TRILIONI 3.6 KUONGEZA MTANDAO WA BARABARA



📌 MWANDISHI WETU

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI), Ummy Mwalimu, amezindua Mpango Mkakati wa pili wa miaka mitano wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini(TARURA) wenye thamani ya Sh.Trilioni 3.6.

Uzinduzi huo umefanyika leo Agosti 12,2021 jijini Dodoma Waziri Ummy amesema kuwa Mpango huo unaanza mwaka huu 2021/22 hadi 2025/26.

Mhe.Ummy ameeleza kuwa mpango huo utaongeza mtandao wa barabara kutoka kilometa 2,404.90 hadi 3,855.65, changarawe kutoka kilometa 29,116.57 hadi 102,358.14 na madaraja kutoka 2,812 hadi 6,620 na fedha zitakazotumika ni Sh.Trilioni 3.6.

Mpango huu kwa miaka mitano unahitaji Sh.Trilioni 3.6 sidhani kabisa Rais Samia kama atashindwa kwa kuwa anauwezo wa kuzitafuta ndani ya miaka mitatu, twendeni tukaoneshe kazi yenye ubora na ufanisi

Waziri Ummy  amesema serikali  itaupatia Wakala huo magari 122 na mchakato wa kuomba ajira za Wahandisi unaendelea na wataajiri Maofisa manunuzi kwa ajili na kutoa ajira za muda.

Aidha Ummy, amesema kuwa kwenye miji hiyo zitajengwa kilometa tano za barabara ya lami huku akisema kuna andiko litaandaliwa kwa ajili ya miji ambayo haitapata.



Hata hivyo Ummy ametoa angalizo kwa Wakala huo kuhakikisha kazi za ujenzi wa barabara zifanyike kwa ufanisi kwa kuwa ni kipimo chao kwa watanzania.

“Tunataka tuone tija katika suala zima la ukarabati wa barabara mijini na vijijini, ndugu zangu mnakazi kubwa mwaka huu mmoja ndio mwaka wa kuwapima je, kile kisingizio cha kuwa hamna fedha kilikuwa kisingizio au hamna uwezo na ubunifu na utashi wa kazi mnazotakiwa kuzifanya,”amesema.

Amesema matarajio ya serikali kwa Tarura ni makubwa sana hivyo wasiiangushe na waoneshe kuwa ni taasisi sahihi ya kufungua barabara za mijini na vijijini.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ofisi hiyo, David Silinde, amesema TARURA katika historia ya nchi kwa mara ya kwanza imetengewa fedha nyingi.

“Nipongeze Bunge kupitia kwa Spika wetu Job Ndugai kwa kupitisha kiwango cha fedha, ambacho Tarura itaweza kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, malengo na mikakati tuliyojadili hapa itatekelezwa kama ilivyokusudiwa,”amesema.

Naye Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Prof.Riziki Shemdoe, amesema mkutano huo wa siku wa tatu mbali na kuzindua kauli mbiu, watapitia utekelezaji wa Mkakati wa kwanza wa miaka minne na kupitia Mkakati wa Pili wa mwaka 2021/22 hadi mwaka 2024/25.



Awali Mtendaji Mkuu wa TARURA, Mhandisi Victor Seff ,amesema katika utekelezaji wa Mpango Mkakati kuanzia mwaka 2017 hadi Juni mwaka 2021, jumla ya Sh. trilioni 1.3 zimetumika kutengeneza kilomita 24,979.24, ambapo kilomita 955.35 zimetengwa kwa kiwango cha lami, kilomita 16,857.82 za kiwango cha changarawe.

Post a Comment

0 Comments