama hicho Angela Kiama, amesema wamepokea kwa furaha mabadiliko ambayo serikali imeyafanya katika kanuni.

Tatizo lilikuwepo mathalani kwa walemavu, unaweza kukuta mlemavu mmoja katika eneo anashindwa kupewa mkopo kwa kigezo cha kuwataka wawe kikundi, kwa kweli tunaishukuru sana serikali kwa kuliona hili na kufanya maboresho kwenye kanuni hizo.

 Kiama.

Maafisa Maendeleo Jamii hao waliokutana kwa siku tatu kutathmini hali ya utendaji wao wa kazi sambamba na kuwachagua viongozi wa chama chao.

Mkutano mkuu wa Maafisa Maendeleo ya Jamii, ni wa nne tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 2017, na ulikuwa na kauli mbiu, “Maafisa Maendeleo ya Jamii Nguzo Muhimu kufikia Uchumi wa Viwanda” huku ukiwa umewashirikisha maafisa wa kada hiyo kutoka serikalini na taasisi binafsi.

 


Post a Comment

0 Comments