ZAIPUNA: NMB KUSHIRIKIANA NA SERIKALI KUFIKISHA HUDUMA BORA KWA WANANCHI KUPITIA TEKNOLOJIA


 

         ðŸ“ŒBAHATI MSANJILA


Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna, amesema benki hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali kwa kutumia majukwaa yake kuhakikisha huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi za umma zinawafikia wananchi kwa urahisi, ufanisi na ubora unaotakiwa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam mbele ya maafisa kutoka Wizara ya Katiba na Sheria waliokuwa katika ziara ya mafunzo ya siku mbili ndani ya benki hiyo, Zaipuna alieleza kuwa NMB imewekeza kwa kiasi kikubwa katika teknolojia ya kisasa inayowezesha utoaji wa huduma bora kwa wateja, pamoja na kubuni suluhisho mbalimbali kwa changamoto za kijamii.

Mbali na teknolojia, benki hiyo pia imejikita katika utawala bora na kuwajengea uwezo wafanyakazi wake ili kuhakikisha kila huduma inayotolewa inakidhi viwango vya juu vya kitaalamu. Kupitia ushirikiano kati ya taasisi binafsi na serikali, NMB inaamini changamoto nyingi za wananchi zinaweza kutatuliwa kwa pamoja kwa haraka na ufanisi zaidi.

Kwa upande wao, maafisa kutoka Wizara ya Katiba na Sheria walieleza kuwa ziara yao imelenga kujifunza namna bora ya kuboresha kituo cha huduma kwa wateja walichokianzisha mwaka jana, ambacho kinapokea malalamiko ya kisheria kutoka kwa wananchi kupitia simu na mitandao ya kijamii.

Kwa mujibu wa wizara hiyo, lengo la kituo hicho ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata haki yake kwa wakati ili kujenga jamii tulivu, inayoweza kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, na hivyo kuchangia katika kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Katika ziara hiyo, maafisa hao walitembelea vitengo mbalimbali vya huduma kwa wateja ndani ya benki hiyo na kujionea namna teknolojia inavyotumika kuboresha huduma, jambo lililowapa mafunzo ya moja kwa moja yatakayosaidia katika maboresho ya huduma za wizara yao.








Post a Comment

0 Comments