KICHEKO!HAZINA SACOSS YASHUSHA RIBA ZA MIKOPO



📌SAIDINA MSANGI, WFM

WAZIRI wa Fedha na Mipango Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba amekipongeza Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo cha Hazina, (Hazina Sacoss) kwa kutekeleza agizo la Serikali la kushusha riba za mikopo kwa wanachama wake kutoka asilimia 12 hadi asilimia 11 kwa mwaka.

Hayo yalielezwa na Kamishna Msaidizi wa Idara ya uendelezaji wa Sekta ya Fedha Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Dionisia Mjema kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), wakati akifungua Mkutano Mkuu wa nane wa Mwaka wa Hazina Saccos Ltd uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage uliopo Wizara ya Fedha na Mipango, jijini Dodoma.

“Sacoss ni nyenzo muhimu ya kupambana na umasikini, kujenga uchumi wa kaya kwa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla hivyo ni muhimu kuwa na sacoss imara na endelevu ambayo inatatua changamoto za wanachama”, alisema Dkt. Nchemba.

Alisema ili kufikia azma hiyo viongozi wa Hazina Sacoss wanapaswa  kuimarisha mifumo ya kuweka akiba, kununua hisa na kuongeza huduma bora na zenye gharama nafuu zinazokidhi matakwa ya wanachama hasa kuwa na gharama nafuu za mikopo.



Naibu Kamishna Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Dionisia Mjema, akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo Hazina (Hazina Saccos) uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage, jijini Dodoma.


Dkt. Nchemba aliwataka viongozi wa Saccos hiyo  kuwa na mpango wa kuongeza wanachama wapya, kuongeza akiba za hisa zao, kuwa wabunifu na kufanyia kazi changamoto na maoni yanayotolewa na wanachama.

Aidha Dkt. Nchemba aliwaagiza viongozi wa hazina sacoss kufanya tathmini sahihi ya miradi yao ukiwemo mradi wa Njedengwa juu ya uwezekano wa kupata mwekezaji ili wanachama waweze kunufaika na miradi hiyo na kuokoa fedha ambayo inaonekana imekaa muda mrefu kwenye ardhi bila uzalishaji.

Waziri Nchemba aliwapongeza viongozi wa hazina sacoss kwa kuunga mkono Serikali kwa kuendeleza jiji la Dodoma kwa kuwapatia viwanja wanachama wake katika maeneo ya Ihumwa ngaloni, Iyumbu, Nzuguni na Ihumwa Ilolo sehemu ambazo zilikuwa mapori yasiyotumika. 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Hazina Sacoss Bw. Aliko Mwaiteleke alisema kuwa mtaji wa chama umekua na  kufikia kiasi cha Sh. bilioni 18 ambazo zinajumuisha akiba za wanachama na hisa na ameongeza kuwa kama Chama cha ushirika  wamejipanga kusimamia kikamilifu kuhakikisha watumishi wengi wanajiunga na ushirika huu ili waweze kunufaika.

‘’Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo Hazina kilianzishwa mwaka 1972 wakati huo kikiwa na wanachama mia moja (100), lakini mpaka sasa chama kinahudumia wanachama takribani 5,624’’ Alisema Bw. Mwaiteleke.

Aida, Bw. Mwaiteleke aliishukuru Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuimarisha usimamizi wa Taasisi za Fedha nchini kwa kuanzisha sheria Namba 10 ya mwaka 2018 ya huduma ndogo za Fedha pamoja na kanuni zake za mwaka 2019 kwa ajili ya ustawi wa sekta ya fedha nchini.



Mwenyekiti wa Bodi wa Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo Hazina Bw. Aliko Mwaiteleke (kulia) akiteta jambo na Katibu wa Bodi hiyo Bw. Festo Mwaipaja wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa chama hicho

Aliongeza kuwa Hazina Saccos imejipanga kuwa chama chenye mlengo wa kutoa huduma kulingana na mahitaji na changamoto zinazowakabili wanachama ili waweze kufikia malengo waliyojiwekea.

Chama chetu kinatarajia kuongeza kiwango cha kukopa hasa mikopo ya dharura kwa wanachama wetu kutoka shilingi milioni mbili (2,000,000/-) mpaka shilingi milioni tano (5,000,000/-)

Bw. Mwaitekele

Bw. Mwaiteleke alitoa rai kwa wanachama kuwa waadilifu katika urejeshaji wa mikopo wanayochukua ili kuweza kukuza mfuko wa chama na kuwezesha wanachama wengi zaidi kunufaika na huduma zinazotolewa na chama hicho.

Mkutano wa mwaka wa Chama cha Kuweka na Kukopa cha Hazina unafanyika kwa siku mbili Jijini Dodoma ambao unahudhuriwa na wajumbe kutoka Mikoa mbalimbali nchini wanaowakilisha wanachama zaidi ya 5,000 kutoka kwenye mafungu (votes) 282 Tanzania Bara.

(Picha na Kitengo cha Mawailiano Serikalini – WFM, Dodoma)

 

Post a Comment

0 Comments