WADAU WAOMBA ELIMU ZAIDI MAPAMBANO YA RUSHWA

 


📌RHODA SIMBA

WADAU wa mradi wa mapambano dhidi ya rushwa ujulikanao “Tuungane kutetea Haki   awamu ya pili unaotekelezwa na Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini[TAKUKURU]  kwa kushirikiana na shirika la Konrad  Adenauer Stiftung[KAS] kutoka nchini Ujerumani wameitaka taasisi hiyo kuongeza kasi ya kusambaza elimu ya rushwa katika ngazi za chini katika jamii.

Wadau hao ni pamoja na Viongozi wa  TAKUKURU  Mkoa,na Wilaya viongozi wa dini sambamba na waratibu vitengo vya taaluma za rushwa wamesema vitendo vya rushwa vinaweza kukoma ikiwa kila mwanajamii ataelewa madhara na kuchukia rushwa.

Kadhi wa Mkoa wa Dodoma Kisusu Mvumbo  ameshauri TAKUKURU katika kuendeelea na mapambano hayo dhidi ya rushwa watoa elimu watembelee nyumba za ibada na kuomba kutumia japo dakika 15 kuelimisha waumini kuhusu rushwa.

Mvumbo amesema pamoja na kutoa elimu hiyo kanisani na misikitini lakini pia watumie vyombo vya habari zikiwemo radio na televisheni kuielimisha jamii kujua haki zao ili kusiwepo na mianya ya utoaji wa rushwa.

Mwenyekiti kamati ya Maadili ya Chuo Kikuu  cha Dodoma (UDOM) Ombeni Msuya amesema TAKUKURU kupitia watoa elimu waendelee kusambaza elimu ya rushwa katika vyuo  kwa wanafunzi ili waelewe haki zao na kujua namna ya kutopokea au kutoa rushwa.

Tunaona kiukweli jitihada ambazo TAKUKURU wanazifanya lakini elimu hii isambazwe kwenye vyuo ili wanafunzi wetu waendelee kuelewa rushwa ni nini

 Dk.Msuya.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kikao hicho Dkt.Francis    Michael  ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora  amekiri umuhimu wa mapendekezo ya sheria ya rushwa ili kutoa adhabu zaidi kwa viongozi wala rushwa.

Sheria hiyo kwa sasa inaelekeza kutaifishwa kwa mali za viongozi ambao watakutwa na hatia ya kupata mali hizo kwa vitendo vya rushwa. 

Utaratibu huu wa kuwataifisha mali zao halafu wanaendelea na shughuli zao kiukweli haijakaa sawa na haitoi hofu kwani mtu anajua nikitaifishwa mali zangu ajira yangu inabaki kuwa pale pale TAKUKURU inabidi ikae itazame upya sheria hii

Naye Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU nchini  Neema Mwakalyelye amesema lengo la mradi wa tuungane ni kuwashirikisha wadau ngazi za vijiji na mitaa hadi Taifa namna ya mapambano dhidi ya rushwa huku meneja mradi wa KAS Tanzania Damas Nderumaki akisema matarajio ya sasa ni kufikia mikoa 24 .

“Tumejipanga kusambaza elimu hii mashuleni,misikitini,makanisani, watendaji wa mitaa kuwashirikisha katika vikao vya halmashauri na pia mtaala mashuleni tunaendelea  kujipanga elimu hii ianzie katika shule ya msingi ili watoto wawe na uelewa  kuhusu rushwa”amesema Neema

Kwa upande wao baadhi ya wadau wa mradi wa Tuungane akiwemo Naibu Kamishina Mkuu wa Skauti Tanzania Abdallah Sakasa,mbunge wa Mbagala,Abdallah Chaurembo pamoja  Afisa Uchunguzi  TAKUKURU Wilaya ya Sikonge Mkoani Tabora Ilandike Julius wamesema kikao hicho kimekuwa na mchango mkubwa katika mapambano dhidi ya rushwa .

Wamefafanua kwamba kupitia mapendekezo yaliyotolewa  katika kikao kazi hicho yakiwemo ya kutoa elimu katika jamii ikiwemo misikitini,makanisani, shuleni na mitaala kuangaliwa upya wanaamini ya kwamba endapo yatatekelezwa kwa ufanisi kwa kiasi kikubwa watakuwa wamejitahidi katika mapambano dhidi ya rushwa .

 


Post a Comment

0 Comments