MIUNDOMBINU ILIYOPO KATIKA SHULE ZETU INAWASAIDIA WANAFUNZI WENYE MAHITAJI MAALUM?

 


📌RHODA SIMBA

LICHA ya  Serikali  kuendelea kuboresha na kuweka sera, pamoja na mikakati ya miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu, lakini bado kuna  changamoto ya miundombinu na hali hiyo huwafanya baadhi ya watoto wenye ulemavu  kushindwa kumudu mazingira ya shule.

 

Aidha kutokana na changamoto hiyo inawasukuma  baadhi ya wazazi wa watoto wenye ulemavu kushindwa kuwaandikisha   darasa la awali.

Sera ya Taifa ya Maendeleo na huduma kwa watu wenye ulemavu ya mwaka 2004 kipengele cha 1.2.5  kinasema  bado  mfumo wa elimu nchini  hautoi fursa na nafasi sawa kwa watoto wenye ulemavu wa aina mbalimbali.

Aidha mafunzo ya walimu na mitaala ya shule kadhalika haizingatii mahitaji maalumu ya watu wenye ulemavu, kwa mfano matumizi ya lugha ya alama na maandishi ya nukta nundu.

Kutokana na mazingira haya idadi ya watoto wenye ulemavu wanaoandikishwa darasa la kwanza ni chini ya asilimia moja na idadi ni ndogo zaidi katika shule za sekondari na vyuo.

 

HALI ZILIVYO KWENYE BAADHI YA SHULE.

Michael Mfanyakazi ni  mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya sekondari Viwandani iliyopo hapa mkoani Dodoma,ambae yeye ana ulemavu wa viungo. Anasema changamoto anayokabiliana nayo shuleni ni maliwato.

“Hali ya vyoo vyetu hapa shuleni siyo rafiki kwangu, napata  tabu sana wakati wa kwenda  maliwatoni, vyoo vichache na havijatuzingatia sisi wenye ulemavu, kuna wakati najitahidi kujibana mpaka muda wa kurudi nyumbani. Naamini Serikali yetu ni sikivu naiomba ituangalie katika hili wanapotuboreshea madarasa  sisi wanafaunzi wenye ulemavu wa viungo itujali na masuala ya vyoo,” anasema Mwanafunzi Michael

Wakati huo huo Trivol Ruge mwanafunzi wa kidato cha kwanza  Viwandani Sekondari  ambae ana uoni hafifu anasema changamoto ambayo anakutana nayo ni kutoona vizuri ubaoni.

“Nakuwa sioni vizuri ubaoni utakuta mwalimu anaandika, anafuta,  mimi nakuwa sijamaliza kuandika  kwa sababu natumia muda mwingi kuunganisha herufi ili niandike. Naiomba Serikali miundombinu hii iwe jumuishi kwetu sisi wanafunzi wote wenye mahitaji maalum wa aina tofauti,” anasema mwanafunzi Trivol.

Rafael Olaf ni mwanafunzi wa kidato cha pili mwenye ulemavu wa ngozi (albinism) kutoka shule ya  Umonga Sekondari pamoja na Seif Mazika mwanafunzi mwenye ulemavu wa mguu wa kidato cha nne  shule hiyo hiyo pia, wanaendelea kupaza sauti zao  kuiomba Serikali iendele na juhudi za ukarabati wa miundombinu ya vyoo  shuleni ili iwe rafiki kwao.

 

Shule ya Sekondari ya Patandi ni moja ya shule chache ambazo miundombinu yake imeboreshwa na kuwa rafiki kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu.

WALIMU WAZUNGUMZA

Gerad Kailembo  ni  Mkuu wa idara ya wanafunzi wenye mahitaji maalum katika shule ya Sekondari Dodoma, ambapo anasema shuleni hapo wana  wanafunzi wenye mahitaji maalum  71 wakiwa wamegawanyika katika vipengele mbalimbali ambapo kuna wenye ulemavu wa miguu, ulemavu wa mkono, wenye uoni hafifu  pamoja na wasiosikia (Viziwi).

