RC RUKWA ATAKA VIONGOZI WA TARAFA NA VIJIJI WAELIMISHWE UHAMASISHAJI CHANJO YA UVIKO-19


 Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Joseph Mkirikiti akifungua kikao cha Kamati ya Afya ya Msingi ngazi ya mkoa leo mjini Sumbawanga ambapo ameagiza viongozi wa tarafa, kata na vijiji kutumika kutoa elimu na ushawishi ili wananchi wajitokeze kupata chanjo ya UVIKO -19 aina ya Sinopharm.


Mwenyekiti wa Kamati ya Afya ya Msingi na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti (aliyekaa katikati) akiwa na wajumbe wa Kamati ya Usalama Mkoam leo mjini Sumbawanga mara baadha ya kikao cha tathimini ya zoezi la chanjo ya UVIKO-19 awamu ya kwanza na maandalizi ya chanjo awamu ya pili.


Mkuu wa Wilaya ya Nkasi Peter Lijuakali akizungumza kwenye kikao cha tathmini ya Mpango Harakishi na Jumuishi ya Utoaji chanjo ya UVIKO-19 leo mjini Sumbawanga.


Mwenyekiti wa kamati ya amani mkoa wa Rukwa na Askofu wa KKKT Dayosisi ya Ziwa Tanganyika Ambele Mwaipopo ameshauri watalaam wa afya kuwtembelea wananchi kwenye maeneo yao ikiwemo makanisa na misikiti ili watoe hamasa na elimuya uchanjaji chanjo ya UVIKO-19 .


Kiongozi wa Machifu wa Rukwa Mwene Charles Chilindo Katata wa Himaya ya Nkasi akizungumza kenye kikao cha tathmini ya utoaji chanjo ya UVIKO -19 leo mjini Sumbawanga ambapo amekanusha taarifa kuwa chanjo ya korona inasababisha upungufu wa nguvu za kiume.

Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Bw. Alli Lubeba akitoa taarifa ya mapokezi ya chanjo za UVIKO -19 aina ya Sinopharm ambapo amesema jumala ya dozi 42,183 zimepokelewa na tayari zimesambazwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya katika halmashauri nne za Rukwa.

Sehemu ya wadau na wajumbe walioshiriki  kikao cha Tathmini ya Mpango Harakishi na Jumuishi ya Chanjo ya UVIKO-19 kwa mkoa wa Rukwa leo mjini Sumbawanga.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti ameagiza viongozi wa Tarafa, Kata na Vijiji kuelimishwa na kuhamasishwa ili washiriki kikamilifu kwenye utoaji hamasa ya wananchi kujitokeza kuchanja chanjo ya UVIKO-19 aina ya Sinopharm iliyoanza kutolewa kote mkoani.
Ametoa agizo hilo leo (25.10.2021) mjini Sumbawanga wakati akifungua kikao cha Kamati ya Afya ya Msingi ngazi ya mkoa kilichokutana kufanya tathmini ya Mpango Harakishi na Jumuishi ya chanjo ya UVIKO-19 awamu ya kwanza.
Mkirikiti alibainisha kuwa changamoto zilizojitokeza kwenye uhamasishaji wa zoezi la chanjo ya UVIKO-19 imeonesha kuwa viongozi wengi ngazi ya chini hawakushiriki kikamilifu kwenye utoaji elimu na hamasa hatua iliyopelekea kuchelewa kukamilika kwa kazi ya uchanjaji kwenye vijiji na mitaa.
“Tuimairishe na kushirikisha watendaji ngazi ya tarafa, kata, vijiji, mitaa na vitongoji ili waweze kutoa elimu na ushawishi kwenye jamii ili watu wengi sasa wapate kuchanja chanjo ya korona aina ya Sinopharm, hatua itakayosaidia kuongeza kinga dhidi ya ugonjwa huo” alisisitiza Mkirikiti.
Akiwasilisha taarifa ya tathmini ya uchanjaji Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Alli Lubeba alisema jumla ya wananchi 17,757 walichanja chanjo aina ya J &J ya kinga dhidi ya UVIKO-19 kwenye mkoa wa Rukwa ambapo wanaume waliokuwa 9,575 na wanawake 7,182.
Lubeba alisema pia katika awamu ya pili mkoa wa Rukwa umepokea chanjo ya UVIKO-19 aina ya Sinopharm dozi 24,183 ambapo tayari zimepelekwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya katika halmashauri zote nne.
Ametaja mgao wa chanjo kwa awamu ya pili kwenye kila halmashauri kuwa Kalambo (dozi 3,600), Sumbawanga Manispaa (dozi 4,800), Nkasi (dozi 4,800) na Sumbawanga vijijini (dozi 4,800) aina ya Sinopharm ambapo dozi 6,000 zimesalia kama akiba kwenye famasi kuu ya mkoa.
“Chanjo hii ya aina ya Sinopharm tutaitoa kwa mtu kuchanja dozi mbili ambapo dozi ya pili hutolewa baada ya wiki tatu tangu dozi ya kwanza.Hii ni tofauti na ilivyokuwa dozi za J&J ambapo mtu alipata dozi moja pekee” alisema Lubeba. 
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Amani ya Mkoa ambaye pia ni Askofu wa KKKT Dayosisi ya Ziwa Tanganyika Ambele Mwaipopo, alisema ili mafanikio zaidi yapatikane kwenye awamu ya pili ya kuchanja ni budi wataalam wa afya kuyafikia makundi ya jamii kwa karibu ikiwemo makanisani, misikitini, kwenye misiba na matamasha kuwapa elimu ya umuhimu wa chanjo.
Naye Kiongozi wa Machifu Mkoa wa Rukwa Mwene Charles Chilindo Katata wa Himaya ya Nkasi Akizungumza kwenye kikao hicho aliwataka viongozi wa serikali kuwatumia viongozi wa kimila kutoa elimu ya umihimu wa chanjo ya uviko kwani jamii inawaheshimu na kuwasililiza.
Kuhusu uvumi kuwa chanjo ya korona inasababisha kupungua nguvu za kiume Mwene Katata alisema yeye amechanja tayari na hakuna tatizo lolote la kiafya alilopata.
“Sisi wanaume tumechanja na sasa ni miezi mitatu hakuna nguvu iliyopunua.Mambo kwenye familia yapo sawa hivyo si kweli chanjo ya UVIKO -19 inasababisha nguvu za kiume kupungua.” alisisitiza Chifu Katata.
Mwisho.
Imeandaliwa na;
Afisa Habari Mkuu,
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Rukwa
SUMBAWANGA
25.10.2021

Post a Comment

0 Comments