KAMATI YA BUNGE MADINI YARIDHISHWA NA KANUNI ZINAZOSIMAMIA SEKTA YA MADINI

 


📌MWANDISHI WETU

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeeleza kuridhishwa kwake na Kanuni zinazosimamia Sekta ya Madini na kueleza kuwa, marekebisho kidogo yaliyopo hayazuii Sekta kufanya kazi.

Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini, Dunstan Kitandula Aprili 17, 2021 jijini Dodoma wakati akizungumza na Waandishi wa Habari mara baada ya Kamati hiyo kujengewa uelewa kuhusu Kanuni mbalimbali zinazosimamia Sekta ya Madini.

Amesema kuwa, upo umuhimu wa Kamati hiyo kupatiwa elimu  kwani ndiyo inayofanya kazi kwa niaba ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hivyo elimu hiyo itaiwezesha  Kamati husika kuisimamia Sekta ipasavyo ikiwemo kuisadia Serikali katika usimamizi wa Sekta  ya Madini.

Tunapokutana kama hivi tunapata nafasi ya kuangalia ni namna gani Kanuni hizi zinafanya kazi, zinachangia vipi kwenye maendeleo na ukuaji wa sekta lakini pia tunapata nafasi ya kuona changamoto na kushauri Serikali namna ya kuzitatua.

 Kitandula.


Katika Semina hiyo, Kamati hiyo ya Bunge imeelimishwa kuhusu Sheria ya Madini Sura ya 123 na Marekebisho yake yaliyofanyika Mwaka 2007, Kanuni mbalimbali  zikiwemo Kanuni za Masoko ya Madini,  Kanuni za Madini  (Biashara ya Almasi) za Mwaka 2019,  Kanuni za Madini (Udhibiti wa  Eneo Tengefu la Mirerani ya Mwaka 2019 na Sheria ya Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali  Madini, Mafuta na Gesi Asilia).

Naye, Waziri wa Madini Doto Biteko akizungumza katika Semina hiyo, amesema kuwa, kama nchi imepiga hatua katika utekelezaji wa Matakwa 18  ya Kimataifa  kuhusu Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali Madini, Mafuta na Gesi Asilia na kueleza kuwa, ni maeneo 7 tu kati ya 18 ambayo bado yanaendelea kutekelezwa na Wizara.

Kauli hiyo ya Waziri ni ufafanuzi baada ya Kamati hiyo kutaka kujua ni kwa namna gani Serikali imetekeleza matakwa ya Sheria ya Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali za Madini, Mafuta na Gesi Asilia Tanzania (TEITA) ya Mwaka 2015.

Akizungumzia Semina hiyo amesema inalenga kujenga uelewa wa pamoja ili kuiwezesha Kamati husika kuifahamu vizuri sekta na hivyo kuishauri Wizara ipasavyo na hatimaye kuiwezesha sekta kusonga mbele.


Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Madini Sura ya 123, Mkurugenzi wa Huduma za Sheria Wizara ya Madini Edwin Igenge, ameieleza Kamati hiyo kuhusu historia ya mabadiliko   ya Sheria ya Madini  kabla na baada ya Uhuru ikiwemo kubainisha mapungufu kadhaa ambayo yalipelekea kufanyika kwa Mabadiliko  Makubwa Mwaka 2017.

Igenge ameeleza kuwa, Mabadiliko ya Mwaka 2017 yaliwezesha kutungwa kwa Sheria za Kulinda Maliasili za Nchi  na hivyo kuwezesha umiliki wa  Rasilimali Madini, Mafuta na Gesi Asilia kwa wananchi chini ya usimamizi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa niaba ya wananchi.

 Akiwasilisha kuhusu Kanuni za Masoko ya Madini, Afisa Sheria Wizara ya Madini Damian Kaseko, ameileza Kamati hiyo kuhusu masuala kadhaa ikiwemo taratibu za uanzishwaji wa masoko ya madini, namna masoko hayo yanavyofanya kazi, utatuzi wa migogoro inayotokana na shughuli katika masoko, utaifishaji wa madini kwa mujibu wa Kanuni za Masoko pamoja na mambo mengine.

 

Post a Comment

0 Comments