Akizungumzia hali ya miundombinu  kwa wanafunzi wenye ulemavu wa viungo anasema  wanakutana na changamoto mbalimbali ikiwemo miundo mbinu ya  vyoo, ambapo anasema idadi ya vyoo vilivyopo na wanafunzi  havitoshi lakini pia havijazingatia  mazingira rafiki  ya wanafunzi wenye ulemavu ambapo anaiomba Serikali iongeze jitihada  katika suala la ujenzi wa vyoo na kupeleka vitendea kazi kwaajili ya walimu  wenye uoni hafifu.

“Wanafunzi walio wengi ni zaidi  ya wanafunzi 60 wenye uoni hafifu ubaoni, na wanakutana na changamoto za kutoona maandishi yakiwa ubaoni tatizo hili  limekuwa changamoto kwetu na tunalitatua  wakati wa mitihani tunachapa maandishi makubwa, na tunawaweka mbele ili waone vizuri, pia tunawanafunzi ambao hawasikii vizuri lakini  tumewaomba walimu waongee nao vizuri kwa kurudia rudia  na inatulazimu wanafunzi hawa kuwafundisha mmoja mmoja ofisini,” anasema Mwalimu Kailembo.

 

Nae mwalimu Ester Simchimba Mkuu wa shule ya Viwandani Sekondari anasema  ana wanafunzi wawili wenye ulemavu  hali ya miundombinu katika shule ya viwandani  inaridhisha kiasi si kama zamani na  kutokana na juhudi za Serikali  hasa katika kutambua wanafunzi wenye ulemavu madarasa yaliyojengwa hivi karibuni yamezingatia miundombinu ya wamafunzi wenye ulemavu.

“Zamani miundombinu ilikuwa si rafiki ilikuwa haimuwezeshi hata mwanafunzi ambae anatambaa kufika darasani  hapa shuleni tunao wanafunzi wawili   lakini tunaishukuru Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan katika haya madarasa ya UVIKO  yamezingatia  miundombinu kwa hali ya juu na kilichosalia hapa ni ukarabati yale madarasa ya zamani,

“Lakini wito wangu kwa  Serikali yetu inapoboresha miundombinu yetu ya madarasa pia ituangalie na katika suala la vyoo viboreshwe kwa kuzingatia idadi ya wanafunzi na ikiwajumuisha na  hawa wanafunzi wenye mahitaji maalum,”anasema mwalimu Simchimba.

Leticia Singo ni  Mkuu wa  shule ya Umonga Sekondari  anasema shuleni hapo ana wanafunzi wanne wenye changamoto ya ulemavu na  wote ni wavulana .

Akiongelea hali ya miundombinu shuleni hapo  anasema  miundo mbinu  ni rafiki ukilinganisha na idadi  pamoja na aina ya ulemavu wa  wanafunzi alionao

.

Kwa kipindi cha nyuma sikuwa na madarasa ambayo ni rafiki kwa watoto nashukuru ukarabati wa mwaka jana, lakini na madarasa ya UVIKO pia yametusaidia

Mwalimu Singo.


Akitoa wito kwa Serikali,  Mwalimu Singo anasema  Serikali ione namna ya kuboresha miundombinu ya madarasa ya zamani ambayo hayakuwa na miundombinu rafiki kwa watoto  wenye ulemavu wa miguu watoto wanapata changamoto ya kuingia darasani na kuongeza kuwa  wakiwezesha fedha wakuu wa shule kupitia kamati zao za ujenzi watoe fursa ya kutumia hizo fedha kwaajili ya kuboresha miundombinu ambayo kwa sasa si rafiki kwa wanafunzi.

HAKI ELIMU.

Shule ya Sekondari Patandi ni moja ya shule zinazotoa elimu jumuishi ambako Wanafunzi wenye mahitaji Maalum wanasoma na wanasoma darasa moja na wanafunzi wasio na mahitaji maalumu.

Godfrey  Boniventura  Mkuu wa miradi kutoka Shirika la HAKI ELIMU  linalo jishughulisha na masuala ya utetezi wa kisera na kuhakikisha kwamba watoto wote wa kitanzania wanapata fursa ya kuwa shuleni na kupata elimu bora amesema moja kati ya eneo ambalo wanalifanyia kazi kwa sasa ni pamoja na eneo la Elimu Jumuishi (Inclusive Education).

