TAASISI YA ELIMU YA WATU WAZIMA IMEWAFIKIA WASICHANA 3,333 WALIOSHINDWA KUENDELEA NA MASOMO.

 ðŸ“ŒRHODA SIMBA

TAASISI ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) imesema kuwa imefanikiwa kuwafikia wasichana 3,333 sawa na asilimia 111 ya lengo ambao walishindwa kuendela na shule ya sekondari kutokana na mazingira magumu, kupata ujauzito na ndoa za utotoni.

Hayo yamebainishwa leo Oktoba  24 jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima Dkt.Emanuel Ng'umbi ambapo amesema kuwa wameendesha mafunzo kwa nyakati tofauti kwa wasimamizi na watendaji, wawezeshaji na walimu wa madarasa ya mradi wa SEQUIP.

Kwa mwaka 2022/2023, TEWW itaendelea kushirikiana na Wizara ya Elimu Sayansi na Tekonolojia katika kuandaa Juma la Elimu ya Watu Wazima kwa mwaka 2023,vile vile, TEWW itahamasish kusajili na kufundisha wanafunzi 3,000 wa mradi wa SEQUIP kwa mwaka 2023.

Amesema kuwa TEWW inatarajia kupanua mpango wa IPOSA katika mikoa mipya sita (6), kwa kujenga karakana za kufundishia, na pia kupanua mafunzo ya TEHAMA kwa wanafunzi wa IPOSA. Kwa upande wa programu ya IPPE, TEWW inatarajia kuanza kusajili vituo vya mafunzo vitakavyotumia mtaala ulioboreshwa wa IPPE.

Ameeleza kuwa TEWW imekusanya takwimu za hali ya kisomo kutoka mikoa yote ya Tanzania bara na inaendelea na uchambuzi wa taarifa na takwimu hizo ikiwa ni hatua ya mwanzo ya utafiti wa hali ya kisomo na elimu kwa umma nchini. 

Katika mwaka 2022/2023 TEWW itaendelea kutekeleza majukumu yake katika eneo hili, ikiwa ni pamoja na kuendelea kuwatumia wanachuo wake katika kufungua vituo vya kisomo nchi nzima ikiwa ni sehemu ya mafunzo kwa vitendo, TEWW pia inatarajia kuandaa, kuchapisha na kusambaza ripoti ya hali ya kisomo katika mikoa ya Tanzania bara

Kuboresha miundombinu ya ujifunzaji na ufundishaji katika mwaka 2021/2022, kwa kupitia mradi wa SEQUIP, TEWW ilikarabati majengo ya ofisi na madarasa katika mikoa minne ya Dar es Salaam, Morogoro, Ruvuma, na Dodoma. Halikadhalika, TEWW ilianza ujenzi wa majengo ya ofisi na madarasa katika mikoa minne ya Pwani, Rukwa, Iringa na Manyara,"amesema.

Aidha amesema kuwa jumla ya TZS 1,200,000,000/= zimetumika. Pia TEWW ilianza ujenzi wa jengo la utawala katika kampasi ya Morogoro kwa kutumia fedha kutoka serikali kuu. 

Amesema kiasi cha TZS 50,000,000/= kilitolewa na serikali kuu kwa ajili ya kazi hiyo kwa mwaka 2021/2022 na katika mwaka wa 2022/2023, TEWW inatarajia kuendelea na ujenzi wa madarasa na ofisi katika vituo vya mikoa sita (6) na ukarabati katika vituo vya mikoa miwili.

Ikumbukwe kuwa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) ni Taasisi ya Umma iliyoanzishwa chini kwa Sheria ya Bunge Na. 12 ya Mwaka 1975; ikiwa ni taasisi chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambayo jukumu la TEWW kusimamia elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi nchini.

 

Post a Comment

0 Comments