DKT. SAMIA SULUHU HASSAN AWAHIMIZA VIONGOZI WA CCM KUHAMASISHA VIJANA KUJIJIANDIKISHA KUPIGA KURA

 



📌BAHATI MSANJILA.

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka viongozi wa chama hicho kuhamasisha vijana kujijiandikisha kwenye daftari la Tume ya Uchaguzi ili waweze kushiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Dkt. Samia ameyasema hayo leo jijini Dodoma, katika kilele cha maadhimisho ya miaka 48 ya chama cha mapinduzi, yaliyofanyika uwanja wa Jamhuri. Alisisitiza umuhimu wa kila mwanachama kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura, akisema kuwa ni hatua muhimu katika kuhakikisha haki ya kupiga kura inatambulika.

“Vijana, tunahitaji kuhakikisha mnaingia kwenye daftari la wapiga kura ili kushiriki kwenye uchaguzi. Bila ya kuwa kwenye daftari, hatuwezi kupiga kura.

Hivyo, ni muhimu vijana wote wa Kitanzania waende na kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura,” alisisitiza Dkt. Samia.

Katika hotuba yake, Dkt. Samia alitaja kuwa CCM inajivunia mafanikio ya chama, ikiwemo kuwa na zaidi ya wanachama milioni 12 na wapenzi wengi, huku akieleza kuwa chama kimejipanga vema kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

“Chama cha Mapinduzi kina mtaji mkubwa unaotokana na kukubalika kwake na utekelezaji mzuri wa ilani yetu. Tumekuwa na mafanikio katika nyanja mbalimbali, na sasa tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu tukiwa na nguvu kubwa,” alisema.

Dkt. Samia pia aliwashukuru wanachama wa CCM kwa imani yao, akieleza kuwa chama kitashinda uchaguzi wa 2025 kwa kushirikiana na wananchi.

Akizungumza kuhusu vijana, Dkt. Samia alisema kuwa ni muhimu kuwajengea uwezo wa kisiasa na kiitikadi, ili waweze kuimarisha jumuiya za Umoja wa Wanawake (UWT) na jumuiya ya Wazazi. Alisisitiza umuhimu wa kuwa na viongozi vijana ambao wangeimarisha chama katika ngazi zote.

Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Emmanuel Nchimbi, alifafanua kuwa sherehe za maadhimisho ya miaka 48 ya chama hicho zitaendelea kufanyika kila baada ya miaka mitano, na mwaka huu sherehe hizo zilifanyika kitaifa, zikihusisha mikoa mbalimbali. Alieleza kuwa kaulimbiu ya sherehe za mwaka huu inasisitiza uadilifu katika uchaguzi na aliwataka wanachama wa CCM kushiriki kwa uadilifu ili kuendeleza mafanikio ya chama.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma, Alhaji Adam Kimbisa, alitoa ahadi ya kushinda kwa kishindo uchaguzi wa 2025, akisema, “Tunaahidi kuleta ushindi shindo hapa Dodoma,” na kuongeza kuwa wananchi wa Dodoma wataunga mkono chama kwa nguvu zote.

Sherehe hizo zilijumuisha shughuli mbalimbali za jumuiya za CCM na ziara za viongozi mbalimbali, na kilele chake kilifanyika jijini Dodoma.

 


Post a Comment

0 Comments