WAHANDISI WATAKIWA KUONGEZA UBUNIFU



 ðŸ“ŒMWANDISHI WETU

KATIBU Mkuu, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Ujenzi), Mhandisi Joseph Malongo, amewataka wahandisi nchini kujiendeleza kitaaluma na kuongeza ujuzi mara kwa mara ili waweze kulisaidia Taifa katika utekelezaji na usimamizi wa miradi mikubwa na ya kimkakati nchini.

Amesema hayo leo Jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya usimamizi wa miradi kwa wahandisi yalioandaliwa na Bodi ya Usajili wa Wahandisi nchini (ERB).

Malongo ameipongeza Bodi hiyo kwa utaratibu wa kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa wahandisi na kuwataka kuendeleza utaratibu huo ambao unawajenga kitaaluma na kimaadili uwe endelevu.

Aidha amezungumzia umuhimu wa Bodi hiyo kuanzisha mfuko maalum wa wahandisi utakaowawezesha kuwajengea uwezo wahandisi kiuchumi na hivyo kumudu kuwaendeleza.

Hakikisheni mnatembelea miradi mikubwa inayoendelea nchini ili kujifunza changamoto zilizopo na kuzipatia ufumbuzi

Mhandisi Malongo.

Naye mwenyekiti wa Bodi ya ERB, Mhandisi Ninatubu Lema, amesema wahandisi wamejipanga kuhakikisha Sekta ya Ujenzi nchini inaimarika na hivyo watashirikiana na Serikali ili kuhakikisha miradi inayojengwa inawiana na thamani ya fedha.



Kwa upande wake Msajili wa Wahandisi, Mhandisi Patrick Barozi, amesema mafunzo ya usimamizi wa miradi yataendelea kutolewa ili kuimarisha uwezo wa wahandisi nchini na kuwataka wahandisi wenye sifa kujisajili na Bodi hiyo.

Zaidi ya wahandisi elfu 30 wamesajiliwa na Bodi ya Usajili wa Wahandisi  (ERB), katika fani mbalimbali hapa nchini na mafunzo hayo yatawawezesha wahandisi hao kubobea kwenye fani zao na kuongeza ubunifu kwenye utekelezaji na usimamizi wa miradi katika maeneo yao.

 

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,
Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

 

 

Post a Comment

0 Comments