WALIOSHIRIKI KATIKA MAKOSA YA UPATU KUTOREJESHEWA FEDHA ZAO

 


📌FAUSTINE GIMU GALAFONI

MKURUGENZI wa Mashtaka  hapa nchini ,Biswalo Mganga ametoa maelekezo kwa vyombo vyote vya upelelezi nchini kutorejesha fedha kwa watu walioshiriki katika makosa ya upatu .

Mkurugenzi huyo wa Mashtaka amebainisha hayo Machi,15,2021 jijini Dodoma  wakati akizungumza na Waandishi wa Habari  kuhusu kuibuka upya kwa biashara haramu ya upatu  hapa nchini kwa kupitia mitandao .

“Kwa kuzingatia masharti yaliyoainishwa katika ibara ya 59B  ya katiba ya jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977  na vifungu vya 8 na 9[1][c] vya sheria ya usimamizi wa mashtaka   [Sura ya 430  Marejeo ya  2019],ninatoa  maelekezo kwa vyombo vyote vya  upelelezi  kutorejesha fedha  kwa watu walioshiriki katika makosa ya upatu,amesema.

Mkurugenzi huyo wa mashtaka amesema siku za  hivi karibuni ,kumekuwa na wimbi kubwa la mipango ya udanganyifu inayodai kutoa fursa za uwekezaji  na biashara kwa wananchi   ambayo imekuwa ikiwaaminisha  kupata faida  kubwa kwa kipindi kifupi  na wanaojiunga  wanahamasishwa kushawishi watu wengine  kujiunga na mipango hiyo  na waendeshaji wa mipango hiyo  wamekuwa na desturi ya kutumia watu wenye ushawishi  kwenye jamii kama vile viongozi wa dini ili kujenga imani na kuvutia washiriki wapya.

“Mipango hii inafanyika pasipo kupata idhini ama vibali  kutoka katika mamlaka  za serikali  na hawana ofisi  rasmi  zinazotambulika  katika uendeshaji wa shughuli zao ,hivyo napenda kuchukua fursa hii kuutahadharisha umma juu ya mipango hiyo danganyifu  inayopotosha umma kuwa ni uwekezaji halali  wakati ni biashara haramu ya upatu na mipango hii imekuwa ikitangazwa kupitia mikutano  ya uhamasishaji na mitandao ya kijamii,amesema.

Hivyo,Mganga amesema hiyo ni biashara haramu ya upatu [Pyramid schemes] na ni kosa la jinai chini ya vifungu vya 171A,171B,171C vya   sheria ya kanuni ya Adhabu ,Sura ya 16]  na vinakiuka masharti ya sheria ya Benki na taasisi za kifedha  Na.5 ya mwaka 2006 inayokataza  mtu yeyote  kupokea miamala ya kifedha  toka kwenye umma bila leseni.

Ikumbukwe kuwa ,kujihusisha na mipango hii  ni kosa la jinai sio tu kwa anayehamasisha na kupokea fedha ,bali hata kwa wanaotoa fedha hizo ,hivyo wanaoshiriki katika biashara hizo wapo katika hatari kupoteza fedha zao  pamoja na kushtakiwa mahakamani  kwa kosa la kushiriki biashara haramu ya upatu,amesema.

Mkurugenzi huyo wa mashtaka ameendelea kufafanua kuwa mipango hiyo ni ya kilaghai  na imewahi kujitokeza   siku za nyuma   na kusababisha wananchi wengi kupoteza  fedha zao  huku akizitaja kampuni   zilizoshiriki katika udanganyifu wa michezo ya upatu ni pamoja na Rifaro   Africa,IMS,D9,Miradi ya kuku  kupitia kampuni ya Mr Kuku na Development  Entreneurship Initiative [DECI].

Amebainisha kuwa kwa sasa mipango hiyo  imeibuka kwa sura mpya  kama biashara ya kimtandao  na wananchi wanaalikwa kushiriki  na kuwashawishi wengine  kujiunga  huku akitolea mfano kampuni ya QNET  LIMITED.

“Kampuni hii imefunguliwa nchini Hong Kong  na inajihusisha na biashara ya kuuza  bidhaa kwa njia ya mtandao  kupitia anwani yao ya  WWW.qnet.net imeweka masharti mawili  kwa anayetaka kujiunga na biashara yao ,kwanza wanataka kuhudhuria   mafunzo ya kumwezesha kuwa mwanachama  na pili mwanachama mpya analazimika kushawishi wengine  kujiunga na kununua bidhaa  za kampuni hiyo na anayefanikiwa  kushawishi wengine kujiunga anapewa ahadi ya kupata kamisheni ,amefafanua.

Mkurugenzi huyo wa mashtaka ameendelea kusema kuwa mnamo tarehe 1,Februari ,2021 kampuni hiyo ilimwandikia barua  katibu mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara na kumpatia nakala mkurugenzi wa mashtaka huku ikimtaka kuchukua hatua za kulinda mazingira ya kampuni hiyo  kufanya biashara nchini   ili kuipa hakikisho  la kutokubughudhiwa  na vyombo  ama mamlaka za serikali   ambapo amesema hilo sio moja ya jukumu la mkurugenzi wa mashtaka.

“Biashara inayofanywa na kampuni hii ni biashara haramu ya upatu  ambayo ni kosa la jinai ,kwa muktadha huo siwezi kulinda wahalifu ama kuweka mazingira mazuri ya wahalifu  kuendelea kutenda vitendo vya kihalifu ,kwa msingi huo nimeagiza vyombo vya vya upelelezi   kufanya upelelezi wa kina ikiwa ni pamoja na kuwakamata  na kuwahoji wote wanaohusika na nimebaini baadhi ya taasisi za serikali zimekuwa zikirejesha fedha    kwa baadhi ya watu wanaodaiwa  kuwa ni wahanga   wa uhalifu huo wa upatu “amesema.

 

Post a Comment

0 Comments