UCSAF YAINGIA MIKATABA KUFIKISHA HUDUMA ZA MAWASILIANO

 ðŸ“ŒRHODA SIMBA

MFUKO wa Mawasiliano kwa wote (UCSAF) umeingia mikataba ya kufikisha huduma za mawasiliano katika kata 1,242 zenye vijiji 3,654, na wakazi 15,130,250 ili kuimarisha huduma za mawasiliano nchini.

Hayo yamesemwa leo Februari 13 2023, jijini Dodoma na Mtendaji Mkuu wa Mfuko huo Justina Mashimba, wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Mfuko huo kwa waandishi wa habari.

Amesema pia minara 1,087 yenye vijiji 3,378 na wakazi 13,320,750 inatarajiwa kujengwa nchini.

Utekelezaji unaendelea katika Minara 155 yenye vijiji 276 na wakazi 1,809,500 ruzuku iliyotolewa kufanikisha kazi hii ni Sh. bilioni 199

Kadhalika, amesema mradi mwingine ni ule wa kimkakati wa Zanzibar,  wa minara 42, katika  Shehia 38 na ruzuku ilyotolewa ni Sh. bilioni 6.9.

Kuhusu mradi wa kupeleka vifaa vya TEHAMA alisema jumla ya shule 811 nchini zimefikiwa hadi sasa.

Vilevile amesema kwa wastani shule hupewa kompyuta tano , Printa moja na Projekta moja.

Kwa mwaka wa fedha 2022/23, Shule 150 zitafikishiwa vifaa vya TEHAMA Bajeti kwa mwaka wa fedha 2022/23 ni Sh.1,950,000,000

Aidha amesema Mradi wa kupeleka vifaa maalum vya kujifunzia kwa shule zenye watoto wenye mahitaji maalum, Shule 16 zimefikishiwa vifaa vya TEHAMA ambavyo ni pamoja na TV, Braille Machine (Nukta Nundu) Orbit reader (Machine za Kisasa), Laptops, Embosser (Printa ya nukta nundu).

Amesema shule zitakazonufaika ni pamoja na shule ya Sekondari ya Mpwapwa (Mpwapwa-Dodoma), Sekondari ya Mkolani (Mwanza), Sekondari ya Kashaulili (Mpanda-Katavi), Sekondari ya Morogoro (Morogoro).



 

 

 

Post a Comment

0 Comments