SIMBACHAWENE AWEKA WAZI VIPAUMBELE VYA BAJETI OFISI YA WAZIRI MKUU

 

📌RHODA SIMBA

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera,Bunge na Uratibu) George Simbachawene amesema vipaumbele vya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake kwa mwaka  wa fedha 2022/2023 ni sawa na ongezeko la asilimia 20.61 ukilinganisha na bajeti ya shilingi 80,179,385,000.00 iliyotengwa mwaka wa fedha 2021/2022. 

Akizungumza Jijini Dodoma Waziri Simbachawene amesema lengo la kufanya jambo hilo ni kuwawezesha wananchi kufuatilia utekelezaji wa shughuli na miradi ya maendeleo iliyopangwa kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2022/23 na hivyo kuwapa nafasi ya kuihoji Serikali pale ambapo wataona baadhi ya mambo hayajatekelezwa.

Ili kutekeleza majukumu yake, kwa mwaka wa fedha 2022/2023, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) na Taasisi zilizo chini yake iliidhinishiwa na Bunge jumla ya Shilingi 101,030,914,000. Kati ya fedha hizo, Sh. 15,740,061,000/= ni Mishahara, Sh. 47,857,087,000/= ni matumizi mengineyo, Sh. 17,563,000,000/= ni ruzuku kwa vyama vya siasa na Sh. 19,870,766,000 ni matumizi ya maendeleo

 Simbachawene

Aidha, amesema kuwa shughuli zitakazotekelezwa kwa mwaka wa fedha 2022/23 ni pamoja na kuratibu upatikanaji wa huduma za VVU na UKIMWI kwenye Mikoa ya kipaumbele ikiwemo; Iringa, Kagera, Katavi, Mbeya, Mwanza, Njombe, Pwani, Ruvuma, Shinyanga, Dodoma, Geita, Tabora na Songwe pamoja na kuweka kipaumbele katika kuzuia maambukizi ya VVU kwa vijana wa miaka 15 - 24. 

Mapambano dhidi ya UKIMWI kwa mwaka wa fedha 2022/23, Tume ya kudhibiti UKIMWI Tanzania iliidhinishiwa na Bunge Shilingi 14,981,224,000.00 ambapo shilingi 2,979,018,000.00 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Shilingi 12,002,206,000.00 kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo ukilinganisha na bajeti ya Shilingi 4,317,818,000.00 zilizotengwa mwaka 2021/22 kwa ajili ya kutekeleza shughuli za matumizi ya kawaida na maendeleo sawa na ongezeko la asilimia 71.2

Simbachawene 

Aidha amesema Ofisi itaendelea kutafuta Vyanzo vya Fedha kwa ajili ya Mfuko wa UKIMWI (ATF), Mfuko huo umelenga kuiwezesha nchi kuwa na rasilimali fedha za kutosha kwa ajili ya kudhibiti UKIMWI hata pale fedha za nje zitakapopungua au kutokuwepo kabisa.

Pia ameeleza kuwa ili kutekeleza shughuli hizo, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imeitengea Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kiasi cha Shilingi 21,973,414,000.00 ili iweze kutekeleza majukumu yake. Aidha, kiasi cha Shilingi 10,413,014,000.00 kimetengwa kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ili kutekeleza majukumu yake.

Amesema Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 Ibara ya 51(1), Waziri Mkuu ni msimamizi na mfuatiliaji wa shughuli zote zinazotekelezwa na Serikali na Ofisi ya Waziri Mkuu ina jukumu la kuratibu utekelezaji wa shughuli zote za Serikali. 

Wakati huo huo, amefafanua kuhusu Mapambano Dhidi ya Biashara na Matumizi ya Dawa za Kulevya Katika mwaka wa fedha 2022/23 ambapo amesema Mamlaka ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya Nchini imeidhinishiwa Shilingi 11,974,701,000.00 kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake ukilinganisha na kiasi cha Shilingi 8,529,797,000.00 kilichoidhinishwa mwaka wa fedha 2021/22 sawa na ongezeko la asilimia 28.8. 

 

 

 

Post a Comment

0 Comments