TANROADS YATAKIWA KUTOA ELIMU

 


📌MWANDISHI WETU

WAZIRI wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Dkt. Leonard Chamuriho, amewataka watendaji wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), kutoa elimu ya kutosha kwa wasafirishaji kuhusu matumizi sahihi ya magari yanayostahili kupita katika barabara na madaraja nchini.

Dkt. Chamuriho amesema hayo jijini Dodoma, wakati akifungua kikao kazi cha menejimenti na mameneja wa Wakala huo ambacho kinalenga kutatua changamoto mbalimbali za wakala huo na kupanga mikakati ya kiutendaji

“Nimefanya tathimini ya haraka haraka nikagundua kuwa bado kuna magari ambayo ni mazito sana ambayo yanastahili kuwa site tu na si kutembea barabarani kama inavyoonekana sasa, jambo hili si sahihi watendaji naomba mlisimamie kwa karibu mkilifumbia macho litaendelea kuharibu miundombinu yetu”, amefafanua Dkt. Chamuriho

Aidha, Dkt. Chamuriho ameuagiza wakala huo kuongeza usimamizi mzuri wa mizani pamoja na watumishi wa mizani kujengewa uwezo kwa kupewa mafunzo ili waweze kutoa huduma bora kwa wateja na kupunguza malalamiko ya wasafirishaj

Waziri Dkt. Chamuriho ameusisitiza uongozi wa TANROADS kuongeza juhudi katika kusimamia wakandarasi wa ndani ili waweze kujengewa uwezo wa kufanya kazi kwa weledi zaidi kwa sababu wengi wao bado wanahitaji usimamizi wa karibu ili waweze kufanya vizuri, pamoja na kuboresha kitengo cha Wahandishi Washauri kutoka katika wakala huo (TECU).

Naye Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Rogatius Mativila, amesema kuwa mizani zote nchini zimefungwa CCTV kamera kwa lengo la kufuatilia kwa karibu utendaji wa mizani hizo ili kuhakikisha kuwa huduma zinatolewa kama inavyostahili.

“TANROADS tumeshafunga kamera katika mizani zote na ni matumaini yetu kuwa barabara zitalindwa na zitadumu kwa muda mrefu”, amesema Mhandisi. Mativila.

 

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Post a Comment

0 Comments