📌RHODA SIMBA
MKUU wa Mkoa wa Dodoma Anthony Mtaka
ameitaka wakala wa Misitu Tanzania (TFS) pamoja na uongozi wa bonde la
maji la Wami Ruvu kuongeza jitihada za upandaji na utunzaji wa miti katika
chanzo cha maji Mzakwe mkoani Dodoma.
Mtaka amebainisha hayo jijini hapa mara baada
ya kutembelea katika eneo la upandaji wa miti katika chanzo hicho cha maji
ambacho ni chanzo muhimu cha maji mkoani Dodoma na kutoridhishwa na hali
ya upandaji wa miti katika eneo hilo lenye zaidi ekari elfu nne, ikiwa ni
sehemu ya ziara yake maalum kuhusu masuala ya utunzaji wa mazingira.
Aidha, Mkuu huyo wa mkoa amesema takwimu
zinazotolewa juu ya idadi ya miti iliyopandwa katika eneo hilo haziendani na
hali halisi na kuwataka viongozi wa bonde kuacha uzembe na kudanganya
viongozi wakuu wa nchi.
Kutokana na baadhi ya jamii inayozunguka
katika chanzo cha maji Mzakwe kuwa na tabia ya kuingiza mifugo pamoja na
kuchoma moto chanzo hicho, mkuu huyo wa mkoa ameagiza sheria zitekelezwe
ikiwemo faini ya kuanzia Tsh. Elfu hamsini (50,000/=) hadi Tsh laki tatu (300,000/=)
Katibu tawala mkoa wa Dodoma Dkt.Fatuma Mganga
amesema kuna umuhimu wa uratibu mzuri wa utunzaji wa miti katika chanzo
hicho, huku Mstahiki Meya jiji la Dodoma Prof.Davis Mwamfupe akizungumzia
umuhimu wa ushirikishwaji wa jamii ya eneo husika katika utunzaji wa
chanzo hicho ambapo mkazi wa Makutupora mtaa unaozunguka eneo la hifadhi ya
chanzo cha maji Mzakwe Mzee Shaban Nyambo akishauri aina ya miti ya asili
inayopaswa na kustahimili eneo hilo kuwa ni pamoja na migunga na mikambala.
Mhifadhi misitu na wakala wa Misitu Tanzania (TFS)
kanda ya kati Alexanda Mboya ameanisha changamoto zilizosababisha miti
iliyopandwa kutostawi katika eneo hilo kuwa ni pamoja na mbuga hivyo mahitaji
ya eneo hilo la chanzo cha maji Mzakwe ni miti ya asili huku Mkuu wa kikosi cha
Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Makutupora Resto Mbanga akisema kuna
uhitaji wa ushirikiano wa kulinda eneo hilo.
0 Comments