WAZIRI MKUU ATIA 'CHACHU' UZALISHAJI ZABIBU,BENKI YA KILIMO YAFUNGUA MILANGO



 ðŸ“ŒMWANDISHI WETU

KATIKA kuendeleza juhudi za kukuza uzalishaji wa zao la zabibu nchini Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameziagiza taasisi za majeshi nchini, ikiwemo Jeshi la Kujenda Taifa (JKT) na Jeshi la Magereza kuanza kulima zao hilo kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa wakulima wengine.

Ameyasema hayo leo  wakati akizungumza na wadau wa uendelezaji wa zao la zabibu kwenye ukumbi wa Hazina jijini Dodoma,Majaliwa amesema serikali imeamua kuinua uzalishaji wa zao hilo ambalo Tanzania inashika nafasi ya pili kwa barani Afrika ikiongozwa na South Afrika.

Lazima tuongeze uzalishaji wa zabibu ili siku moja tuwe wa kwanza katika uzalishaji wa zabibu Afrika.

Waziri Mkuu amesema kwa vile jeshi la Magereza wana maeneo makubwa ya kilimo kuingia kwao kujihusisha na zabibu kutakuwa ni chachu kwa wakulima wengine na kutumia mashamba hayo kama mfano kwao.

Pia amesema utafiti wa udongo uliofanyika katika maeneo ya Bunda,Tabora,Lushoto na Iringa inaonesha kuwa zabibu inaweza kustawi vizuri katika maeneo hayo,hivyo ni vyema wananchi wa maeneo hayo kuanza kuhamasishwa kulima zabibu.



Pia, Waziri Mkuu amevitaka vyama vya ushirika wa kilimo cha zao la zabibu navyo vianzishe vitalu vya miche na kuwawezesha wanachama wake kupata mbegu bora kwa urahisi. Amesema Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) kupitia kituo chake cha Makutupora iimarishe utafiti wa zao hilo ili kupata miche bora na yenye tija na kuifikisha kwa wakulima.

Kuhusu uwezeshwaji wa wakulima,Waziri Mkuu amezitaka benki za biashara kupunguza urasimu katika kutoa mikopo huku akizitaka kuanzisha dawati maalumu la kusaidia wakulima katika kuandika maandiko ya miradi.

 Moja ya kilio kikubwa cha wakulima ni mtaji,tulianzisha benki ya Kilimo na ina pesa.Lakini changamoto kubwa ni Write-UP,miezi sita mkulima anauliziwa write-up tu.Wekeni mazingira rahisi wakulima wapate mitaji.

Waziri Mkuu,Kassim Majaliwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Kilimo Tanzania (TADB) Japhet Justin amesema benki hiyo ipo tayari kuinua uzalishaji wa zao la zabibu na bidhaa zake katika mkoa wa Dodoma.

Akizungumza mbele ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa,Mkurugenzi wa TADB amesema benki hiyo inaendelea kutoa mikopo yenye masharti nafuu ili kumsaidia mkulima kuongeza tija katika kilimo cha zabibu na usindikaji wa mchuzi wake.

Tunatoa mikopo kwenye mnyororo mzima wa thamani wa zao la zabibu,tunaanzia hatua za awali kabisa.Unaweza kuwa hutaki kuwa mkulima lakini tunaweza kukukopesha ukanunua trekta na kazi yako ikawa ni kuwalimia wakulima tu

Japhet Justin,TADB.


Hata hivyo,Bw.Justine amebainisha kwamba mikopo ya TADB haitolewi kwa kigezo cha dhamana,bali wakulima na wazalishaji wenye maandiko mazuri ndiyo wanapewa vipaumbele ili wapate mitaji ya kuendeleza shughuli zao za uzalishaji.

Naye, Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe amesema kwa sasa Wizara ya Kilimo kupitia mfumo wa simu wa M-kilimo imeanza usajili wa wakulima wa zabibu ili waweze kuwatambua na kuwafikia kwa urahisi.

Amesema mbali na usajili wa wakulima, pia wizara ya Kilimo imepanga kuanzisha maonesha maalumu ya Zabibu (Grapes Trade Fair) ,katika maonesho hayo wakulima na wadau wote wa zabibu wataonesha bidhaa zao ikiwemo zana za kilimo,mvinyo pamoja na aina mbalimbali za zabibu zinazopatokana katika mkoa wa Dodoma.

Naye, Mbunge wa Dodoma Mjini, Anthon Mavunde ameiomba Serikali iwasaidie wakulima katika kuboresha zao hilo kwa kuanza kuuza mchuzi wa zabibu badala ya kuuza matunda.

Mheshimiwa Waziri Mkuu,tunaomba SIDO itengeneze mashine rahisi zitakazowawezesha wakulima na wafanyabiashara wa Dodoma waache kuuza zabibu kama matunda hazina faida,watapata faida kubwa kama wakiuza mchuzi wa zabibu.

Anthony Mavunde,MB.

Nao Wadau wa zao hilo wameiomba Serikali iwasaidie katika upatikanaji wa pembejeo, mikopo pamoja elimu ya namna bora ya kulima zao hilo ili waweze kuongeza tija katika uzalishaji wao,na pia uboreshwaji wa mazingira ya biashara ya mvinyo. 

Post a Comment

0 Comments