AFISA WA TAKUKURU AKAMATWA KWA KUOMBA RUSHWA

 


📌MWANDISHI WETU

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imamkamata mtumishi wa taasisi hiyo aitwaye Zainab Mohamed Jabir, kwa kosa la kuomba na kupokea Rushwa – Kinyume na Kifungu cha 15 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11 ya Mwaka 2007.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Afisa Uhusiano wa TAKUKURU, Doreen Kapwani kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa taaisis hiyo,mtumishi huyu aliomba rushwa kiasi cha shilingi Milioni 50 kutoka kwa mtu mmoja (Jina limehifadhiwa) kwa madai ya kumsaidia mtu huyo katika tuhuma dhidi yake ambazo zinachunguzwa na TAKUKURU.

Kapwani amesema uchunguzi dhidi ya tuhuma zinazomkabili mtumishi huyo unaendelea na utakapokamilika hatua stahiki zitachukuliwa.

Pia Kapwani ametahadhalisha umma uwepo wa tabia ya baadhi ya watu wanaofanya UTAPELI kwa kujitambulisha kwa vyeo tofauti tofauti ikiwemo Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa - TAKUKURU.

Amesema kuwa matapeli hao wamekuwa wakipiga simu na kujitambulisha kuwa wao ni Maafisa wa TAKUKURU wakiwaeleza watu hao kwamba tuhuma zao zipo TAKUKURU na kwamba wanawaita TAKUKURU kwa ajili ya mahojiano.

Unapopokea simu ya aina hii tafadhali fika katika ofisi ya TAKUKURU iliyoko karibu nawe kwani TAKUKURU ina ofisi katik mikoa yote na Wilaya zote Tanzania Bara

TAKUKURU inawapongeza wale wote walioweza kubaini kuwa watu hawa ni MATAPELI na kutoa taarifa TAKUKURU mara moja. Hata hivyo, tunaendelea kusisitiza wananchi kutokubali kutapeliwa na mtu yeyote.

Hata hivyo Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU amewashukuru wananchi na wadau wengine wote ambao wamekuwa wakishirikiana na taasisi hiyo katika kufanikisha jukumu la kuzuia na kupambana na rushwa nchini kwa kutuletea taarifa za wale wote wanaojihusisha na vitendo vya rushwa.

 UMEISOMA HII?👇👇👇

MITAMBO YA KUFUA HEWA TIBA (OKSIJENI) YASIMIKWA HOSPITAL 7 ZA RUFAA,KUPAMBANA NA MATATIZO YA UPUMUAJI

Post a Comment

0 Comments