MTAKA AISIMAMISHA KAMPUNI YA UPIMAJI ARDHI

 


📌DOTTO KWILASA

MKUU wa  Mkoa wa Dodoma,Anthony Mtaka ameisimamisha Kampuni ya upimaji Ardhi ya GEOPLAN  Ltd kufanya shughuli zake na badala yake kazi yake itafanywa na timu ya wataalamu wa Ardhi kutoka Jiji.

Hatua hii imekuja kufuatia   baadhi ya wananchi wa Michese Kata ya Mkonze Jijini Dodoma kuilalamikia kampuni hiyo ya upimaji ardhi kutoa  Lugha za kuudhi pindi wananchi wanapohitaji maelezo kutoka kwao  Pamoja na  kuwadhulumu maeneo yao na kuyauza kinyume na taratibu.

Mtaka ametoa uamuzi huo Jijini hapa mara baada ya kusikiliza kero za wananchi wa eneo hilo kuhusiana na suala la upimaji wa Ardhi  huku akiagiza kazi ya upimaji kufanywa na Wataalam  wa Jiji la Dodoma pamoja na Wizara ya Ardhi,Nyumba na maendeleo ya makazi.

Aidha amewataka wananchi hao kuwa watulivu na kuendelea  kuheshimu maeneo yaliyopimwa bila kutofanya chochote hadi hapo uongozi wa Jiji na Wizara ya Ardhi watakapoenda kusuluhisha migogoro hiyo.

Mbali na hayo Mkuu huyo wa Mkoa wa Dodoma ametumia nafasi hiyo pia kuwaelekeza Wafanyakazi na wataalamu wa Ardhi Jijini hapa kuwa na Lugha nzuri wanaowahudumia wananchi.

Amesema baadhi ya wataalamu wa Ardhi wa jiji wamekuwa na kauli chafu na zinazoudhi kwa wananchi hali inayosababisha suala la migogoro ya ardhi kuendelea kuwa sugu.

"Nawaombeni sana acheni kutoa lugha mbaya kwa wananchi wanapohitaji huduma,jaribuni kuwaelekeza kwa kuwaheshimu na hii itasaidia kumaliza migogoro mapema,"amesema na kuongeza;

"Jaribuni sana kuwa na heshima kwa kila mtu,kabla hujaanza kumhudumia mwananchi mchukulie Kama baba au mama yako aliyeko huko kijijini kwenu,"amesisitiza Mtaka.

Awali wakielezea kero zao baadhi ya wakazi hao wa michese wamesema kuwa wanashangazwa na kitendo cha Kampuni hiyo ambayo imekuwa ikipima maeneo hayo na  kujimilikisha  kinyume  na taratibu.

“Mkuu wa mkoa bora umekuja najua utatusaidia kwasabu tumenyanyasika kwa muda mrefu na hii kampuni, sisi hatuitaki kwasababu imekuwa haitutendei haki licha ya kutupimia maeneo lakini imekuwa ikijimilikisha maeneo mengine”,walisema.

Wamesema kuwa licha ya wao kuwa na kamati ya usimamizi wa Kampuni hiyo katika eneo la Michese hakuna kinachofanyika zaidi ya kuchukuliwa maeneo yao jambo ambalo wamesema sio haki.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini,Jabir Shekimweri amesema kuwa asili ya mgogoro wa eneo hilo  ni kutokona na upimaji na urasimishaji wa eneo na hivyo kupelekea  malalamiko hayo na kuamua kuja na uongozi wa Mkoa ili kusikiliza kero za wakazi wa Michese.

Kutokana na kuwepo kwa migogoro ya Ardhi katika Jiji hilo tayari Wananchi wengi wamefikiwa na zoezi la usikilizaji wa kero tangu Julai5 hadi julai16 kwa Kamati inayosikiliza migogoro hiyo  ambapo tayari imepokea jumla ya migogoro2382kati ya hiyo zaidi ya migogoro500 imetatuliwa huku zikiongezwa siku10 kwaajili ya utatuzi wa migogo ya Ardhi Jijini Dodoma.

 

MWISHO

Post a Comment

0 Comments