SERIKALI IBORESHE POSHO ZA WALIMU.

 


📌Na DEVOTHA SONGORWA.

WAZIRI Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda ameomba Serikali kuboresha posho na maslahi ya walimu hasa wanaofundisha shule za awali akisema kazi yao ni ngumu na wanastahili kupongezwa.

Pinda ambaye ni Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) ametoa kauli hiyo wakati wa kugawa vyeti kwa walimu 436 wa shule za msingi kutoka wilaya za Chemba na Mpwapwa.

Walimu hao walikuwa kwenye mafunzo maalumu ya Stashahada kwa walimu wanaofundisha shule za msingi katika masomo ya awali ambao mafunzo yao kwa miaka miwili yaligharamiwa na Chama cha Walimu Tanzania (CWT).

Mstaafu huyo aliahidi kuwa atawasiliana na Waziri wa Elimu (Profesa Joyce Ndalichako) ili kufikisha kilio cha walimu kuhusu maslahi na posho zao lakini kwake anaamini wanaofundisha madarasa ya chini ndiyo wanastahili kupewa kipaumbele licha ya kuwa kazi ya kufundisha ni ngumu.

“Kwa kweli tukubaliane, posho za walimu hasa wa masomo ya awali ni muhimu zikatazamwa upya, na mimi nitazungumza na Waziri angalau nifikishe kilio chenu kwake ili waone namna ya kulifanya jambo hili ambalo naamini likitekelezwa litaleta tija,” amesema Pinda.

Akizungumzia walimu hao, aliwataka kuwa na mabadiriko chanya katika shule wanazokwenda kufundisha ili wasio na elimu kama yao wakajifunze umuhimu na faida ya Mwalimu kusoma zaidi.

Amesisitiza kwa Serikali na CWT kuwasiliana na wadau wengine kwa pamoja wafufue vituo vya walimu (Teacher Center) ambavyo vilikuwa ni msaada katika kuwafanya walimu waende na wakati.

Amekiagiza OUT kuanzisha mjadala kuhusu ubora wa elimu nchini ambao unalalamikiwa na wengi kuwa umeshuka ili waone kama kuna ukweli wowote kuhusu kauli hiyo na nini cha kufanya.

Rais wa CWT Leah Ulaya,amesema pamoja na kufanya kazi kwa juhudi na maarifa, lakini walimu bado wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo suala la maslahi yao kutoboreshwa.

Ulaya alimwomba Pinda kufikisha kilio chao kwa Rais John Magufuli ili aweze kuwatazama kwa jicho la Huruma huku wao wakiahidi kufanya kazi katika mazingira yoyote watakayopangiwa.

Awali Katibu wa CWT Deus Seif amesema waliwadhamini walimu hao kusoma Stashahada kwa ushirikiano Shirikisho la vyama vya walimu duniani (EI).

Seif alisema CWT imeachana na mpango wa malalamiko badala yake kimeamua kujikitza zaidi kwenye kuwasomeha walimu ili wawe na manufaa na uelewa wa pamoja ambao utazaidia kulijenga Taifa.

 

Post a Comment

0 Comments