MHANDISI MCHARO - ZAIDI YA TRILIONI 29 ZAWEKWA KWENYE MFUMO WA NeST.

📌RHODA SIMBA

IMEBAINISHWA kuwa  zaidi ya Shilingi Trilioni 29 imewekwa kwenye mfumo wa NeST kwa ajili ya kufanya ununuzi wa bidhaa, huduma na kazi za ujenzi, ambapo  hadi kufikia Aprili 09, 2024 mikataba ya zaidi ya Shilingi Trilioni 5.14 imetolewa kwa wazabuni kupitia mfumo huo ambapo wazabuni 18,101 wamejisajili kwenye mfumo huo.

Hayo yamesemwa leo April 9, 2024 jijini Dodoma na Mkurugenzi wa huduma za ushauri na kujenga uwezo Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) Mhandisi Amini Mcharo,  wakati akitoa taarifa kwa waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya miaka mitatu ya Rais wa Jamhuri Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan na mageuzi makubwa katika ununuzi wa umma nchini.

Kufuatia ushiriki wa makundi maalum katika ununuzi wa umma hadi kufikia Februari 2024, jumla ya tuzo za mikataba zenye thamani ya shilingi bilioni 1.95 zimetolewa kwa makundi maalum kupitia zabuni za umma zilizotangazwa na taasisi  nunuzi kupitia mfumo wa ununuzi wa kielektroniki (NeST)

Ambapo kundi la vijana wamepata tuzo za mikataba zenye thamani ya shilingi milioni 709 , wanawake shilingi bilioni 1.2 na wazee shilingi milioni 78.3

Mhandisi Mcharo.

Aidha, amesema katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita mamlaka ilifanya uchunguzi kwa zabuni zilizotekelezwa katika mwaka wa fedha 2021/22 na 2022/23, na kufanikiwa kuokoa jumla ya fedha za umma kiasi cha Shilingi Bilioni 16.27. 

Kati ya fedha hizo, kiasi cha Shilingi Bilioni 13.83 ilitokana na kuingilia kati kwa Mamlaka kwenye mikataba ambayo ilitolewa kwa wazabuni wenye bei ya juu wakati wenye bei ya chini wakitolewa kwenye mchakato (disqualified) na kiasi cha shilingi bilioni 2.44 ni kiasi kilichorudishwa na wasambazaji wa bidhaa (suppliers) na wakandarasi kwa malipo ya ziada yaliyofanywa na taasisi nunuzi

Mhandisi Mcharo.

Pamoja na hayo Mhandisi Mcharo amesema kutungwa sheria mpya ya ununuzi wa umma Na. 10 ya mwaka 2023 “Kipekee, sheria hii imeweka masharti muhimu yatakayohakikisha uwepo wa upendeleo wa bidhaa na wazabuni wa ndani, ambapo inatarajiwa kuwa zabuni zote zilizo chini ya bilioni 50 zitafanywa na wazawa,”

Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) ina dhamana ya kusimamia  sekta ya ununuzi wa umma kwa lengo la kuwezesha upatikanaji wa thamani ya fedha kwenye ununuzi na ugavi, kuhakikisha uzingatiaji wa haki, ushindani, uwazi na kufuatilia uzingatiaji wa sheria kwa taasisi za umma, pamoja na kujenga uwezo katika Ununuzi wa umma kwa kushirikiana na wadau. 

 




 

 

Post a Comment

0 Comments