SERIKALI YAENDELEA NA JUHUDI ZA KUPATA CHANJO ZAIDI


TAARIFA YA WIKI YA MSEMAJI MKUU WA SERIKALI, GERSON MSIGWA

📌 MWANDISHI WETU

# Baada ya EWURA kupandisha bei za mafuta kwa mujibu wa kanuni za ukokotoaji wa bei hizo, Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa alielekeza kusitishwa kwa bei mpya na kamati iliyoundwa inaendelea kupitia kanuni ili kutoa bei zitakazoleta nafuu kwa wananchi.           

#Tunasisitiza kuwa chanjo ya Uviko-19 ni ya hiari, wataalamu wetu wanatusisitiza kuwa chanjo ni salama, mpaka sasa zaidi ya Watanzania 325,000 (31.5%) wamepokea chanjo, Serikali inawasihi wananchi ambao wapo katika makundi hatarishi kujitokeza kupokea chanjo hizi.

Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kufanya juhudi za kupata chanjo zaidi kwa ajili ya Watanzania na yapo matumaini makubwa ya kupata chanjo baada ya shehena ya dozi 1,058,400 iliyoletwa Julai 24, 2021 kutoka Marekani kuisha.

#Serikali imetoa muda wa kati ya tarehe 01 – 07 Septemba,  2021 kwa kampuni za simu kuweka sawa mitambo yao ili punguzo la asilimia 30 na asilimia 10 katika tozo za miamala ya simu lianze.

#Napenda kusisitiza kuwa tozo hizi zinakusanywa kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania, zimewekwa ili kuharakisha utatuzi wa changamoto za wananchi kwa sababu tukiendelea kwa kasi iliyokuwepo tungeweza kutumia muda mrefu zaidi.

#Utoaji wa vitambulisho vya Taifa unaendelea vizuri. NIDA imeshazalisha vitambulisho Milioni 9.4, kati yake vitambulisho Milioni 8.5 vimehakikiwa na kupelekwa kwa wahusika katika vituo mbalimbali.

#Serikali inatoa wito kwa wote ambao wameandikishwa kwa ajili ya kupata vitambulisho vya Taifa kwenda kwenye vituo vya wasajili walikoandikishwa ili wakachukue vitambulisho vyao na kwa wale ambao wameomba kubadilishiwa taarifa kuwa na subira wakati uhakiki unafanyika.

#NIDA inaendelea kutafuta namna rahisi ya kuhakikisha wananchi walioko maeneo ya pembezoni wanapelekewa vitambulisho vyao.

#Napenda kuwahakikishia kuwa kwa sasa nchi ina sukari ya kutosha. Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuhakikisha upatikanaji wa sukari unakuwa wa uhakika na bei nafuu  wakati juhudi kubwa zikielekezwa katika kuongeza uzalishaji katika viwanda vyetu vya ndani pamoja na kuhamasisha kuanzishwa kwa mashamba na viwanda vipya.

#Katika kipindi cha miaka 3 ijayo viwanda vyetu vya Kagera, Mtibwa na Kilombero vinatarajia kuongeza uzalishaji wa tani 265,000. Hizi zitaongezeka kwenye tani 367,000 zinazozalishwa sasa.

#Na pia tunao wawekezaji wapya, “Bagamoyo Sugar” ambao kwa sasa wameshalima shamba na kufunga mitambo kule Bagamoyo mkoani Pwani na wanatarajia kuzalisha sukari kuanzia mwezi Juni 2022 wakianza na tani 20,000 na baadaye kwenda zaidi ya tani 50,000 katika miaka mitatu ijayo.

#Katika mradi wa uwekezaji wa ubia kati ya NSSF na Magereza tayari shamba limeshalimwa na uzalishaji unatarajiwa kuanza kati ya Julai na Agosti mwakani 2022 kwa kuzalisha tani 50,000.

Katika kipindi cha miaka 3 ijayo tunatarajia kuwa na uzalishaji mpya wa sukari wa jumla ya tani 305,000 ambazo zitaungana na tani za sasa 367,000. Kwa hiyo katika miaka 3 ijayo tunatarajia uzalishaji wa jumla ya tani 672,000.

#Kigoma ni kati ya maeneo yaliyofikiwa na umeme wa Gridi ya Taifa, tuna jumla ya MegaWati 1,604 ambazo ni zaidi ya mahitaji ya nchi ya MegaWati 1,400 hivyo kukatika umeme mkoani humo ni kutokana na marekebisho ya miundombinu yanayofanywa na TANESCO.

 

IMEANDALIWA NA IDARA YA HABARI - MAELEZO

Post a Comment

0 Comments