JE UNAFAHAMU UHUSIANO KATI YA MJI MKUU WA DODOMA NA HAYATI JOHN POMBE MAGUFULI?




📌EZEKIEL KAMWAGA

Imesadifu kwamba msiba wa kitaifa wa hayati Rais John Magufuli aliyefariki dunia Machi 17 mwaka huu, utafanyika katika jiji la Dodoma - ambalo kama isingekuwa uongozi wake pengine bado usingekuwa na hadhi ulionayo leo.

Wakati Magufuli akiingia madarakani mwaka 2015, hakuna aliyetaraji kuwa serikali nzima ingekuwa imehamia huko katika kipindi cha miaka mitano yake ya kwanza tu madarakani.

Ingawa serikali ilifanya uamuzi wa kufanya Dodoma kuwa makao makuu ya nchi mnamo mwaka 1973, jambo hilo -kwa sababu tofauti tofauti, halikuweza kufanikiwa hadi Magufuli alipoonyesha kwamba inawezekana tena ndani ya muda mfupi.

Wakati Watanzania na wananchi wa Dodoma wakimuaga katika Uwanja wa Jamhuri mnamo Machi 22 mwaka huu - itakuwa ni buriani kwa mwanasiasa ambaye kipekee kabisa alikuwa na maono na nguvu ya kutekeleza alichokipanga, hata kama jambo hilo halilikubaliwa na wengi.

Danadana za Dodoma kuwa makao makuu

Serikali iliamua kuifanya Dodoma kuwa makao makuu kwa sababu moja kubwa - kwamba tofauti na Dar es Salaam iliyo pembezoni Mashariki mwa nchi, yenyewe iko katikati ya nchi na hivyo ni rahisi kufikika kwa watu wote.

Mpango wa serikali ulikuwa kwamba mchakato huo wa kuhamia Dodoma uchukue muda wa miaka 10. Kwa maana hiyo, serikali ilitakiwa iwe imehamia huko kufikia mwaka 1983.

Kampuni ya masuala ya mipango miji ya PPAL kutoka Canada ndiyo ilipewa kazi ya kupanga namna mji huo utakavyokuwa - wenye bustani za kutosha, njia za watembea kwa miguu, baiskeli na magari na mbwembwe zingine. Kwa sababu Tanzania ilikuwa ikifuata sera za kijamaa wakati huo, Dodoma pia ilitakiwa kuakisi itikadi hiyo katika kujengwa kwake.

Ingawa aliyekuwa Rais wa Tanzania wakati huo, hayati Julius Nyerere, alikuwa na nia ya dhati ya kuhamia Dodoma, matukio yaliyofuata baada ya uamuzi huo yalisababisha serikali isitimize dhamira yake hiyo.

Katikati ya miaka ya 1970, dunia iliingia katika mtikisiko wa uchumi uliosababisha hali ngumu na baadaye Tanzania ikapata majanga ya kuvunjika kwa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka 1977 na Vita ya Kagera ya mwaka 1978/79 ndiyo ikazima kabisa ndoto hizo.

Wakati Ali Hassan Mwinyi alipoingia madarakani mwaka 1986, uchumi wa Tanzania ulikuwa katika hali mbaya sana kiasi kwamba isingewezekana kupata fedha za kutumia kwenye ujenzi wa mji mkuu mpya.

Kufikia mwaka 1993, mmoja wa wasomi maarufu kutoka Chuo Kikuu Kishiriki cha Ardhi, Lusuga Kironde, aliandika chapisho maarufu lililoeleza kwamba ingawa takribani dola milioni 4.9 (zaidi ya shilingi bilioni 10 kwa viwango vya sasa) zilikuwa zimetumika kwenye mradi wa kuhamia Dodoma, ilikuwa vigumu kwa ndoto hiyo kutimia.

Mwaka 2004, msomi mwingine mashuhuri, Dk. Aloysius Mosha, kutoka Chuo Kikuu cha Gaborone nchini Botswana, aliandika chapisho lililoonyesha kwamba jambo hilo ni kama limeshindika - labda kama atapatikana mtu mwenye uwezo wa kulisukuma mbele.

Kila nikisikia kuhusu uamuzi wa Magufuli kuhamishia serikali Dodoma, huwa nakumbuka tukio moja la mwaka 2017.

