JAMII YAHIMIZWA KUPAZA SAUTI VITENDO VYA UKATILI.

 ðŸ“ŒJASMINE SHAMWEPU

KATIBU Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. John Jingu ameitaka jamii, wadau na kila mmoja kwa nafasi yake kupaza sauti dhidi ya vitendo vya ukatili ambavyo vimekuwa vikiendelea katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Jingu ameyasema hayo Jijini Dodoma kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi wakati akifungua kikao cha Makatibu Wakuu na Manaibu Makatibu  Wakuu kuhusu  mafunzo ya Usawa wa Kijinsia na Tathimini ya Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA), Jijini Dodoma.

Amesema licha ya mafanikio yaliyopo kufuatia juhudi zinazofanywa kukabiliana na vitendo hivyo  lakini bado ukatili umeendelea kufanywa hivyo ipo haja ya kuwa na afua mbalimbali za kuwatetea manusura wa vitendo hivyo.

MTAKUWWA lengo lake ni kutokomeza ukatili wa aina zote unaofanywa katika jamii zetu sasa ukatili bado upo hivyo tumekubaliana kila mmoja wetu awe kinara wa mabadiliko chanya kuhakikisha tunakuwa na malezi bora, afua za kuyalinda makundi yote

Dkt. Jingu.

Vilevile ametoa wito  kila kundi kwa nafasi yake  Wizara za Kisekta, Taasisi za Serikali, Mashirika ya Kimataifa, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Viongozi wa Dini, Wazee wa Kimila na Vyombo vya Habari yana sehemu ya kufanya kwa kuongeza  juhudi za kuimarisha usawa wa jinsia na kutokomeza ukatili .

Nitoe rai tuendelee kushirikiana ili tuweze kutokomeza vitendo vya ukatili katika jamii na kufikia malengo  na mikakati tuliyojiwekea na nishukuru wadau wote kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali na kuhakikisha makundi yote yanalindwa dhidi ya ukatili wa kijinsia 

Amebainisha kwamba miongoni mwa masuala yaliyojadiliwa ni pamoja na kuwepo kwa Mpango maalumu wa malezi ya vijana balehe ili waweze kukua katika maadili, kujitambua na kufahamu nafasi yao kwa jamii.

Sambamba na hayo Dkt. Jingu ameeleza kuwa uzingatiaji wa bajeti kwa mtizamo wa kijinsia  katika Sera, Mipango na Bajeti za Wizara  na Sekta utasaidia  kuleta maendeleo endelevu katika nyanja zote za Kijamii.

Uandaaji wa bajeti na mipango kwa mtizamo wa kijinsia una manufaa makubwa sana katika jamii yetu kama kushughulikia upungufu wa kijinsia hususan ule unaotokana na uwepo wa mahitaji tofauti baina ya wanawake na wanaume katika jamii au sehemu zetu za kazi

Aidha aliwashukuru Wadau wa Maendeleo, Taasisi za serikali na binafsi, viongozi wa dini, kimila na mtu mmoja mmoja kwa kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuimarisha usawa wa jinsia na kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto hapa nchini.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake  na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula amewataka maafisa maendeleo kupitia ngazi ya Vijiji, Kata hadi Wilaya kutimiza wajibu wao kuhakikisha maendeleo yanapatikana, wananchi wanakuza  uchumi wao na kushiriki katika maendeleo kwa kulipa kodi.

Kupitia mafunzo haya tumeongea mambo mengi yakiwemo mpango wa Kitaifa wa malezi kwa makundi ya vijana balehe ambao una malengo mengi kama kuzuia UKIMWI, mimba za utotoni, ajira na matumizi ya dawa za kulevya pamoja na kumuandaa mtoto kuwa kiongozi bora kuanzia ndani ya familia

Dkt. Zainab.

Aidha Mratibu wa MTAKUWWA, Bw. Joel Mangi Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ameeleza kuwa tangu kuanza kwa mpango huo mwaka 2017/18 na 2021/2022 ambao umekamilika na kufanyika kwa tathmini ambayo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa ikiwemo kuongezeka kwa uelewa ndani ya jamii, uanzishwaji wa vituo 21 vya huduma kwa manusura wa ukatili ambapo vinafanya kazi nchi nzima.

Mwelekeo katika awamu ijayo tumependekeza kuanzishwa kwa kampeni jumuishi ya Kitaifa  itakayoleta sekta zote pamoja kupaza sauti , tuimbe kupinga ukatili huu jamii ijue vitendo hivi havifai kwa sababau vinazorotesha ustawi hasa kwa watoto 

Mratibu 

 

Post a Comment

0 Comments