VIFO WAKATI WA KUJIFUNGUA ,WAKUNGA WATOA NENO

 

📌RHODA SIMBA

IMEBAINISHWA  kuwa wakina mama 30 wanakufa kila siku,na wengine elfu 11,000 wanakufa  kwa mwaka, sababu kubwa za vifo hivyo vikitajwa kuwa ni kutokwa na damu nyingi wakati wa kujifungua na baada ya kujifungua.

Kadhalika Utoaji mimba usio salama umetajwa kwa (asilimia 19), Kifafa cha mimba (asilimia 17), uzazi pingamizi (asilima 11) na uambukizo (asilimia 11), huku sababu nyingine zinazochangia ni pamoja na ukosefu wa damu, malaria na maambukizi ya Virus Vya UKIMWI.

Akizungumza jijini Dodoma katika kilele  cha siku ya wakunga duniani Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI Switbert Mkama amesema kuwa pamoja na kuwa na ongezeko la akina mama kuhudhuria kiliniki na kujifungulia katika vituo vya huduma lakini takwimu zimeonesha ongezeko la vifo vya wanawake wajawazito kutoka 454 hadi  kufikia vifo 556 kwa kila vizazi hai  laki 100,000.

"Nimeelezwa kuwa  jumla ya wanawake wajawazito 2,373,668  waliohudhuria kiliniki  1,636,273 ( asilimia 69) walipimwa wingi wa damu,  1858856 ( asilimia 71 ) walipata chanjo ya kuzuia pepopunda,  

Waliojifungulia katika vituo vya huduma  walikuwa  1778987, kati ya hao  walizalishwa na Wakunga  watalaam  walikuwa  1657170 ( (asilimia 93 ),"amesema. 

Kwa hizi takwimu chache zinadhihirisha kazi kubwa inayofanywa na wakunga  katika kutoa huduma  kwa wanawake wajawazito na watoto. 

"Kwa mfano asilimia ya wajawazito wanaohudhuria kliniki imeongezeka na kufikia asilimia 98,  idadi ya  wakina mama wanaojifungulia  katika vituo vya huduma kutoka  asilimia 47 hadi asilima 63,"amefafanua. 

Aidha alisema kuwa takwimu zinaonyesha kuwa vifo vya watoto chini ya miaka mitano vimepungua  kutoka 81 hadi  67 kwa kila vizazi hai 1000.

Amesema kuwa Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa na jitihada  za wakunga  kwani hata mafanikio yaliyopo katika kupunguza vifo vya watoto chini ya mwaka mmoja na  watoto chini ya miaka mitano inatokana na kazi nzuri wanazozifanya wakunga hapa nchini.

Pia amesema kuwa shahidi kutoka tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa  mkunga akielimishwa  na kufikia kiwango cha kimataifa   kulingana na Shirikisho la Vyama vya Wakunga  Duniani  anaweza kutoa huduma za kuokoa maisha  kwa mama na mtoto mchanga kwa asilimia 87.

Kwa upande wake rais wa Chama Cha Wakunga Tanzania Bi Feddy  Mwanga alisema kuwa wakunga 200 waliotoka sehemu mbalimbali nchini waliweza kuhudhuria katika Kongamano hilo.

Amesema Kongamano hilo lilikuwa na mafanikio makubwa kwani wakunga na wadau wa Afya ya mama na mtoto walijitoa katika kuleta abstracts na kutoa mada ambazo zilikuwa za kuelimisha na kutoa matokeo ya tafiti mbalimbali.

Pia amesema waliweza kubadilishana uzoefu au kupeana taarifa mpya na mabadiliko kadhaa yaliyotokea kwenye taaluma ya ukinga.

"Kama ulivyoona wakunga na wadau walionyesha shughuli mbalimbali za ukinga katika mabanda uliyotembelea kumekuwa pia na vipindi vya kujengeana uwezo kwa kufundisha Jinsi ya kuhudumia wakinamama na watoto wachanga,"amesema.

Napenda nitambue na kuwashukuru sana mashirika ya umoja wa mataifa yakiongozwa na UNFPA ambapo tumekuwa nao katika safari nzima ya maandalizi ya shughuli hii pamoja na mashirika mengine.

Siku ya Wakunga huadhimishwa duniani kote tarehe tano mwezi wa tano ya kila mwaka kwa kufanya shughuli mbalimbali zinazohusiana na Wakunga pamoja na kuwahamasisha Wadau mbalimbali na Jamii kwa ujumla kuhusu  umuhimu wa huduma bora kwa akina mama na watoto. 

Kauli Mbiu ya Mwaka huu  ni “Invest in Midwives: Save lives ” kwa maana ya “Wekeza kwa Mkunga: Okoa Maisha”.

 

Post a Comment

0 Comments