Nilikuwa mji mkuu kwenda kumsalimu mmoja wa rafiki zangu ambaye alikuwa ameteuliwa kuwa Naibu Waziri katika Serikali ya Rais huyo wa Awamu ya Tano.

Nilipoingia ofisini kwake, sikuona jambo lolote lililonionyesha kuwa niko ofisini kwa mtu wa wadhifa wake. Kaofisi kalikuwa kadogo na watu wamebanana kwelikweli.

Wizara mbili tofauti zilikuwa zimehamishiwa sehemu moja.

Kuna watumishi walikuwa wakilalamika kwamba wamelazimishwa kuhamia Dodoma wakati mji wenyewe hauna maji, shule wala huduma muhimu za kiwango cha juu katika maeneo kama afya na mengineyo. Sikuona watu wenye furaha katika ofisi zile za serikali.

Lakini Magufuli alishikilia ajenda hiyo na sasa, hata kama kuna minong'ono ya hapa na pale, watumishi wa serikali wamekubali kuwa Dodoma ndiyo makao makuu ya nchi.

Huduma za muhimu zimeanza kuimarika ikiwamo ujenzi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, shule kadhaa binafsi za kimataifa zimeanza kujengwa Dodoma na bei za viwanja zimeanza kupanda.

Miaka mitatu iliyopita, mkoa huo uliongoza kwa kukusanya kodi kubwa kuliko mikoa yote nchini na Magufuli mwenyewe alimalizia ujenzi wa Ikulu ya Chamwino na katika siku zake za mwisho madarakani alikuwa akikaa zaidi Dodoma kuliko Dar es Salaam.

Katika siku ya mwisho ya kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020, Magufuli alishangaza wengi kwa uamuzi wake wa kuamua kutumia siku hiyo kuzungumza na wazee wa mkoa wa Dodoma badala ya kufanya mkutano wa hadhara kama ilivyozoeleka.

Huko nyuma, ilizoeleka kwa marais wa Tanzania kuhutubia taifa kupitia mazungumzo na wazee wa mkoa wa Dar es Salaam lakini hatua ile ya Magufuli ilionyesha rasmi sasa kwamba mamlaka yamehamia rasmi Dodoma na si kwa maneno pekee bali matendo.

Dodoma itaendelea kung'ara baada ya Magufuli?

Wakati wananchi na viongozi wakijiandaa kumuaga Magufuli, swali kubwa ambalo litakuwa vichwani mwa wengi ni endapo uongozi wa Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, utaendeleza alipoishia Magufuli au utarejea Dar es Salaam kulikozoeleka.

Kuna mambo makubwa ambayo Magufuli aliahidi kwa watu wa Dodoma ambayo yanasubiriwa kwa hamu. Kwanza watu wanasubiri kukamilika kwa reli ya mwendokasi (Standard Gauge) ambayo hatua yake ya pili itaishia eneo la Makutupora.

Lingine ni ujenzi wa uwanja mkubwa wa kisasa wa mpira wa miguu unaotarajiwa kutoa ajira nyingi kwa vijana wa mkoa huo. Ni uwanja uliopangwa kuwa na uwezo wa kuingiza watazamaji wengi kuliko ule wa Benjamin Mkapa uliopo Dar es Salaam.

Lakini bado Dodoma inahitaji ofisi nyingi zaidi, majengo mengi zaidi, shule nyingi zaidi na huduma nyingi za maendeleo.

Katika chapisho lile la Kironde, alionyesha kwamba fedha nyingi zilizotumika katika awamu zilizopita ziliangalia eneo la huduma pekee na si miundombinu.

Utawala wa Magufuli ulikuwa maarufu kwa kuangalia miundombinu.

Watanzania wanamlilia Magufuli kwa mengi, lakini wananchi wa Dodoma watamlilia zaidi kuliko wengine Tanzania - labda wakizidiwa tu na watu wa mahali alikozaliwa; Chato.

Kwao, huu ni msiba wa Rais aliyeupenda mkoa wao. Huu ni msiba wa Rais aliyewapenda watu wa Dodoma - akiwatania kama watani zake kila alipopata fursa ya kufanya hivyo.

Kwao, huyu ndiye Rais aliyeuvunja mfupa uliowashinda watangulizi wake wote wengine katika ofisi hiyo.

 MAKALA HII IMETOKA BBC SWAHILI

 

Post a Comment

0 Comments