VYUO CHINI YA WIZARA YA FEDHA VYAAGIZWA KUONGEZA TAFITI

 

 


📌PETER HAULE, WFM.

NAIBU Waziri wa Fedha na Mipango, Mhandisi Hamadi Yussuf Masauni, amekiagiza Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) na Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA) kufanya tafiti zitakazo ibua vyanzo vipya vya mapato na kodi ili kuisaidia Serikali katika kutekeleza mipango ya maendeleo kwa watanzania.

Agizo hilo limetolewa jijini Dar es Salaam alipotembelea Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) na Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA) ambapo alikutana na kufanya mazungumzo na Menejimenti ya vyuo hivyo katika mwendelezo wa ziara yake ya kutembelea taasisi zote zilizo chini ya wizara hiyo.

Mhandisi Masauni alisema kuwa Vyuo hivyo vimekuwa vikifanya vizuri katika mambo ya taaluma kwa kuongeza Kozi mbalimbali, idadi ya wanafunzi licha ya changamoto ya miundombinu na ufaulu lakini suala la utafiti linatakiwa pia kupewa msukumo wa ziada.

Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka 2021/22 imepokelewa vizuri na wabunge na wananchi kwa ujumla hususani katika mabadiliko ya kodi na vyanzo vya mapato, lakini jambo hili linaweza kuwa endelevu kwa kufanya tafiti zaidi ili kuweza kuwa na kodi na vyanzo vipya vya mapato ambavyo si kero kwa mwananchi.

Mhandisi Masauni.

Mhandisi Masauni amevitaka Vyuo hivyo kuendelea kufanya tafiti pia katika eneo la ununuzi na ugavi na kutoa ushauri kwa Serikali ili kuongeza nguvu katika usimamizi wa fedha za miradi kwa kuwa fedha nyingi hutengwa kwa ajili ya maeneo hayo.

Amezihakikishia Menejimeti za Vyuo hivyo kuwa Wizara ya Fedha na Mipango itashirikiana navyo kufanikisha tafiti zitakazoongeza tija kwenye uchumi na maendeleo ya    nchi.

Mhandisi Masauni alisema kuwa Vyuo hivyo vinawataalamu wabobezi katika masuala ya usimamaizi wa fedha na bima, masuala ya ugavi na ununuzi hivyo wanaweza kuwa washauri wazuri katika nyanja hizo kwa Wizara ya Fedha na Mipango iliyopewa dhamana ya kusimamia uchumi wa nchi na Serikali kwa ujumla ili kuweza kupiga hatua za maendeleo.



Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Hamad Yussuf Masauni (Mb), akizungumza na baadhi ya wanafunzi wa Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA), alipofanya ziara ya kutembelea Chuo hicho, jijini Dar es Salaam.

Alisema kuwa suala la ushauri elekezi unaotokana na tafiti una tija si tu kwa mapato ya Serikali lakini pia kwa vyuo, hivyo ni vema Vyuo hivyo vikaongeza jitihada za kuongeza tafiti na ushauri kwa Serikali kwa kuwa kuna uhitaji mkubwa.

Aidha amevitaka Vyuo hivyo kutoa mafunzo ya muda mfupi hususani kwa watumishi wa umma wanaofanya kazi kwenye taasisi zinazofanana na fani zilizopo katika Vyuo hivyo ili kuwaongezea uwezo lakini pia kukuza kipato cha chuo.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA), Dkt. Momole Kasambala, alisema kuwa, katika mwaka wa fedha 2019/20 hadi sasa taasisi imefanikiwa kuboresha miundombinu ya utafiti, ushauri wa kitaalamu na machapisho.

Dkt. Momole alisema kuwa TIA imefanikiwa kutoa ushauri wa kitaalamu kuhusu mbinu za ukusanyaji mapato na kubuni vyanzo vipya vya mapato kwa Halmashauri tano hadi kufikia, Juni 2021.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Prof. Tadeo Satta, amesema kuwa idadi ya tafiti imeongezeka na sasa wameingia katika hatua ya uandishi wa vitabu na pia suala la mafunzo kwa watumishi wa umma litafanyiwa kazi ili kuongeza tija katika utendaji kazi kwa waTumishi wa umma.



Baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA) wakimsikiliza  Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Hamad Yussuf Masauni

Wakuu wa Vyuo hivyo wamemshukuru Naibu Waziri Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, kwa kutembelea taasisi zilizo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango ili kuona majukumu yanatekelezwa kwa ufanisi.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhandisi Masauni, anaendelea na ziara ya kutembelea taasisi zilizo chini ya wizara hiyo, jijini Dar es Salaam.

 

Post a Comment

0 Comments