JUMLA YA SH MILIONI 545.8 SERIKALI IMEKABIDHI TEMESA KUBORESHA UTENDAJI KAZI.

 ðŸ“ŒJASMINE SHAMWEPU

SERIKALI imenunua vifaa vya umeme na viyoyozi vyenye thamani ya sh.milioni 545.8 na kukabidhi kwa Wakala wa Ufundi na Umeme(TEMESA) ili kuboresha utendaji kazi.

Akikabidhi vifaa hivyo kwa TEMESA Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi sekta ya ujenzi Mhandisi Adelard Kweka alisema hizo ni jitihada za Rais Dk.Samia Suluhu Hassan za kuboresha utendaji kazi wa TEMESA.

Amesema matarajio ya Rais Dk. Samia ni kuona vifaa hivyo vinaenda kusimamiwa na kutunzwa vizuri ili vikaongeze tija iliyokusudiwa.

Tunamshukuru Rais Dk.Samia kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya kuboresha utendaji kazi wa TEMESA, hivyo sisi watendaji hatuna budi kuendelea kuunga mkono jitihada hizi kwa kuhakikisha vifaa hivi vinatunzwa ili vikatumike kwa muda mrefu na kuongeza tija

Katika hatua nyingine Mhandisi Kweka amesema serikali itaendelea kutoa fedha ili kuhakikisha TEMESA inasimama na kufanya kazi zake kwa ufanisi.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TEMESA Lazaro Kilahala amesema katika mwaka huu wa fedha serikali ya awamu ya sita ilitoa fedha sh.bilioni 3.9 kwa ajili ya ukarabati wa karakana za mikoa.

Amesema kupitia fedha hizo wanaendelea na ukarabati wa karakana katika mikoa ya Arusha, Mara, Kigoma, Tabora, Mtwara, Simiyu na Mwanza.

Tunatambua kuwa serikali inawekeza fedha nyingi kwa TEMESA kwasababu ya umuhimu wa shughuli za ufundi zinazotekelezwa hivyo sisi watumishi tunawajibu wa kuimarisha ubora wa huduma na kuongeza tija na ufanisi ili kukidhi matarajio ya serikali

Amesema kupitia fedha hizi ambazo Rais Dk.Samia amekuwa akitoa kwa ajili ya kutuboreshea huduma tunaahidi kufanya kazi kwa jitihada na weledi wa hali ya juu ili kufanikisha malengo ya serikali.

Kilahala amewataka Mameneja na Wakuu wa vituo vya TEMESA kuhakikisha wanatunza vifaa hivyo na kuvitumia kwa ufanisi na tija ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Serikali inataka kuona TEMESA inaimarika na kuchagia zaidi katika maendeleo ya nchi hivyo tunapopokea vitendea kazi hivi pia tulitambue deni tulilonalo kwa serikali na wananchi kwa kuongeza tija na ufanisi katika utoaji wa huduma zetu

Amefafanua kuwa fedha zilizotolewa na Rais Dk.Samia zingeweza kuelekezwa katika kutimiza mahitaji mbalimbali ya watanzania ikiwemo kuboresha huduma za afya, elimu na maji lakini zimeelekezwa TEMESA kwa sababu maalumu.


Post a Comment

0 Comments