CWT YAITAKA SERIKALI KUENDELEA KUTATUA CHANGAMOTO ZA WALIMU

 ðŸ“ŒRHODA SIMBA

KATIKA kuadhimisha siku ya walimu Duniani Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kimeiomba Serikali iendelee kutatua changamoto mbalimbali zinazomkabili Mwalimu ili aweze kufanya kazi katika mazingira rafiki.

Aidha changamoto hizo ni pamoja na uhaba wa nyumba za walimu, kuongezewa mshahara, posho ya kufundishia upatikanaji wa mafunzo kwa walimu kazini yatakayo endelea kuwajengea uwezo katika majukumu yao.

Akizungumza Leo October 5 Wilayani Kondoa Mkoani Dodoma katika kikao kilichowakutanisha viongozi wa CWT ngazi ya Wilaya zote za Mkoa wa Dodoma pamoja na walimu kuadhimisha siku hiyo, Mkuu wa Idara ya elimu na mafunzo CWT Mwl. Stella Kiyabo amesema Kikao hicho kinalenga kutumia siku hiyo kujadili changamoto zinazomkabili Mwalimu.

Tunaipongeza Serikali ni kweli inapambana na Ujenzi wa madarasa pamoja na vyoo lakini pia ichukue tatizo la uhaba wa nyumba za walimu kuwa ni tatizo ambalo ni la kipaumbele na lina muathiri Mwalimu kwasababu vitu vyote hivyo vikiwepo Mwalimu akawa hana mahala pazuri pa kuishi unadhani atafanya kazi kwa weledi Serikali ilitazame hili kwa jicho la tatu

Mwl. Kiyabo

Amesema maslahi madogo yanamfanya Mwalimu kuingia kwenye mikopo katika benki mbalimbali ambazo baadae marejesho yanamfanya Mwalimu awe na msongo wa mawazo.

Mwalimu anakopa mikopo baadae inampa mawazo na haya mawazo yatamfanya atumie muda mwingi kuona namna ya kuyatatua, Mwalimu hajawahi kupata mafunzo tangu amalize shule wakati huo anakuwa na muda wa ziada wa kufundisha halipwi kwakweli Serikali ilitazame hili

Mwl Kiyabo

Amesema Serikali inapotoa muongozo wa usajili wa shule kuwa lazima uwe na Madarasa na matundu ya vyoo pia iweke suala la nyumba za walimu kuwa ni moja ya muongozo huo.

Shule inasajiliwa kwasababu ina madarasa ina matundu ya vyoo sasa nyumba za walimu hakuna haya huyu Mwalimu anaye kuja kufundisha hapo anapoishi hapajulikani unadhani kazi itafanyika vizuri, maana tunaona kasi ya mwanafunzi inaenda na Mwalimu, akiwa na msongo wa mawazo ya kukosa huduma za msingi unadhani kazi itafanyika vizuri?

Mwl.Kiyabo

Amesema takwimu za TAMISEMI za mwaka 2020 zinaonesha bado kuna mahitaji makubwa ya nyumba za walimu na zilizopo zimechakaa na zinahitaji matengenezo ya hali ya juu.

Kwa shule za msingi za binafsi na za Serikali nyumba zinazohitajika za walimu ni 251,052 lakini zilizopo ni 46,904 sawa na asilimia 81. Huku shule za sekondari za binafsi na Serikali nyumba zinazohitajika ni 95,690 zilizopo ni 44,364 pungufu ni 192,758 sawa na asilimia 81.

Mwl.Kiyabo

Naye Mjumbe wa Kamati Tendaji Taifa CWT Mwalimu Bakari Mtembo amesema kuwa ipo haja ya Serikali kupitia siku ya walimu duniani kuitambua na kuithamini kwa kuijengea afua.

Hii ni siku kubwa na muhimu kwa Mwalimu na itapendeza kila Mkoa kwa nafasi zao waweze kukutana kupitia siku hii na kutoa mawazo yao ili kuishauri Serikali, ni lazima Serikali itambue jukumu alilonalo Mwalimu

Naye Mwenyekiti wa CWT Wilaya ya Kondoa Ester Ntomola amesema ili mabadiliko yaweze kupatikana ni lazima Mwalimu ahusike kwa asilimia 100 kwasababu Mwalimu ndiye anamuandaa mwanafunzi ambaye baadae anakuwa kiongozi mkubwa.

Mwalimu asipomuandaa mwanafunzi hatuwezi kupata viongozi wazuri lakini akisimama bila ya kuwa na vikwazo tutapata viongozi wenye weledi na wenye uelewa hivyo basi Mwalimu ndiye kila kitu kwani yeye ndiye anazalisha Daktari, wahandisi, mawaziri na hata viongozi wa juu

Mwalimu Ntomola

Kila tarehe 5 ya mwezi Oktoba Dunia inaadhimisha siku ya Walimu Duniani ambapo kwa mwaka huu siku hii imebebwa na kauli mbiu isemayo "Mabadiliko ya elimu yanaanza na Mwalimu"



 

Post a Comment

0 Comments