FAO YAZINDUA MFUMO WA UCHAMBUZI WA UHAKIKA WA CHAKULA NA LISHE TANZANIA KUBORESHA HALI YA LISHE




📌DOTTO KWILASA

SERIKALI  imewataka wataalamu wanaofanya tathimini ya uhakika wa usalama wa chakula na lishe  kufanya tathmini hizo kwa kuzingatia mazingira husika kwa kuangalia mitazamo ya ndani ya nchi badala ya kutumia mifumo ya nje ambayo wakati mwingine hukosa uhalisia wa maisha ya watanzania.

Hayo yamesemwa Jijini hapa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya kilimo, Prof. Siza Tumbo wakati akizindua Mfumo wa Uchambuzi wa Uhakika wa Chakula na Lishe Tanzania (MUCHALI) unaoratibiwa na Shirika la kilimo na chakula  la Umoja wa Mataifa (FAO) kwa kushirikiana na Wizara ya kilimo nchini.

Prof.Tumbo amesema, hali ya kufanya tathmini ya chakula  nchini bado hairishishi kwani mara nyingi wataalamu hutumia mbinu za kutoka nje na kuzitumia katika kufanya tathmini za ndani ya nchi jambo ambalo linatakiwa kufanyiwa marekebisho.

Tafiti nyingi za masuala ya chakula na lishe hazijaleta mafanikio kwa sababu Mara nyingi wataalamu wetu hawazingatii uhalisia wa maisha ya watanzania yalivyo,nawaomba mnapofanya tafiti,tafiti zenu ziendane na mazingira husika

Mbali na hayo Naibu Katibu mkuu huyo ametumia nafasi hiyo kuwataka watanzania kuzingatia ulaji wa vyakula vya asili vinavyojenga na kuongeza kinga ya mwili hali itakayoimarisha afya badala ya  kutumia vyakula vya kisasa ambavyo asilimia kubwa huchangia udhaifu wa kinga ya mwili .

Amesemà,nchini Tanzania maeneo yote yamezungukwa na vyakula vya asili hivyo ni wajibu kuvitumia ili kukabiliana na maradhi mbalimbali ambayo wakati mwingine hutokana na ulaji wa vyakula vilivyosindikwa usio na mpangilio  .

Kwa umuhimu huo,amewataka wataalamu hao wa mfumo wa uchambuzi wa chakula na lishe kujiendesha kidijitali ili kuweza kuwa sehemu ya dunia.

Dunia ikiwa katika Mfumo wa digitali hatuna pa kujifisha,hatua hii ya MUCHALI inapaswa kuendeshwa kisasa zaidi ili kuwa na nguvu ya pamoja

Naye  Mtaalamu wa  Lishe  kutoka Shirika la Mpango wa Kilimo na Chakula  la Umoja wa Mataifa (FAO),Stella Kimambo amesema muongozo uliozinduliwa utatathmini hali ya chakula na lishe kwa ngazi ya mkoa na wilaya .

Mbali na hayo ameainisha  hatua muhimu ambazo zitachukuliwa na MUCHALI Kupitia  wadau wengine wakati wa ukusanyaji kuwa ni pamoja na  uchambuzi na usambazaji wa taarifa za usalama wa chakula ili jamii ipate mwamko na kuwa na matumizi sahihi ya lishe .

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Uhakika wa Chakula na Lishe kutoka Zanzibar,Hamad Masoud Ali amesema kuwa amefurahishwa na mwenendo mzima wa MUCHALI huku akisisitiza kuwa hatua hiyo inapaswa kuendeshwa kidijitali ili kufanikiwa.

Kutokana na hayo ameahidi kufanya mabadiliko ya muongozo wa tathmini ya usalama wa chakula na lishe kwa upande wa Zanzibar kwa kuzingatia  mabadiliko ya kisera ikiwemo muundo wa serikali za mitaa ambao awali haukuwepo ili kufanikisha zoezi hilo.

Post a Comment

0 Comments