WAZIRI BASHUNGWA ATOA MAAGIZO KWA WALIMU,TAMISEMI NA CWT WAKIGAWA TUZO



📌RHODA SIMBA

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Innocent Bashungwa ametoa maagizo kwa wakuu wote wa shule nchini  kuhakikisha kwamba wanasimamia sheria, miongozo, na  taratibu  katika sekta ya elimu, kusimamia miradi  yote inayotekelezwa  katika maeneo yao, pamoja na kutunza majengo  ili yatumike hata katika vizazi vijavyo.

Kadhalika Bashungwa amewataka wakuu hao  kuandaa motisha  kwa walimu na wanafunzi   ili kujenga ari ya ushindani ,   na kuwa  viungo kati ya jamii na viongozi wanao wazunguka  kwa kuishi kwa ushirikiano ambao utawasaidia  katika kutekeleza kwa ufasaha  miradi mbalimbali  ya serikali  katika jamii.

Waziri Bahungwa ametoa maagizo  hayo leo February  11 jijini hapa katika hafla ya  utoaji tuzo  za  walimu  za ubora  wa taaluma kwa matokeo  ya mtihani  wa kumaliza elimu ya msingi, kidato cha nne na kidato cha sita  kwa mwaka 2021 kwa mikoa 26 ya Tanzania bara.

Amesema  ili kufikia malengo ya serikali ni lazima kusimamia miradi yote kwa ufasaha  na iendane na  thamani ya fedha, na mali za shule zitunzwe kwa ufasaha ili ziweze kutumika na vizazi vijavyo.
 

Wapo baadhi yenu hawana mahusiano mazuri na jamii hivyo  kukwamisha utekeleaji wa baadhi ya shughuli za serikali mnapokuwa na mahusiano mazuri na viongozi katika jamii hii pia inarahisisha katika utekelezaji na hata utunzaji wa majengo ya serikali
Waziri Bashungwa.

Nae Kaimu rais wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) Mwalimu Dina  Mathamani amesema wao kama walimu wameona umuhimu wa kutoa tuzo na pongezi kwa walimu waliofanya vizuri na kuwafanikisha wanafunzi kufaulu vizuri.

“Ufaulu  unaendelea kupanda siku hadi siku  taaluma zinapanda na mazingira ya walimu yataendelea kuboreshwa na niahidi kwa niaba ya Chama cha walimu tutafanya kazi kwa weledi ili kuhakikisha ufaulu unaongezeka ili tupate wataalamu katika sekta mbalimbali”amesema Mwl.Mathamani.

Naye Makamu wa rais Chama cha Walimu Tanzania ambao ndiyo wadhamini wakuu wa tuzo hizo,Dinna Mathamani ametoa pongezi kwa walimu pamoja na wadau mbalimbali kwa juhudi zao zilizofanikisha kiwango cha ufaulu kinaendelea kupanda mwaka hadi mwaka.



Kwa upande wake katibu mkuu wa Chama Cha Walimu  Tanzanaia (CWT )Mwalimu  Deus Seif  amesema Chama kinatambua  jitihada  kubwa zinazofanywa na serikali katika kuboresha  maisha ya watanzania wakiwemo walimu.

“Miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo ujenzi wa reli ya kisasa, (SGR) lakini katika Sekta ya elimu  yapo mambo kadhaa ambayo serikali  imeyafanya ikiwemo ongezeko la miundo mbinu na samani ,upandishwaji wa madaraja na  urekebishwaji wa mishahara kwa walimu, pamoja na malimbikizo ya madeni  yasiyo ya mishahara”amesema Mwl Deus.

Hata hivyo amesema pamoja na jitihada za Serikali lakini bado walimu wanakabiliwa na changamoto mbalimbali   zikiwemo uhaba  wa nyumba za walimu, madai mbalimbali  ya walimu  bado yapo katika halmashauri  pamoja na ajira  kwa walimu.

Akizungumzia kuhusu tuzo hizo za Ubora katika Elimu,Katibu Mkuu Ofisi ya Rais,TAMISEMI,Prof.Rziki Shemdoe amesema TAMISEMI ilianzisha muongozo wa utoaji wa tuzo mwaka 2019  ambapo  mwaka huu tuzo zaidi ya 480 zimetolewa kwa wanafunzi,walimu na wasimamizi wa mitihani.

Kwa upande wake Katibu mtendaji Baraza la Mtihani la Taifa (NECTA) Dkt.Charles Msonde  amesema  jumla ya Wanafunzi 481 wamepatiwa tuzo mbalimbali  baada ya kuonekana kufanya vizuri katika mitihani yao ya shule za msingi,kidato cha nne na kidato cha sita  kwa mwaka 2021.

Tuzo hizo pia zimetunikiwa kwa  shule 10 bora kitaifa ,walimu,mikoa,halmashauri zilizofanya vizuri na zinazoendelea kuimarika kuongezeka  kwa kiwango cha ufaulu kadiri miaka  inavyokwenda.

Dkt.Msonde amesema kwa mwaka 2021 ufaulu katika kumaliza elimu ya msingi umefikia 82.97%, mtihani wa kumaliza kidato cha nne umefikia 87.30% na kidato cha sita 99.62%. 

 Kauli mbiu  ya Tuzo za mwaka huu inasema “Uboreshaji wa Ufundishaji na Ujifunzaji shuleni ni chachu ya kuongeza kiwango cha ufaulu wa Wanafunzi”

 


 

Post a Comment

0 Comments