BASHE AFURAHISHWA NA M-KILIMO INAVYOSAIDIA WAKULIMA

 


NAIBU Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amesema wizara imefanikiwa kutekeleza agizo la Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu utambuzi wa wakulima ambapo hadi sasa kupitia Mfumo wa M-Kilimo tayari wakulima 1,979,662 na Maafisa Ugani 6,840 wamesajiliwa kwenye mfumo hatua inayosaidia kufikisha huduma za ugani na masoko kwa haraka.

Bashe ametoa kauli hiyo leo (04.07.2021) wakati alipoongea na Waandishi wa habari ofisini kwake Dodoma ambapo amesema lengo la wizara ya kilimo ni kusajili wakulima takribani milioni 6 kupitia kaya zao hatua itakayosaidia utambuzi na ufikwishwaji wa huduma za ugani ili kuwezesha tija kwenye kilimo kupatikana.

Aliongeza kusema kuwa ili wizara iweze kuwahudumia wakulima ni lazima kuwatambua na kufahamu mahala walipo ndio maana ikaanzisha mfumo wa kiteknolojia wa usajili wa wakulima (M-Kilimo) ambao sasa umefika mikoa yote ya Tanzania Bara.

" Katika bajeti ya mwaka 2021/22 wizara imepanga kufundisha maafisa ugani (re-training) ili waweze kusaidia wakulima kuongeza tija kwenye uzalishaji mazao ambapo ili lengo hilo lifanikiwe lazima uwatambue wakulima ndio maana tumeanzisha mfumo huu wa Mobile Kilimo ambapo wakulima wanasajiliwa kupitia maafisa ugani kwenye kata." aliema Bashe.

Akizunguza juu ya umuhimu wa mfumo huo Naibu Waziri Bashe alisema mfumo M-Kilimo utasaidia kupima kazi zaMaafisa ugani Kilimo katika maeneo ya kiutendaji kwa kuwa takwimu zinaonesha kila ushauri alioutoa kwa mkulima ikiwa ni wa ana kwa ana (physical consultation) au kupitia njia ya mtandao (online consultation).

“ Hadi sasa jumla ya maswali ya wakulima yapatayo 7,792 yamepokelewa na kujibiwa na maafisa Ugani Kilimo kupitia mfumo wa M-Kilimo unaoratibiwa na Wizara ya Kilimo” alisisitiza Bashe na kuongeza kuwa wizara inatarajia kufungua kituo cha huduma kwa wakulima (Call Centre) kuwezesha wakulima kupiga simu na kujibiwa maswali yao kwa haraka zaidi.

Katika hatua nyingine Bashe ametaja mikoa iliyofanya vizuri kwenye usajili wa wakulima kuwa ni Morogoro (153,977), Njombe (153,158) na Mara (148,772) huku mikoa ambayo bado ipo chini ikiwa ni Pwani imesajili wakulima 14,784) na Mtwara (28,000) .

Kufuatia hatua hiyo Bashe ametoa wito kwa wakurugenzi wa halmashauri nchini kuwawezesha maafisa ugani wao wa wilaya kusajili na kuhamasisha wakulima ili waingie kwenye mfumo wa M-Kilimo kuwezesha kufikia lengo la kukuza tija kwenye uzalishaji mazao ya kilimo kupitia huduma bora za ugani.



Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Prof. Siza Tumbo (aliyesimama) akitoa taarifa kuhusu utendaji kazi wa mfumo wa M-Kilimo leo wakati Naibu Waziri Kilimo Mhe. Hussein Bashe ( kushoto) alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma.


Ili kuleta ufanisi kwenye usajili wa wakulima Naibu Waziri huyo wa wizara ya Kilimo alisema kupitia bajeti 2021/22 inatarajia kununua simu za mkononi za kisasa (smartphones ) na kuzigawa kwa Maafisa Ugani kote nchini ili zitumike kusajili wakulima  kwa kutumia teknolojia maalum (App)

Naye Mratibu wa Mfumo wa M-Kilimo Rajab Mkalange amesema mfumo huu ni wa kiteknolojia unaoweza kumsaidia mkulima kupata huduma za ugani na masoko kupitia maswali kwenye simu yake ya kiganjani kuwasiliana na Afisa Ugani ngazi za kijiji, kata, wilaya na Wizarani.

Aliongeza kusema mfumo huu tangu uliopanza kufanya kazi mwanzoni mwa mwaka huu umewezesha kupunguza tatizo la upungufu wa maafisa ugani kwa kuwa wakulima wanaweza kupata huduma hizo pale wanapokuwa wamesajiliwa kwenye mfumo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mifumo ESRF John Kajiba alisema taasisi yake ilifanya utafiti kwenye mikoa ya Kagera na Mara kuhusu mahitaji ya wakulima kwenye huduma za ugani na kugundua kuwa wakulima wanahitaji taarifa za huduma za ugani na masoko kwa haraka kutaboresha tija kwenye Kilimo.

Kajiba aliongeza kusema kuwa kupitia utafiti huo ndipo wakaanzisha ushirikiano na Wizara ya Kilimo kuanzisha mfumo wa M-Kilimo unaotekelezwa kote nchini .

Mtaalam wa mifumo ya teknoljia toka kampuni ya MULTICS Bw. Emmanuel Kagongo (kulia) akiwa na Mkuu wa Mifumo ESRF Bw.John Kajiba (kushoto) leo wakati wa kikao cha Naibu Waziri Kilimo kuhusu mfumo wa M-Kilimo leo jijini Dodoma.


Wakulima wanaweza kujiunga na Mfumo wa M-Kilimo kupitia simu zao za mkononi ambapo wanaweza kubonyeza *152*00# na kuchagua neon Huduma za Serikali kisha kubofya namba 7 Kilimo.

Imeandaliwa na :

Kitengo cha Mawasiliano Serikalini

Wizara ya Kilimo

DODOMA

04  Julai, 2021

 

Post a Comment

0 Comments