NMB YADUMISHA MICHEZO JWTZ KWA KUKABIDHI VIFAA VYA MIL. 19 KWA TIMU ZA MASHUJAA

 



📌BAHATI MSANJILA

Benki ya NMB inaendelea kuonesha dhamira yake ya kuwekeza kwenye michezo na maendeleo ya vipaji nchini baada ya kukabidhi vifaa vya michezo vyenye thamani ya shilingi milioni 19 kwa timu za Mashujaa kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Hafla ya kukabidhi vifaa hivyo imefanyika katika makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam, ikihudhuriwa na viongozi wa NMB pamoja na wawakilishi kutoka JWTZ. 

Vifaa hivyo vinatarajiwa kusaidia timu za Mashujaa Queen na Mashujaa Under 20 katika maandalizi ya michezo yao mbalimbali.

Meneja Mwandamizi wa Wateja Binafsi kutoka NMB, Ally Ngingite, amesema benki hiyo imekuwa na uhusiano mzuri na JWTZ kwa muda mrefu, hasa kwenye sekta ya michezo.

Amesisitiza kuwa NMB inatambua mchango wa jeshi hilo katika kukuza vipaji na kuimarisha michezo, jambo linaloleta mshikamano, afya bora na maendeleo ya kijamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utimamu wa Mwili, Michezo na Utamaduni kutoka JWTZ, Kanal David Luoga, ametoa shukrani kwa NMB kwa kuwa mdau wa kuaminika katika kukuza michezo ndani ya jeshi.

Ameeleza kuwa michezo ni njia mojawapo ya kudumisha furaha, mshikamano na afya kwa wanajeshi na jamii kwa ujumla.

Katika vifaa vilivyokabidhiwa, kuna jezi za kuchezea seti nne, gloves za magolikipa seti nne, track suit hamsini, jezi za kusafiria arobaini pamoja na sanamu za mazoezi. Vifaa hivi vitasaidia si tu kuinua morali ya wachezaji, bali pia kuongeza ubora wa maandalizi yao kuelekea mashindano mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.

Kupitia mchango huu, NMB inaendelea kujikita katika kusaidia makundi mbalimbali ya kijamii, huku ikitanguliza maendeleo ya vijana na vipaji kama sehemu ya mkakati wake wa uwajibikaji kwa jamii.





Post a Comment

0 Comments