CCM YASISITIZA BAJETI IGUSE KILIMO, ARDHI NA NISHATI

 




📌RHODA SIMBA

CHAMA Cha Mapinduzi CCM kimetoa msisitizo kwa Serikali  katika bajeti ya  fedha  kwa mwaka 2021,2022 izingatie katika  sekta kubwa tatu, za Ardhi, Kilimo na Nishati.

Hayo yamesemwa leo jijini Dodoma na Katibu wa Chama Cha Mapinduzi CCM Daniel Chongolo wakati akizungumza na waandishi wa habari kwa mara ya kwanza tangu alipochaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa chama hicho.

Chongolo amesema  tangu alipochaguliwa kushika nyadhifa hiyo moja kwa moja alianza kufanya kazi  kwenye uchaguzi mdogo uliyofanyika  katika majimbo ya Muhambwe na Buhigwe na kata 17 katika maeneo tofauti hapa nchini.

Aidha amesema   katika kipindi hiki cha Bunge la bajeti wao kama chama wanaikumbusha Serikali izingatie vipaumbele na maeneo muhimu ndani ya bajeti hizo kama ilani ya CCM 2020/2025 inavyoeleza.

“Kazi hii ya kuikumbusha Serikali kuzingatia  maeneo muhimu tunaifanya kutokana na ukweli kwamba yamekuwapo manung’uniko kadhaa kutoka kwa wananchi kutoka katika baadhi ya maeneo nchini licha ya chama kuahidi kwenye ilani yake,

“ Hapa nataka kuwaahidi wananchi kwamba CCM ndiyo iliyobeba dhamira kwasemea wao na kwamba jukumu hilo tutalifanya kwa ustadi na kusimamia srikali zote mbili kuhakikisha hili lina fanikiwa” amesema Chongolo.

Katika wizara ya ardhi amesema  kutokana na malalamiko ya wananchi ya umiliki wa ardhi zao kuwa na tija katika umiliki huo CCM katika ilani ya 2020/2025 ibara ya 74  kimeeleza serikali ihakikishe inaongeza  kasi ya utoaji wa hati miliki  za ardhi mjini na hati za kimila vijijini ili kuwawezesha  wananchi  kumiliki kisheria maeneo  ili wananchi wawe huru na maeneo yao.

Amesema CCM inaelekeza Serikali kuhakikisha inawalipa fidia stahiki na kwa wakati wananchi walio twaliwa  maeneo yao kwa shughuli za Umma na kinaelekeza uimarishwaji  wa mfuko wa fidia na Serikali,

“Pia viongozi wote wa serikali kuanzia ngazi za mtaa kijiji, mpaka wizara wahakikishe wanatatua migogoro ya ardhi kwa haki na wakati Chama  kinaielekeza kumaliza haraka migogoro ya ardhi katika wilaya za Kondoa,Ngorongoro Kiteto Kongwa Morogoro Kinondoni na pembezoni mwa hifadhi mbalimbali”amesema Chongolo

Katika upande wa Wizara ya Kilimo Chongolo amesema  kutokana na changamoto ya mbegu ambayo imekua ikiwasumbua wakulima chama kimeielekeza serikali kuongeza bajeti ya mbegu na taasisi zote zinazofanya utafiti zihusishwe kama zilivyoorodheshwa ndani ya ilani ibara ya 37 kifungu b na a.

Aidha ameeleza makampuni ya taasisi za uzalishaji bora wa mbegu kama TARI, TOSCI na ASA ziwezeshwe ili kuongeza tija katika uzalishaji bora wa mbegu .

‘’Ili kukuza masoko ya mazao yetu katika nchi jirani chama kinaelekeza serikali kupitia wizara ya kilimo,ujenzi wa ghala za kimkakati mipakani mfano katika mpaka wa Namangan a Mtukula ili kuimarisha uuzaji wa mazao nje ya nchi.’’amesema 

Chongolo amesema ili kukuza wakulima nchini serikali ihakikishe inatoa mikopo ya pembejeo yenye masharti nafuu kwa wakulima  ikiwemo mitambo ya mashambani pembejeo za kilimo  matrekta ya mikono zana za pembejeo ,zana za usindikaji ,matunda mbogamboga, mazao mengine  na vifungashio vya mazao.

Katika upande wa Wizara ya Nishati chama kimeiagiza Serikali kuhakikisha vijiji vyote ambavyo havijapata umeme vinapata umeme kwa mwaka huu wa fedha .

‘’Vijiji na vitongoji vilivyo rukwa na awamu za usambazaji wa umeme zilizopita navyo vipate umeme 

mathalani katika vijiji vya chihanga ,nzasa na kiterela hapa jijini Dodoma pamoja na Mikoa mingine’’amesema Chongolo.

Pia Chama kimeielekeza Serikali ihakikishe kuwa kero zote na urasmu unaokera wananchi katika kuunganisha umeme unaondoka  mara moja huku gharama za nguzo ,mita na Ankara za malipo ya umeme zinaondoshwa kwani zimekuwa ni mzigo kwa wananchi.

Hata hivyo amesema kutokana na mahitaji ya umeme kwa wananchi chama kinaelekeza serikali kukamilisha miradi ya usambazaji wa umemem ikiwemo miradi ya rufiji chalinze ,Dodoma ,Kinyerezi hadi chalinze ,Geita ,Nyakanazi hadi kigoma ,Singida ,Arusha hadi Namanga.

Mbali na hayo ameielekeza Serikali kuhakikisha kunakuwepo na umeme wa kutosha na wa uhakika kwa ajili ya uendeshaji wa Reli ya Kisasa (SGR).

 

 

Post a Comment

0 Comments