MITAMBO YA KUFUA HEWA TIBA (OKSIJENI) YASIMIKWA HOSPITAL 7 ZA RUFAA,KUPAMBANA NA MATATIZO YA UPUMUAJI

 


Waziri wa Afya Dkt. Dorothy Gwajima akikagua mitambo ya kufua hewa tiba (Oksijeni) iliyosimikwa Kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Dodoma


📌CATHERINE SUNGURA-WAMJW

SERIKALI  imeweza kujibu changamoto za wataalamu wa afya katika hospitali saba za rufaa za mikoa ili kuwahudumia kwa ufanisi wagonjwa wa dharura kwa kuimarisha  kwa kusimika  mitambo ya kufua  hewa tiba (Oksijeni) na hivyo kupunguza gharama za uendeshaji wa hospitali hizo na kuwezesha hospitali zingine za halmashauri na vituo vya afya.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima wakati alipotembelea hospitali ya rufaa ya mkoa Dodoma kujionea jinsi walivyounganisha mitambo hiyo kwenye wodi ya wagonjwa mahututi  na  watoto.

Dkt.Gwajima amesema mitambo hiyo ambayo Serikali kwa kushirikiana na Benki Kuu ya Dunia hivi sasa imefungwa kwenye hospitali za rufaa za mikoa saba ya Dodoma, Mtwara ,Manyara, Mbeya, Amana Geita na Songea na hivyo wizara yake ipo njiani kukamilisha kufungia hospitali zote za rufaa za mikoa hapa nchini.

Mitambo hii  imefungwa kwa gharama  isiyopungua bilioni 1.4 kila hospitali na inalenga kuzalisha mitungi 200 ya hewa hiyo kwa masaa 24 , na kila mtambo unayo sehemu  ya mabomba yenye mita 400 yanayosafirisha hewa hii pia mitungi 73 imenunuliwa pamoja na mitambo hii kwa hivyo,  haya ni mapinduzi makubwa

Dkt.Gwajima



Mmoja wa Wazazi wa Watoto waliolazwa Kwenye hospitali hiyo akiongea na Waziri wa Wizara ya Afya Dkt.  Dorothy Gwajima wakati alipotbelea wodi hiyo na kujionea jinsi Oksijeni ilivyounganishwa wodini

Aidha, Dkt. Gwajima amefurahishwa na uongozi wa hospitali hiyo kwa kukamilisha kufunga  mitambo hiyo  na kuanza kutoa huduma kwenye wodi ya wagonjwa mahututi(ICU) pamoja na wodi ya watoto na hivyo wameweza  kuunganisha vitanda 78 kutoka vitanda 10 vya awali na kufanya jumla ya vitanda 88 kupatiwa huduma hiyo hospitalini hapo.

Hatua hii itapunguza  kwa kiwango kikubwa  gharama za  kuhudumia mgonjwa  mwenye mahitaji ya hewa hii. Wito wangu  tuitumie vizuri na kuzingatia na kuhakikisha  matengenezo kinga  yanafanyika kwa ufanisi.

Dkt. Gwajima amesema kuwa uwekezaji huo umeweza kujibu changamoto  ya kipindi cha mlipuko wa Covid-19 ulioripotiwa  nchini mwezi Machi mwaka 2020 na hivyo kusababisha kuongezeka kwa mahitaji ya hewa ya oksijeni na kuwa gharama zake zilipanda.

“Niwapongeze sana waganga wafawidhi wa hospitali za rufaa za mikoa kwa kuja na wazo hili la kufunga mitambo hiyo kwenye hospitali zetu na hivyo tutaweza kusaidia hospitali za wilaya na vituo vya afya na hivyo kuwapunguzia matumizi ya fedha ya kununua oksijeni, haya ni mapinduzi makubwa kwa Serikali yetu”. Alisisitiza Dkt. Gwajima

Kwa upande kwa kuepuka magonjwa ya kuambukiza ambayo  yameanza kuyakumba mataifa mengine, Waziri huyo aliwataka waganga wakuu wa mikoa na wafawidhi kwenye hospitali za rufaa za mikoa kuendelea kutoa elimu kwa umma kwa kutumia vyombo vya radio vilivyopo kwenye maeneo yao (Community radio) ili kuwaondolea wananchi hofu na kuendelea kuchukua tahadhari ya kujikinga na magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza ikiwemo janga la Corona.

Serikali kupitia sekta ya afya  kwa kushirikia na wadau wake nchini iko makini  kufuatilia kinachoendela duniani na kuchukua  hatua mbalimbali  za kuhakikisha nchi yetu  inaendelea kuwa salama na imara  katika kudhibiti  milipuko ya magonjwa  mbalimbali ikiwemo  huu wa Covid-19

 Dkt. Gwajima.

Dkt. Gwajima aliwakumbusha wadau,wataalam pamoja na wananchi wote kuendelea kuchukua  tahadhari muhimu ambazo zimekuwa  zikielimishwa mara kwa mara  dhidi ya kujikinga  na kudhibiti magonjwa mbalimbali ikiwemo Covid-19 kwa kuepuka hofu, kuimarisha tabia  ya kunawa mikono mara kwa mara  kwa maji safi tiririka na sabuni, kufanya mazoezi,kula lishe  au vyakula vya mbogamboga kwa wingi na matunda,kutumia tiba asili, kuepuka misongamano isiyo ya lazima  na mwisho kuwahi kwenye vituo vya kutolea huduma za afya  mara unapoona dalili za maradhi yeyote.

Naye Mganga Mfawidhi wa hospitali ya rufaa ya mkoa Dodoma Dkt. Ernest Ibenzi amesema  wanatarajia kufunga mitambo  ya kujazia hewa tiba hiyo ili kuweza kusaidia vituo vya afya vilivyo jirani na kusambaza huduma hiyo kwenye hospitali nzima.

Post a Comment

0 Comments