📌 PENDO
MANGALA
WAZIRI wa Muungano na
Mazingira Seleman Jafo ameitaka jamii pamoja na Wadau mbalimbali kuhakikisha
wanazingatia suala zima la utunzaji wa mazingira ili kukabiliana na mabadiliko
ya Tabia nchi kwani nchi haiwezi kupata uchumi endelevu endapo itashindwa
kutunza mazingira.
Waziri Jafo ametoa
kauli hiyo Jijini Dodoma wakati alipokuwa akizungumza na Mashirika yasiyo ya
Kiserikali yanayojihusisha na masuala ya mazingira kwa lengo la kufahamiana
pamoja na kutengeneza mtandao wa utendaji kazi.
“ lengo la Serikali ni kuhamasisha
utendaji kazi wa Asasi hizo kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu stahiki
na kuimarisha uratibu wa shughuli za Usimamizi wa Mazingira nchini na kudumisha
mahusiano kati ya Ofisi ya Makamu wa Rais na Asasi zisizo za Kiserikali
zinazohusu Hifadhi ya Mazingira;”Alisema
Aidha amesema kama
Serikali wamekuwa na afua mbalimbali licha ya bajeti ya mazingira kuwa ndogo
lakini watahakikisha suala la mazingira wanalipa kipaumbele huku akiwataka
wadau hao kujikita zaidi katika usimamazi wa mazingira kwa kushirikiana
na Serikali ili kuratibu shughuli za Mazingira kwa ufanisi zaidi katika Mikoa
yote..
“Nafahamu, nyinyi
mmekuwa wadau wakubwa katika hifadhi ya mazingira nchini na mmekuwa mkijitoa
katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoaji wa elimu kwa umma kuhusu
agenda hii muhimu ya mazingira kwa mustakabali wa vizazi vya sasa na vizazi
vijavyo,” Waziri Jafo alisisitiza.
Hata hivyo Waziri Jafo
amezitaka asasi hizo kusogeza huduma katika maeneo mengi nchini ili kuleta tija
na kupambana na uharibifu wa mazingira ambao kwa kiasi kikubwa unasababishwa na
shughuli za kibanadamu zisizo endelevu.
“Ndugu zangu hatuwezi kupata uchumi endelevubila kudhibiti mazingira yetu, uharibifu wa mazingira duniani ni wakutisha, athari za mabadiliko ya tabianchi nsi kubwa na kumekuwa na ongezeko la kina cha maji katika Mito, Mabwawa na Maziwa kutokana kuongezeka kwa mvua juu ya wastani,” Jafo alisisitiza.
Kwa upande wake
Mkurugenzi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira,Dk
Andrew Komba amesema kuwa Serikali imekuwa na miongozo mbalimbali ya mazingira
ikiwemo Sera ya Mazingira pamoja na mpango wa maendeleo huku akisema
vipaumbele vya Serikali ni kumaliza changamoto za utendaji kazi na
Asasi za kiraia.
Amesema kuwa kikao
hicho kimefungua sura mpya baina ya Asasi hizo za kiraia na Serikali
kwani hapo awali zimekuwa zikitekeleza mipango yake bila kuzingatia vipaumbele
vya Serikali.
Naye Mmoja wa
washiriki wa Mkutano huo Bi. Winifrida Shonde kutoka Asasi ya Tanzania Environment
and Empowerment Movement (TEEM) aliishauri Serikali kuhakikisha kila
Asasi ya kiraia kupewa majukumu ya kuainisha malengo katika hifadhi
ya mazingira.
“Naamini Serikali
kwakufanya hivi itasaidia kuweka utaratibu bayana wa utekelezaji wa shughuli za
usimamizi wa mazingira hapa nchini,”alisema
Katika kikao hicho
baina ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira na
Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali (NGOs, CSOs & CBOs) kimehusisha
takribani washiriki Mia Mbili kote nchini.
0 Comments