WAANDISHI WAASWA KUANDIKA HABARI CHANYA KUHUSU WATU WENYE ULEMAVU

 


📌RHODA SIMBA

KATIKA kuiwezesha jamii kuendelea kupata taarifa kuhusu watu wenye ulemavu mradi wa elimu  Jumuishi umetoa mafunzo kwa waandishi wa habari lengo likiwa ni kuwapa uelewa namna ya kuandika habari chanya kuhusu watu hao .

Aidha licha ya kuandika pia kuna lugha za kutumia wanapofanya mazungumzo nao,namna ya kuwafikia pamoja nakuelewana pindi wafanyapo mahojiano.

Hayo yamesemwa jijini hapa na Mkurugenzi Mtendaji kutoka kituo cha habari kuhusu ulemavu Fredrick Mkatambo katika mafunzo ya siku mbili ya mradi wa elimu jumuishi  kwa waandishi wa habari mradi Unaofadhiliwa na kanisa la Free Pentecoste na  information center on disability (IDC) mradi unaolenga zaidi watoto wenye ulemavu.

Mkatambo amesema ushawishi na utetezi kupitia waandishi wa habari itakuwa ni njia rahisi kuifikia jamii ambayo ndio inaishi na watu wenye ulemavu.

"Hii ni fursa  jinsi ya kufanya kazi  ya kusambaza elimu hii itasaidia sana kwa jamii kwani wengine wamekua wakiona aibu kwahiyo kupitia waandishi wa habari tunaamini tutaenda kufichua watu wenye  ulemavu,

"Haki za watoto, masuala ya kuwaficha badala ya kwenda shule kwasababu ya wazazi kuona aibu  serikali tu tunaendelea kuisistiza iendelee kuweka sera madhubuti katika kundi hili la watu wenye mahitaji maalum"amesema Mkatambo

Amesema suala la kupata elimu ni haki  ya kila mtu na linapokuja suala la elimu jumuishi hapa linakua linagusa makundi  yote ambapo utekelezaji wa sheria  ya watu wenye ulemavu ili kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu izingatiwe kwa usawa.

"Kwahiyo ndugu zangu waandishi wa habari  mkitumia kalamu zenu kupaza sauti tutafikia malengo tuliyokubaliana hapa kwani Serikali pia itaongeza bajeti kwa shule jumuishi ambazo watoto wenye ulemavu wanasoma,

“Hii ni kutokana na ukweli kwamba vifaa na nyenzo  za kujifunzia na kufundishia ni ghali" amesema Mkatambo

Amesema kumekuwepo na changamoto kwa waandishi wa habari pale wanapokua wakitekeleza majukumu yao hasa katika ushirikiano kwa walengwa kwaajili yao amesema wao wapo tayari kuungana na waandishi pale watapohitaji ushirikiano.

"Mfano katika masuala ya takwimu imekua changamoto lakini niwahakikishie popote penye changamoto mimi nipo hata mkinipigia simu nipo tayari kuwapa ushirikiano"

Akizungumzia kuhusu baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari kuweka vipindi vya watu wenye ulemavu amesema wamejitahidi kadri ya uwezo wao  na matokeo wameyaona ni mazuri.

Ila sasa nanyi waandishi wa habari niwaombe basi mkitaka kufanya vipindi hivyo msiweke nyimbo za huzuni wekeni za kawaida tuu kwani  kuna mwingine hapendi anaweza akatoa kabisa hata kipindi chenyewe asisikilize

"hata mfanyapo mazungumzo usibadili sauti utakuta kuna mtu mwingine anaanza kuongea kama anaongea na mtoto kuna lugha fulani hivi ayayaya jamani hizi kwakweli zinakuwa hazipendezi" amesema mkatambo

Hata hivyo licha ya kupata  mafunzo hayo  kwa waandishi  wa habari kuna mikakati itayoendelea ya kuibua matatizo ya watoto watu  wenye  ulemavu kwenye jamii ili  kuhakikisha tatizo la  jamii kutokuwa na elimu linapungua ama kuisha kabisa.


 

Post a Comment

0 Comments