“Elimu ya wanafunzi wenye mahitaji maalum kwa sisi  HAKI ELIMU  mchango wetu umekuwa hasa kwenye matukio ya huu mkakati wa Elimu Jumuishi ambao umezinduliwa mwaka huu 2022,  umebainisha namna unavyokwenda kubadilisha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi wenye mahitaji,’’

Anasema   kwenye uboreshaji wa elimu jumuishi uliozinduliwa mwaka huu ulitumia  mawazo na nyaraka kutoka shirika hilo limekuwa ni sehemeu ya kuboresha  mkakati huo

Anaeleza kuwa mkakati wa Elimu jumuishi  uliozinduliwa mwaka huu  2022 shirika limechangia  mawazo na nyaraka  mbalimbali za shirika hilo zimetumika  kuboresha mkakati huo na Serikali  imeahidi kuhakikisha kwamba  mpango huo  unatekelezwa.

Anaongeza  kusema  sekta ya elimu kwa sasa  ina mpango mama  ambao unaitwa( Education self development plan) wa miaka mitano na  mpango huo ndio unahuisha  mikakati ya makundi yote ikiwemo Elimu Jumuishi.

“Mpango huu wa miaka  mitano ndio unahusisha makundi yote ambayo yemeanza utekelezaji wake kwa mwaka  2021/ 2022  na umelitambua eneo  la Elimu Jumuishi kama eneo husika na limepewa eneo mahususi ambalo linazungumzia elimu ya msingi,  ndani  yake wakisema kuongeza udahili ubora  wana eneo la tatu wanaliita Elimu Jumuishi kwenye elimu ya msingi,elimu ya sekondari,vyuo vya kati na vyuo vikuu,

“Niseme tu kwamba  mpango mkakati huu umeweza kulitambua  kwa mapana  na umebainisha kwa namna gani wanaweza kubadilisha mazingira ya kujifunzia kwa watoto wenye mahitaji maalum” anasema Boniventura

AFISA ELIMU.

Upendo  Rweyemamu ni  Afisa Elimu Sekondari jiji la Dodoma anasema Serikali imekuwa ikikarabati miundombinu yake kwa wanafunzi wote mwaka hadi mwaka ili kukidhi mahitaji ya watoto wote wa kawaida na maalum.

“Zamani miundombinu ilikuwa ikijengwa ya kawaida lakini baada ya kugundua hilo tatizo kuanzia mwaka  2017 kuna mabadiliko mengi yanafanyika hasa katika miundombinu mipya ambayo inajengwa mfano kwa mwaka 2021 2022 tulitenga billion 3 kutoka mapato ya ndani kwaajili ya kujenga miundombinu mbalimbali kama madarasa maabara hostels nyumba za walimu na miundo mbinu mingine”

“Kwa upande wa Dodoma jiji ina jumla ya  wanafunzi  wa sekondari elfu  34,500  ambao ni jumla ya  shule za Serikali na binafsi ambapo  kwa shule za Serikali wanafunzi  jumla wapo elfu 32 napenda kusema kwamba  miundombinu yote iliyojengwa  na inayojengwa kwa sasa imezingatia mahitaji ya wanafunzi wenye mahitaji maalum kwa maana ya ngazi zao za kupandia darasani”anaeleza  mwalimu Rweyemamu

Rweyemamu anasema jiji la Dodoma  kwa idara ya sekondari ilipokea  bilioni 2 na milioni 860  kwaajili ya kujenga madarasa 143  na katika shule zote zilizojengwa hayo madarasa miundombinu ya madarasa hayo imezingatia mahitaji ya watoto maalum

“Kwa mwaka 2022/2023 tumetenga kupitia mapato ya ndani billion 1 na million 600 ili kuweza kuendeleza miundombinu hii ikiwa ni pamoja na maabara vyumba vya madarasa na miundombinu mingine .

“Lakini pia  kuna milion 400 kutoka Serikali kuu tumezibajetia ambazo zitakuwa na   ujenzi wa hostel bwalo pamoja na maabara wataalam wetu  ambao ni wahandisi wetu  wanazingatia miundombinu.”anasema Mwalimu Rweyemamu

 

Post a Comment

0 Comments