ILI KUIMARISHA ULINZI NA USALAMA UCSAF YATANGAZA ZABUNI ZA KUFIKISHA MAWASILIANO MIPAKANI.

 


CELINA MWAKABWALE(UCSAF)

WAZIRI wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe, Dkt. Faustine Ndugulile amesema Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote(UCSAF) imetangaza zabuni mbili za miradi ya kufikisha huduma za mawasiliano katika maeneo ya mipakani na kanda maalum awamu wa sita. Zabuni ambayo ina kata 190 zenye vijiji 380 na imetengewa kiasi cha shilingi za kitanzania 26,830,000,000.

Zabuni ya pili ni ya mradi unaolenga kufikisha huduma za mawasiliano katika ofisi za Halmashauri na kanda maalum na umetengewa ruzuku ya fedha za kitanzania 10,880,000,000 ukiwa na kata 34 zenye vijiji 45.

Waziri Ndugulile amesema hayo katika hafla ya uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Wizara wa miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2021/22 hadi 2025/26 uliofanyika mjini Dodoma na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Manaibu Waziri, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu Mhe. Moshi Kakoso, wakuu wa taasisi zilizo chini ya Wizara na mjumbe kutoka Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.



Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Dkt.Faustine Ndugulile (wa pili kushoto) akizundua Mpango Mkakati wa Wizara  wa miaka miano (2021/22-2025/26) jijini Dodoma. Wa pili kulia ni Naibu Waziri Mhe. Mhandisi Kundo Andrea Mathew, wa kwanza kulia ni mwakilishi wa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Mhe. Mlaghila Jumbe (Mb) na kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Zainab Chaula.



Mradi wa kufikisha huduma za mawasiliano mipakani unalenga kuhakikisha kuwa maeneo yote ya mipakani yanapata mawasiliano ya uhakika ili kulinda na kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi huku mradi wa kufikisha huduma za mawasiliano katika ofisi za Halmashauri na kanda maalumu unalenga kuboresha huduma za mawasiliano katika maeneo hayo.

Akizungumzia Mpango Mkakati wa wizara, Dkt. Ndugulile amesema umejikita katika nyaraka mbalimbali za kisera, malengo ya maendeleo ya kitaifa na kimataifa pamoja na Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2021-2025 katika vipengele vinavyogusa mawasiliano na teknolojia ya habari.

Awali akifanya wasilisho kwenye banda la UCSAF mbele ya Waziri Ndugulile na viongozi wengine wa Serikali waliombatana nae, Mtendaji Mkuu wa UCSAF Justina Mashiba amesema katika kipindi cha siku 200 tangu kuundwa kwa Wizara hiyo, Mfuko umefanikiwa kukamilisha miradi ya mawasiliano ya simu katika kata 84 zenye vijiji 305 na wakazi zaidi ya laki saba wamenufaika na mradi huo.

Aidha ameongeza kuwa, Mfuko umekamilisha mradi wa kuboresha usikivu wa radio katika eneo la Mradi wa kimkakati wa Bwawa la Umeme pamoja na maeneo ya Kisaki, na kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Zanzibar, Mfuko umefanikiwa kuanzisha kituo cha Mawasiliano ya dharura (Emergency call centre) kwa lengo la kuratibu taarifa za matukio ya dharura yanayohitaji uratibu wa pamoja kama kutoa taarifa za matukio ya moto, mafuriko na maambukizi ya magonjwa kama vile ugonjwa wa COVID-19.

Post a Comment

0 Comments